Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushoto: Kimbunga Ian, Florida, Marekani, Septemba 2022 (Sean Rayford/Getty Images); katikati: Mama na mwana wake wakiondoka eneo la vita, Donetsk, Ukrainia, Julai 2022 (Alex Chan Tsz Yuk/SOPA Images/LightRocket via Getty Images); kulia: Watu wakipimwa ugonjwa wa COVID, Beijing, China, Aprili 2022 (Kevin Frayer/Getty Images)

ENDELEA KUKESHA!

2022: Mwaka Uliojaa Misukosuko—Biblia Inasema Nini?

2022: Mwaka Uliojaa Misukosuko—Biblia Inasema Nini?

 Katika mwaka wa 2022 tumesikia ripoti nyingi za vita, matatizo ya kiuchumi, na misiba iliyosababishwa na uharibifu wa mazingira. Biblia tu ndiyo inayoweza kueleza kwa nini mambo hayo yalitokea.

Kisababishi kikuu cha matukio ya 2022

 Matukio ya mwaka uliopita yanathibitisha hata zaidi kwamba tunaishi katika kipindi ambacho Biblia inaita “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1) Kipindi hicho kilianza mwaka wa 1914. Ona jinsi matukio ya hivi karibuni yanavyopatana na mambo ambayo Biblia ilitabiri yangetendeka wakati wetu:

 “Vita.”​—Mathayo 24:6.

  •   “2022 Mwaka Ambao Madhara ya Vita Yaikumba Ulaya kwa Mara Nyingine.” a

 Ona makala “Urusi Yashambulia Ukrainia.”

 “Upungufu wa chakula.”​—Mathayo 24:7.

  •   “2022: Mwaka wa Njaa Kali.” b

 “Magonjwa.”​—Luka 21:11.

  •   “Ugonjwa wa polio ulirudi tena, ndui ya nyani ikawa tatizo kubwa, na COVID-19 ikaendelea kusababisha madhara makubwa. Hali hizo zilionyesha jinsi magonjwa ya kuambukiza yalivyo hatari na jinsi wanadamu wanavyoweza kuangamia kwa urahisi.” c

 “Mambo yenye kuogopesha.”​—Luka 21:11.

  •   “Kupanda kwa kiwango cha joto, ukame, mioto ya msituni, na mafuriko. Majira ya kiangazi ya 2022 yatakumbukwa kwa sababu ya majanga yaliyosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa ambayo yalitokeza uharibifu, yakasababisha vifo vya maelfu ya watu, na kuwaacha mamilioni ulimwenguni pote bila makao.” d

 “Machafuko [au, “misukosuko,” maelezo ya chini].”​—Luka 21:9.

  •   “Mwaka wa 2022 kulikuwa na maandamano mengi zaidi dhidi ya serikali kwa sababu raia walikuwa na hasira kubwa iliyotokezwa na matatizo ya kiuchumi, na hasa kwa sababu ya mfumuko wa bei.” e

 Ona makala “Mfumuko wa Bei Ulimwenguni.”

Mambo yatakuwaje mwaka ujao?

 Hakuna anayejua hali zitakuwaje katika mwaka wa 2023. Tunachojua ni kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu, au serikali ya mbinguni, itabadili mambo hapa duniani. (Danieli 2:44) Serikali hiyo itaondoa kisababishi kikuu cha matatizo ya wanadamu na kuhakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatendeka duniani.​—Mathayo 6:9, 10.

 Tunakuhimiza ufuate ushauri wa Yesu Kristo na ‘kuendelea kukesha’ ili uone jinsi matukio ya ulimwengu yanavyotimiza unabii wa Biblia. (Marko 13:37) Tafadhali wasiliana nasi ili ujifunze mengi zaidi jinsi Biblia inavyoweza kukusaidia sasa na jinsi inavyoweza kukusaidia wewe na familia yako kuwa na tumaini la wakati ujao mzuri.

a AP News, “2022 Mwaka Ambao Madhara ya Vita Yaikumba Ulaya kwa Mara Nyingine,” iliandikwa na Jill Lawless, Desemba 8, 2022.

b Shirika la Chakula Duniani, “2022: Mwaka wa Njaa Kali.”

c JAMA Health Forum, “Kuishi Katika Enzi ya Majanga—Kuanzia COVID-19, Ndui ya Nyani, Polio, na Ugonjwa X,” iliandikwa na Lawrence O. Gostin, JD, Septemba 22, 2022.

d Earth.Org, “Ni Nini Kinachosababisha Mabadiliko Makubwa ya Hali ya Hewa ya Kiangazi cha 2022?” iliandikwa na Martina Igini, Oktoba 24, 2022.

e Carnegie Endowment for International Peace, “Maandamano Ulimwenguni Pote ya Mwaka 2022 Yalisababishwa na Hasira Kuhusu Uchumi,” iliandikwa na Thomas Carothers na Benjamin Feldman, Desemba 8, 2022.