Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 12

Onyesha Kwamba Una Imani ya Kweli!

Onyesha Kwamba Una Imani ya Kweli!

MUNGU anawatahadharisha watumishi wake kwamba watazamie majaribu ya imani. Neno lake linasema: “Iweni wenye kulinda. Adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Petro 5:8) Huenda Shetani akajaribu kuvunja imani yako jinsi gani?

Umewahi kupata upinzani wa aina hii?

Shetani anaweza kutumia watu wengine, hata wapendwa wako, kukushinikiza usisome Maandiko Matakatifu. Kuhusu hilo, Yesu alitabiri: “Adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mathayo 10:36) Huenda watu wa familia na marafiki wasio na nia mbaya wasijue kweli nzuri ajabu zinazopatikana katika Neno la Mungu. Au huenda wakaogopa jinsi wengine watakavyowaona. Hata hivyo, Maandiko yanasema: “Kutetemeshwa na wanadamu ndiko huleta mtego, lakini yeye anayemtegemea Yehova atalindwa.” (Methali 29:25) Ukiacha kujifunza Maandiko ili uwafurahishe wanadamu, je, hilo litamfurahisha Mungu? Bila shaka hapana! Kwa upande mwingine, tunapoonyesha imani ya kweli, Mungu hutusaidia. “Sisi si namna ya watu wanaorudi nyuma kwenye maangamizi, bali sisi ni namna ya watu walio na imani ya kuihifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:39.

Kumbuka kisa cha Dumas, kilichotajwa mapema. Mwanzoni, mke wake alimdhihaki kwa sababu ya imani yake. Lakini baadaye alijiunga naye kujifunza Neno la Mungu. Vivyo hivyo, ukiendelea kutenda mema, huenda ukawachochea marafiki na wapendwa wako kutenda mema. Katika visa vingi, mtu wa familia ‘amevutwa bila neno kupitia mwenendo ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa,’ ya yule ambaye anaonyesha imani ya kweli.—1 Petro 3:1, 2.

Shetani hujaribu kuwafanya watu wafikiri kwamba wana shughuli nyingi sana wasiweze kujifunza Maandiko. Angependa matatizo ya maisha—mahangaiko ya kibinafsi na mahangaiko kuhusu pesa—‘yalisonge neno’ ili imani yako ‘ikose kuzaa matunda.’ (Marko 4:19) Kataa maoni hayo yasiyofaa! Maandiko yanasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Ndiyo, kuendelea kujifunza mengi kumhusu Mungu na Yesu, yule Masihi, ni muhimu ili kuishi milele katika Paradiso!

Mwombe Mungu akusaidie

Mfikirie Musa aliyekuwa mmoja wa watu wa nyumba ya mfalme wa Misri. Angeweza kufuatilia mali, umashuhuri, na mamlaka. Hata hivyo, Musa alichagua “kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu badala ya kufurahia dhambi kwa muda.” Kwa nini? “Aliendelea kuwa imara kama mtu anayemwona Yeye asiyeonekana.” (Waebrania 11:24, 25, 27) Ndiyo, Musa alikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu. Alitanguliza mapenzi ya Mungu badala ya kufuatilia mambo ya kibinafsi, na Mungu akambariki sana. Ukifanya hivyo, Mungu atakubariki pia.

Huenda ukawa shabaha ya Shetani katika njia mbalimbali. Hata hivyo si lazima akunase. Neno la Mungu linatuhimiza: “Mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Unaweza kumpinga jinsi gani?

Endelea kujifunza Maandiko Matakatifu. Soma Neno la Mungu kila siku. Jifunze mafundisho yake. Tumia mashauri yake. Kwa kufanya hivyo, ‘utachukua mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,’ ambayo yatakusaidia kukinga mashambulizi ya Shetani.—Waefeso 6:13.

Shirikiana na watu wenye imani ya kweli. Watafute wengine wanaosoma, wanaojifunza, na kutumia Maandiko Matakatifu. Watu hao ‘huchocheana katika upendo na matendo mazuri, . . . wakitiana moyo.’ Watakusaidia ukue katika imani.—Waebrania 10:24, 25.

Shirikiana na wengine walio na imani

Mkaribie Yehova. Mwombe Mungu akusaidie, na umtumaini. Usisahau kamwe kwamba Mungu anataka kukusaidia. ‘Mtupie [Mungu] mahangaiko yako yote, kwa sababu yeye anakujali.’ (1 Petro 5:6, 7) “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

Shetani humdhihaki Mungu akisema kwamba hakuna mtu anayeweza kumtumikia Mungu chini ya majaribu. Hata hivyo, una nafasi ya kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo! Mungu anasema: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili nipate kumjibu anayenidhihaki.” (Methali 27:11) Ndiyo, azimia kuonyesha kwamba una imani ya kweli!