Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA SITA

Tukifa Tunaenda Wapi?

Tukifa Tunaenda Wapi?

1-3. Huenda ukauliza maswali gani kuhusu kifo, na baadhi ya dini hujibuje?

BIBLIA inatuahidi kwamba “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Katika Sura ya 5, tulijifunza kwamba fidia inatuwezesha kupata uzima wa milele. Lakini bado tunaendelea kufa. (Mhubiri 9:5) Kwa hiyo, swali ni, Tukifa tunaenda wapi?

2 Jibu la swali hilo ni muhimu hasa tunapofiwa na mtu tunayempenda. Huenda tukajiuliza: ‘Ameenda wapi? Je, anatuona? Je, anaweza kutusaidia? Je, tutamwona tena?’

3 Dini nyingi hujibu maswali hayo kwa njia tofauti. Baadhi yao hufundisha kwamba ikiwa unatenda mema utaenda mbinguni na ikiwa unatenda mabaya utaenda motoni. Nyingine hufundisha kwamba ukifa unabadilika na kuwa roho kisha unaenda kuishi na ndugu zako waliokufa. Na nyingine hufundisha kwamba baada ya kufa na kuhukumiwa, unazaliwa upya, au kuwa hai tena ukiwa na mwili tofauti, labda ukiwa mwanadamu au mnyama.

4. Ni wazo gani kuu ambalo dini nyingi hufundisha kuhusu kifo?

4 Mambo ambayo dini hufundisha hutofautiana. Hata hivyo, karibu dini hizo zote hufundisha wazo moja kuu. Zinafundisha kwamba mtu akifa, sehemu fulani ya mwanadamu huendelea kuishi. Je, ni kweli?

TUKIFA TUNAENDA WAPI?

5, 6. Tukifa tunaenda wapi?

5 Yehova anajua hali ya wafu, na ametueleza kwamba mtu akifa, uhai wake unakoma. Kifo ni kinyume cha uhai. Kwa hiyo, mtu akifa haendelei kuishi mahali pengine, hisia na mawazo yake hupotea. * Tukifa hatuwezi kuona, kusikia, wala kufikiri.

6 Mfalme Sulemani aliandika kwamba “waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.” Wafu hawawezi kupenda au kuchukia, na “hakuna kazi wala mipango wala ujuzi wala hekima Kaburini.” (Soma Mhubiri 9:5, 6, 10.) Na katika Zaburi 146:4, Biblia inatuambia kwamba, mtu akifa “mawazo yake” hupotea.

YESU ALISEMA NINI KUHUSU KIFO?

Yehova aliwaumba wanadamu ili waishi milele duniani

7. Yesu alisema nini kuhusu kifo?

7 Rafiki yake mpendwa Lazaro alipokufa, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Rafiki yetu Lazaro amelala usingizi.” Lakini Yesu hakumaanisha kwamba Lazaro alikuwa amepumzika. Yesu akaendelea kusema: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Kwa hiyo Yesu alilinganisha kifo na usingizi. Hakusema kwamba Lazaro alikuwa mbinguni au pamoja na watu wa familia yake waliokufa zamani. Wala hakusema Lazaro anateseka katika moto wa mateso au amezaliwa upya akiwa mwanadamu au mnyama. Alimaanisha kwamba ni kama Lazaro alikuwa amelala usingizi mzito. Maandiko mengine hufananisha kifo na usingizi mzito. Biblia inasema kwamba Stefano alipouawa, ‘alilala usingizi katika kifo.’ (Matendo 7:60) Pia, mtume Paulo aliandika kwamba baadhi ya Wakristo walikuwa “wamelala usingizi katika kifo.”—1 Wakorintho 15:6.

8. Tunajuaje kwamba Yehova hakuwaumba wanadamu ili wafe?

8 Je, Mungu aliwaumba Adamu na Hawa ili wafe? Hapana! Yehova aliwaumba wafurahie maisha milele wakiwa na uhai mkamilifu. Yehova aliwaumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuishi milele. (Mhubiri 3:11) Wazazi hawapendi watoto wao wazeeke na kufa na Yehova pia anahisi hivyo kutuhusu. Hata hivyo, ikiwa Yehova alituumba ili tuishi milele, kwa nini tunakufa?

KWA NINI TUNAKUFA?

9. Kwa nini Adamu na Hawa walipaswa kutii amri ya Yehova?

9 Katika bustani ya Edeni, Yehova alimwagiza Adamu hivi: “Unaweza kula matunda ya kila mti katika bustani mpaka ushibe. Lakini kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwanzo 2:9, 16, 17) Haikuwa vigumu kutii amri hiyo iliyo wazi na Yehova alikuwa na haki ya kuwaeleza Adamu na Hawa jambo linalofaa na lisilofaa. Kwa kumtii Yehova, wangeonyesha kwamba wanaheshimu mamlaka yake. Pia, utii ungeonyesha kwamba wanathamini mambo yote ambayo Yehova aliwapa.

10, 11. (a) Shetani aliwadanganyaje Adamu na Hawa? (b) Kwa nini Adamu na Hawa hawakuwa na sababu ya kutotii amri ya Mungu?

10 Inasikitisha kwamba Adamu na Hawa waliamua kutomtii Yehova. Shetani alimwuliza Hawa hivi: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Hawa akamjibu: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani: ‘Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.’”—Mwanzo 3:1-3.

11 Ndipo Shetani akamwambia: “Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” (Mwanzo 3:4-6) Shetani alitaka Hawa afikiri kwamba angeweza kujiamulia mwenyewe mambo mema na mabaya. Pia, alimdanganya kuhusu matokeo ya kutomtii Mungu. Shetani alimwambia Hawa kwamba hangekufa, hivyo akala tunda na baadaye akampa mume wake. Adamu na Hawa walijua kabisa kwamba Mungu aliwakataza kula matunda hayo. Hivyo walipokula tunda hilo, walikosa kutii amri rahisi na iliyo wazi. Jambo hilo lilionyesha wazi kwamba walimdharau Baba yao mpendwa wa mbinguni. Hawakuwa na sababu ya kutotii amri ya Mungu!

12. Kwa nini inasikitisha kwamba Adamu na Hawa walimwasi Yehova?

12 Inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza hawakumheshimu Muumba wao! Ungehisije ikiwa umejitahidi kuwalea vizuri watoto wako lakini baadaye wanakuasi na kufanya mambo tofauti kabisa na uliyowafundisha? Je, hungeumia sana?

Adamu aliumbwa kwa mavumbi naye alirudi mavumbini

13. Yehova alimaanisha nini aliposema “utarudi mavumbini”?

13 Walipomwasi Mungu, Adamu na Hawa walipoteza fursa ya kuishi milele. Yehova alimwambia Adamu hivi: “Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Soma Mwanzo 3:19.) Jambo hilo lilimaanisha kwamba Adamu angekuwa mavumbi kana kwamba hakuwahi kuishi. (Mwanzo 2:7) Baada ya Adamu kutenda dhambi alikufa na hayupo tena.

14. Kwa nini tunakufa?

14 Kama Adamu na Hawa wangemtii Mungu, wangekuwa hai mpaka leo. Lakini walipokataa kumtii, walitenda dhambi na hatimaye wakafa. Dhambi ni kama ugonjwa hatari tuliorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Sote huzaliwa tukiwa na dhambi na ndiyo sababu tunakufa. (Waroma 5:12) Lakini hilo halikuwa kusudi la Mungu alipowaumba wanadamu. Mungu hakutaka wanadamu wafe, ndiyo sababu Biblia hukiita kifo “adui.”—1 Wakorintho 15:26.

UKWELI UNATUWEKA HURU

15. Kwa nini kujua ukweli kuhusu kifo hutuweka huru?

15 Kujua ukweli kuhusu wafu hutuweka huru na maoni yaliyopotoka. Biblia inatufundisha kwamba wafu hawahisi maumivu wala huzuni. Hatuwezi kuwasiliana nao. Hatuwezi kuwasaidia, wala hawawezi kutusaidia. Hawawezi kutudhuru, hivyo hatupaswi kuwaogopa. Hata hivyo, dini nyingi hufundisha kwamba wafu wanaendelea kuishi mahali fulani na tunaweza kuwasaidia kwa kuwapa viongozi wa kidini au watakatifu kiasi fulani cha pesa ili wawaombee. Lakini tukijua ukweli kuhusu kifo hatutadanganywa.

16. Dini nyingi hufundisha uwongo gani kuhusu wafu?

16 Shetani anatumia dini za uwongo kutupotosha na kufanya tuhisi kwamba wafu wako hai. Kwa mfano, baadhi ya dini hufundisha kwamba tunapokufa, roho huendelea kuishi mahali fulani. Je, dini yako imekufundisha hivyo au je, inakufundisha mambo ambayo Biblia hufundisha kuhusu wafu? Shetani anatumia uwongo kuwatenganisha watu na Yehova.

17. Kwa nini fundisho la moto wa mateso linamshushia heshima Yehova?

17 Mambo ambayo dini nyingi hufundisha yanatisha. Kwa mfano, baadhi ya dini hufundisha kwamba Mungu huwatesa watu waovu motoni milele. Uwongo huo humshushia heshima Yehova. Hawezi kamwe kuwatesa hivyo wanadamu! (Soma 1 Yohana 4:8.) Ungehisije ikiwa mzazi anamwadhibu mtoto wake kwa kumchoma mikono kwa moto? Bila shaka utamwona kuwa mwenye ukatili sana. Hata, hungependa awe rafiki yako. Hivyo ndivyo Shetani anavyotaka tuhisi kumhusu Yehova!

18. Kwa nini hatupaswi kuwaogopa wafu?

18 Baadhi ya dini hufundisha kwamba watu wakifa, wanabadilika na kuwa viumbe wa roho. Dini hizo hufundisha kwamba watu wanapaswa kuwaheshimu na kuwaogopa roho hao kwa sababu wanaweza kuwa rafiki au maadui. Watu wengi wanaamini uwongo huo. Wanawaogopa wafu, kwa hiyo wanawaabudu badala ya kumwabudu Yehova. Kumbuka kwamba wafu hawahisi chochote, hivyo basi hatupaswi kuwaogopa. Yehova ndiye aliyetuumba. Yeye ndiye Mungu wa kweli, na tunapaswa kumwabudu yeye peke yake.—Ufunuo 4:11.

19. Kuna faida gani kujua ukweli kuhusu kifo?

19 Kujua ukweli kuhusu kifo, hutuweka huru kutokana na mafundisho ya uwongo. Pia, ukweli huo unatusaidia kuelewa vizuri ahadi za Yehova za wakati ujao.

20. Tutajifunza nini katika sura inayofuata?

20 Miaka mingi iliyopita, mtumishi wa Mungu, Ayubu, aliuliza hivi: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” (Ayubu 14:14) Je, kweli mtu aliyekufa anaweza kufufuka? Mungu anatupatia jibu zuri sana katika Biblia. Tutajifunza jambo hilo katika sura inayofuata.

^ fu. 5 Baadhi ya watu huamini kwamba roho huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Ili kupata habari zaidi, tafadhali soma Maelezo ya Ziada 17 na 18.