Hamia kwenye habari

Walisimama na Kusaidia

Walisimama na Kusaidia

Siku moja yenye baridi kali sana, Bob alikuwa akiendesha gari lake jijini Alberta, Kanada, kwa mwendo wa kilomita 100 kwa saa wakati ambapo gurudumu la nyuma la gari lake lilipopasuka. Mwanzoni Bob hakujua kilichokuwa kimetokea, kwa hiyo, akaamua kuendelea kuendesha gari hadi nyumbani kwani alikuwa umbali wa kilomita tano tu.

Bob alieleza kilichotokea baada ya hapo katika barua aliyoandika na kuituma kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo. Aliandika hivi: “Vijana watano waliokuwa katika gari moja walikaribia gari langu na kushusha kioo chao. Waliniambia kwamba gurudumu la gari langu lilikuwa limepasuka. Tuliegesha magari pembeni mwa barabara nao wakasema watanibadilishia. Hata sikujua ikiwa nilikuwa na gurudumu la kubadilishia au ikiwa nilikuwa na jeki ya kuinua gari. Nilipoketi kando ya barabara katika kiti changu cha magurudumu, waliingia chini ya gari langu, wakatoa gurudumu la kubadilishia pamoja na jeki, kisha wakabadili gurudumu hilo. Kulikuwa na baridi kali na theluji ilikuwa ikishuka kwa kasi. Ingawa walikuwa wamevalia vizuri, walibadili gurudumu hilo na kuniwezesha niondoke. Nisingaliweza kufanya hivyo bila msaada.

“Ninawashukuru sana hao vijana watano Mashahidi walionisaidia. Walikuja katika eneo hilo kuwatembelea watu nyumbani kwao na kuwahubiria. Kwa kweli, vijana hao hawakuhubiri tu, bali walitenda kama walivyokuwa wakihubiri. Ikiwa hawangenisaidia, ningalipatwa na hali ngumu sana, nami ninawashukuru sana. Nani angalijua kwamba kulikuwa na malaika kama hao barabarani siku hiyo?”