Hamia kwenye habari

Kuhitimu kwa Darasa la 136 la Shule ya Biblia ya Gileadi

Kuhitimu kwa Darasa la 136 la Shule ya Biblia ya Gileadi

Jumamosi, Machi 8, 2014, wanafunzi wa darasa la 136 la shule ya Gileadi walihitimu baada ya kumaliza mtaala wa miezi mitano wa kujifunza Biblia. Shule hiyo huwazoeza wahudumu wenye uzoefu ili waweze kuwa na matokeo zaidi katika huduma yao na vilevile wawaimarishe Mashahidi wenzao katika imani. Wasikilizaji 11, 548 walihudhuria programu hiyo ya kuhitimu. Baadhi yao walikuwepo kwenye kituo cha elimu cha Mashahidi wa Yehova huko Patterson, New York, na wengine waliunganishwa kupitia Intaneti katika maeneo mbalimbali nchini Kanada, Jamaika, Puerto Riko, na Marekani.

“Iweni na Mtazamo Huu wa Akili Ndani Yenu.” David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo. Maneno yake ya ufunguzi yalitegemea Wafilipi 2:5-7: “Iweni na mtazamo huu wa akili ndani yenu.” Yesu alipokuwa duniani, hakuzingatia cheo, lakini alijitoa kikamili na kwa unyenyekevu kufanya kazi ya Mungu.

Kwa mfano, Yesu alikataa vishawishi vyote vya Ibilisi kwa kutumia maneno “Imeandikwa,” akinukuu hotuba ambayo Musa alikuwa amewatolea Waisraeli. (Mathayo 4:​4, 7, 10; Kumbukumbu la Torati 6:​13, 16; 8:3) Hata ingawa Yesu angeweza kusema kwa kutumia mamlaka yake mwenyewe akiwa Mwana wa Mungu aliyetiwa mafuta, kwa unyenyekevu alionyesha kwamba anaheshimu kazi ya Musa. Vivyo hivyo, tunapaswa kutambua uwezo wa wengine na tuwapongeze mara nyingi.

Pia, Ndugu Splane alikazia jinsi Yesu alivyoonyesha mtazamo wa akili unaofaa mwishoni mwa kipindi chake cha mazoezi duniani. Yesu alisema hivi katika sala: “Nimekutukuza duniani, nikiwa nimemaliza kazi ambayo umenipa niifanye. Kwa hiyo sasa wewe, Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:​4, 5) Yesu hakuomba mapendeleo ya ziada. Ombi lake lilikuwa kwamba arudishiwe cheo alichokuwa nacho kabla ya kuja duniani, yaani, anaporudi mbinguni ‘arudishwe kazi yake ya awali.’ Vivyo hivyo, wahitimu wa Gileadi wanapaswa kumwiga Yesu kwa kukazia fikira kazi yao badala ya mapendeleo, yaani, waridhike hata wasipopata mapendeleo ya ziada watakaporudi katika migawo yao.

“Jidhabihu Bila Kujuta.” William Malenfant, msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji ya Baraza Linaloongoza, aliwatia moyo wanafunzi wafuate mfano wa kujidhabihu uliowekwa na mtume Paulo. Badala ya kutazama nyuma na kuangalia mambo aliyokuwa ameacha kwa ajili ya utumishi wa Mungu, Paulo alisema: “Nayasahau mambo ya nyuma na kujinyoosha kwenda mbele kuelekea mambo yaliyo mbele.”​—Wafilipi 3:13, 14.

Wanafunzi wanapojidhabihu bila kujuta, watakuwa wakiwaiga watumishi waaminifu wa kale na wa leo. Ndugu Malenfant alimnukuu Dada Clara Gerber Moyer, ambaye alianza kumtumikia Yehova alipokuwa mtoto. Aliandika hivi: “Ni pendeleo lililoje kutazama nyuma miaka zaidi ya 80 ya utumishi wa kujitoa kwa Mungu—bila hata kujuta! Kama ningeweza kuishi maisha yangu tena, ningeishi vivyo hivyo.”

“Kuhubiri Kuhusu Ufalme Pamoja na Malaika Kama Malaika.” Gerrit Lösch, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliwasaidia wanafunzi kuthamini mapendeleo mawili ambayo wale wanaohubiri wanapata. Kwanza, wanatumika kama malaika wa Mungu wanapotangaza ujumbe wake wa habari njema ya Ufalme, kwa sababu katika Biblia neno “malaika” katika Kiebrania na Kigiriki linaweza kutafsiriwa “mjumbe.” Pili, wanafunzi wanahubiri habari njema chini ya uongozi wa malaika, kama vile mwanafunzi Filipo alivyofanya.​—Matendo 8:​26-​35.

Ndugu Lösch alisimulia mambo kadhaa ambayo Mashahidi wa Yehova wamejionea katika kazi yao ya kuhubiri kuhusu Ufalme. Kwa mfano, Shahidi mmoja nchini Mexico anayeitwa Gabino, ana kawaida ya kubisha mlango mara moja au mbili tu, lakini aliamua kubisha mlango fulani mara nne. Mwanamume aliyefungua mlango alimwambia Gabino kwamba alikuwa karibu kujiua. Mwanamume huyo alisema hivi: “Ulipobisha mara ya nne, kamba ilikuwa shingoni. Lakini niliiondoa ili nifungue mlango. Asante kwa kuendelea kubisha. Ikiwa hungefanya hivyo, ningejinyonga.”

Ingawa huenda nyakati nyingine mambo kama hayo hutokea kwa sadfa tu, tunajua kwamba hali haiwi hivyo nyakati zote. Mambo kama hayo huthibitisha kwamba malaika wa Mungu wanaongoza kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.​—Ufunuo 14:6.

“Mwenye Kuheshimika Atabarikiwa.” Michael Burnett, mwalimu wa Gileadi, alitoa hotuba yenye kichwa hicho akitumia mfano wa Yabesi, mzao wa Yuda, ambaye alikuwa mwenye “kuheshimika kuliko ndugu zake.” Yabesi alisali hivi: “Hakika ukinibariki na kwa kweli upanue eneo langu na mkono wako uwe pamoja nami, nawe uniokoe kutoka katika msiba.”​—1 Mambo ya Nyakati 4:9, 10.

Wanafunzi wanaweza kuiga mfano wenye kuheshimika wa Yabesi kwa kutaja mambo hususa wanapotoa sala, hasa kwa kumwomba Mungu awasaidie watimize kusudi la mazoezi waliyopata katika shule ya Gileadi. Pia wanaweza kumwomba Mungu awalinde misiba inapotokea, si kwa kuzuia wasipatwe na madhara, bali awasaidie wasilemewe na huzuni au madhara yanayosababishwa na uovu. Mungu alijibu sala ya Yabesi, naye Mungu atajibu sala ya wanafunzi hao wa Gileadi.

“Msiuzime Moto Wenu.” Mark Noumair, mwalimu wa Gileadi ambaye pia ni msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji, alitoa hotuba iliyotegemea 1 Wathesalonike 5:​16-​19. Kama tu moto halisi unavyohitaji mafuta, oksijeni, na joto ili uendelee kuwaka, wanafunzi wanaweza kutumia mambo matatu ili waendelee kuwa na uchangamfu katika huduma yao.

Kwanza, “shangilieni sikuzote.” (1 Wathesalonike 5:​16) Wanafunzi wanaweza kujipatia shangwe kwa kutafakari baraka ya kuwa na kibali cha Yehova​—na kufanya hivyo kutawachochea kudumisha uchangamfu. Pili, “salini bila kuacha.” (1 Wathesalonike 5:​17) Sala ni kama oksijeni inayohakikisha kwamba moto unaendelea kuwaka. Tunapaswa kuongeza urefu wa sala zetu, na kummiminia Mungu moyo wetu. Tatu, “kuhusiana na kila jambo toeni shukrani.” (1 Wathesalonike 5:​18) Moyo wenye shukrani hufanya tuwe na uhusiano wenye uchangamfu pamoja na Yehova na ndugu zetu. Ndugu Noumair alisema, “Dumisheni mioyo yenye uchangamfu na uthamini, na mwepuke kuwa na roho ya uchambuzi.”

“Kumsifu Yehova Pamoja na Mbingu.” Sam Roberson, mwalimu wa shule za kitheokrasi, alitoa utangulizi wa hotuba yake kwa kutumia maneno ya Biblia yanayoonyesha kwamba jua, mwezi, na nyota zinamsifu Yehova. (Zaburi 19:1; 89:37; 148:3) Alisema kwamba wanafunzi wamepata pia pendeleo la kumsifu Yehova, kisha akawakaribisha waigize mambo waliyoona hivi karibuni walipokuwa katika kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, mwanafunzi fulani alisimamisha gari alilokuwa akiendesha ili mwanamume fulani aliyekuwa katika kiti cha magurudumu aweze kuvuka barabara. Mwanamume huyo alipoonyesha uthamini kwa tendo hilo ndugu yetu alimshukuru. Walianza mazungumzo, na mwanamume huyo akakubali kujifunza Biblia bila malipo. Katika majuma yaliyofuata, mwanafunzi huyo wa Gileadi aliendelea kujifunza naye Biblia na akafaulu pia kuwahubiria watu wengine waliomtembelea mwanamume huyo. Kwa ujumla, watu wengine saba walianza kujifunza Biblia kutokana na mazungumzo hayo ya kwanza.

“Mfanywe Kuwa na Uwezo Zaidi Kupitia Elimu ya Mungu.” Donald Gordon, msaidizi wa Halmashauri ya Utangazaji, aliwahoji waume wawili na wake zao waliokuwa wanafunzi wa darasa hilo. Ndugu mmoja kati yao alikumbuka kwamba andiko la Waefeso 3:​16-​20 lilizungumziwa sana katika shule yote. Hilo liliwasaidia wanafunzi ‘wafanywe kuwa na uwezo’ wanapoendelea kusitawisha sifa ya unyenyekevu, kuwa wenye kufikika na kutambua kwamba bado Yehova ana kazi nyingi kwa ajili ya Mashahidi wote. Dada mmoja alisema kwamba alifurahia sana jinsi mwalimu mmoja wa Gileadi alivyowatia moyo wanafunzi wasiwe kama samaki mkubwa katika bakuli dogo la maji ambaye hana nafasi ya kukua, bali wawe kama samaki mdogo katika bahari kubwa. Dada huyo alisema: “Nilijifunza kwamba ninapojiendesha kama aliye mdogo zaidi katika tengenezo la Yehova, bila shaka Yehova atanisaidia kukua kiroho.”

“Yehova na Akukumbuke kwa Ajili ya Wema.” Mark Sanderson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi ya programu ya kuhitimu, akitegemeza kichwa cha hotuba yake kutokana na maneno ya sala ya Nehemia: “Unikumbuke kwa ajili ya wema, Ee Mungu wangu.” (Nehemia 5:​19; 13:31) Nehemia hakuwa na wasiwasi eti Yehova angemsahau na kusahau kazi aliyofanya katika utumishi wa Mungu. Badala yake, alikuwa akimwomba Mungu amkumbuke kwa upendo na ambariki.

Vivyo hivyo, wanafunzi wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawakumbuka kwa ajili ya wema ikiwa watatumia mambo ya msingi waliyojifunza wakiwa Gileadi. Kwa mfano, wanapaswa kuhakikisha kwamba upendo wao wa kutoka moyoni ndio unapaswa kuwa kichocheo kikuu cha kumwabudu Yehova. (Marko 12:30) Abrahamu alimpenda Yehova kwa moyo wake wote, na Mungu akamkumbuka kwa upendo. Hata miaka elfu moja baada ya Abrahamu kufa, Mungu alimrejelea kuwa “rafiki yangu.”​—Isaya 41:8.

Kisha, ndugu Sanderson aliwakumbusha wanafunzi wawapende majirani wao, hasa ndugu na dada zao Wakristo. (Marko 12:31) Kama yule Msamaria mwema, ambaye “alijifanya kuwa jirani kwa mtu aliyeanguka katikati ya wanyang’anyi,” wanapaswa kuchukua hatua ya kwanza kuwafikia wale wanaohitaji msaada. (Luka 10:36) Ili kufafanua jambo hilo, Ndugu Sanderson alizungumza kuhusu mfano uliowekwa na Nicholas Kovalak, mhitimu wa Gileadi ambaye aliwahi kutumika akiwa mwangalizi wa wilaya. Ndugu Kovalak alijulikana kuwa mtu mchangamfu na aliyewapenda watu. Pindi moja alimwambia mwangalizi anayesafiri pamoja na mke wake maneno haya, alipokuwa akiwatia moyo wawe na bidii katika kazi ya kuhubiri, “Anzeni mapema kila siku, mapema kila juma, mapema kila mwezi, mapema kila mwaka.” Lakini baada ya kuangalia utendaji wa mke wa mwangalizi huyo kwa siku kadhaa, alimwambia: “Sahau maneno niliyokuambia. Tayari unafanya kazi kwa bidii. Punguza mwendo, ili uweze kufanya kazi hii kwa muda mrefu.” Shauri lake lenye fadhili na huruma limemsaidia dada huyo aendelee na utumishi wa wakati wote kwa makumi ya miaka.

Mwishowe, Ndugu Sanderson aliwatia moyo wanafunzi watimize kusudi la mazoezi waliyopokea kwa kuwafundisha na kuwazoeza wengine. (2 Timotheo 2:2) Aliwahimiza wanapoendelea na migawo yao, wajitahidi kuwaimarisha na kuwategemeza ndugu zao, nao watakuwa na uhakika kwamba Yehova atawakumbuka kwa ajili ya wema.​—Zaburi 20:​1-5.

Umalizio. Baada ya wanafunzi kupokea diploma zao, mhitimu mmoja alisoma barua ya shukrani kwa niaba ya darasa lote. Wanafunzi 15 wa darasa hilo walimalizia programu hiyo kwa kuimba wimbo namba 123 wenye kichwa “Wachungaji—Zawadi Katika Wanadamu” kutoka katika kitabu Mwimbieni Yehova.