Ona video zinazopatikana

Amri Kumi za Mungu Njo Nini?

Amri Kumi za Mungu Njo Nini?

Jibu ya Biblia

 Amri Kumi ni sheria zenye Mungu alipatia taifa ya Israeli ya zamani. Zile amri zinaitwa pia Maneno Kumi, yenye ni tafsiri ya neno kwa neno ya maneno ya Kiebrania ʽaseʹreth had·deva·rimʹ. Ile maneno inapatikana mara tatu mu Pentateuki (Torati), ni kusema, vitabu tano vya kwanza vya Biblia. (Kutoka 34:28; Kumbukumbu la Torati 4:13; 10:4) Maneno yenye kufanana na ile mu Kigiriki ni deʹka (kumi) loʹgous (maneno), na inatokeza neno “Dekaloge.”

 Mungu aliandika Amri Kumi juu ya mabamba mbili ya majiwe na aliipatia nabii wake Musa ku Mulima Sinai. (Kutoka 24:12-​18) Zile Amri Kumi zinapatikana mu kitabu ya Kutoka 20:1-​17 na Kumbukumbu la Torati 5:6-​21.

 Liste ya Amri Kumi

  1.   Umuabudu Yehova Mungu tu.​—Kutoka 20:3.

  2.   Haupaswe kuabudu sanamu.​—Kutoka 20:4-6.

  3.   Haupaswe kutumia jina ya Mungu kwa njia yenye haifae.​—Kutoka 20:7.

  4.   Ushike Sabato.​—Kutoka 20:8-​11.

  5.   Uheshimie wazazi wako.​—Kutoka 20:12.

  6.   Usiue.​—Kutoka 20:13.

  7.   Usifanye uzinifu.​—Kutoka 20:14.

  8.   Usiibe.​—Kutoka 20:15.

  9.   Usitoe ushahidi wa uongo.​—Kutoka 20:16.

  10.   Usitamani.​—Kutoka 20:17.

 Juu ya nini liste za Amri Kumi ziko tofauti?

 Biblia haionyeshe namba ya kila amri. Njo maana, kuko mawazo tofauti juu ya namna Amri Kumi zinapaswa kupangwa. Liste yenye kuwa juu inaonyesha namna watu wanazoea kupanga zile amri. Lakini, wengine wanapanga Amri Kumi mu njia tofauti. Wakati wanazipanga, tofauti inakuwaka ku amri ya kwanza, ya pili, na ya mwisho. *

 Kusudi ya Amri Kumi ilikuwa nini?

 Amri Kumi zilikuwa sehemu ya sheria ya Musa. Ile Sheria ilikuwa na amri zaidi ya 600 na ilifanyiza agano yenye Mungu alifanya pamoya na taifa ya Israeli ya zamani. (Kutoka 34:27) Mungu aliahidi watu wa Israeli kama wangebarikiwa ikiwa wangetii Sheria ya Musa. (Kumbukumbu la Torati 28:1-​14) Lakini, kusudi kubwa ya ile Sheria ilikuwa kusaidia Waisraeli wajitayarishe juu ya kupokea Masiya mwenye aliahidiwa ao Kristo.​—Wagalatia 3:24.

 Wakristo wanapaswa kushika Amri Kumi?

 Hapana. Mungu alipatia taifa ya Israeli ya zamani sheria yake, kutia ndani Amri Kumi. (Kumbukumbu la Torati 5:2, 3; Zaburi 147:19, 20) Wakristo hawalazimike kushika Sheria ya Musa, na hata Wakristo Wayahudi ‘walifunguliwa kutoka katika Sheria.’ (Waroma 7:6) * Sheria ya Musa ilibadilishwa na “sheria ya Kristo,” yenye inatia ndani mambo yote yenye Yesu aliagiza wafuasi wake wafanye.​​—Wagalatia 6:2; Matayo 28:19, 20.

 Amri Kumi ziko na faida leo?

 Ndiyo. Juu Amri Kumi zinaonyesha mawazo ya Mungu, tunaweza kupata faida kwa kujifunza zile Amri Kumi. (2 Timoteo 3:16, 17) Zile Amri Kumi zinategemea kanuni za Biblia zenye kutegemeka zenye haziwezi kupitwa na wakati. (Zaburi 111:7, 8) Kusema kweli, kanuni za mingi zenye zinategemea Amri Kumi njo musingi wa mafundisho yenye mara mingi inaitwa Agano Jipya.​—Ona “ Kanuni za Agano Jipya Zenye Zinatoka mu Amri Kumi.”

 Yesu alifundisha kama Sheria yote ya Musa, kutia ndani Amri Kumi, yote inategemea amri mbili za musingi. Alisema hivi: “‘Unapaswa kumupenda Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote. Hii ndiyo amri kubwa zaidi na ya kwanza. Ya pili kama hiyo, ni hii, ‘Unapaswa kumupenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Sheria yote na Manabii vinategemea amri hizo mbili.” (Matayo 22:34-​40) Kwa hiyo, hata kama Wakristo hawalazimike kushika Sheria ya Musa, wanapaswa kumupenda Mungu na kupenda majirani wao.​—Yohana 13:34; 1 Yohana 4:20, 21.

  Kanuni za Agano Jipya Zenye Zinatoka mu Amri Kumi

Kanuni

Kwenye Inapatikana mu Agano Jipya

Umuabudu Yehova Mungu tu

Ufunuo 22:8, 9

Haupaswe kuabudu sanamu

1 Wakorinto 10:14

Heshimia jina ya Mungu

Matayo 6:9

Umuabudu Mungu kila mara

Waebrania 10:24, 25

Heshimia wazazi wako

Waefeso 6:1, 2

Usiue

1 Yohana 3:15

Usifanye uzinifu

Waebrania 13:4

Usiibe

Waefeso 4:28

Usitoe ushahidi wa uongo

Waefeso 4:25

Usitamani

Luka 12:15

^ Kwa maoni ya Wayahudi, “Kutoka 20: 2 njo ‘amri’ ya kwanza na mustari wa 3-6 inafanyiza amri moya, ni kusema, amri ya pili.” (The Jewish Encyclopedia) Ku ngambo ingine, Wakatoliki wanaona Kutoka 20 mustari wa 1-6 kuwa amri moya. Kwa hiyo, amri yenye inakataza kutumia mubaya jina ya Mungu njo inakuwa amri ya pili. Juu hesabu ya Amri Kumi ienee, wanagawanya amri ya mwisho katika amri mbili, yenye inakataza kutamani bibi ya jirani, na yenye inakataza kutamani vitu vya mwingine.

^ Waroma 7:7 inatumia amri ya kumi sawa vile mufano wa “Sheria.” Ile inaonyesha kama Amri Kumi iko ndani ya Sheria ya Musa.