Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

NJIA YA MAISHA YENYE FURAHA

Kutosheka na Ukarimu

Kutosheka na Ukarimu

NI MARA NGAPI UMEKWISHA KUSIKIA WATU WANASEMA KUWA FURAHA NA MAISHA YA MUZURI VINALETWA NA VITU VYA KIMWILI AO MALI? Mawazo hayo yanafanya mamilioni ya watu watumike saa nyingi zenye kuchokesha ili kupata feza nyingi zaidi. Lakini, feza na vitu vya kimwili vinaleta furaha yenye kuendelea? Ukweli wa mambo unaonyesha nini?

Kulingana na gazeti Journal of Happiness Studies, wakati tu tunatimiza mahitaji yetu ya musingi, kuwa na feza nyingi hakufanye tukuwe wenye furaha zaidi ao kujisikia muzuri zaidi. Tatizo haiko feza. Gazeti Monitor on Psychology linasema kwamba ‘kufuatilia sana [feza] ndilo jambo linafanya mutu akose furaha.’ Maneno hayo yanapatana sana na shauri lenye Biblia ilitoa kumepita miaka 2000 hivi: “Kupenda pesa [ao, feza] ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi [ao, kujikaza sana] kufikia upendo huo wengine . . . wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Maumivu hayo yanatia ndani nini?

WASIWASI NA KUKOSA USINGIZI KWA SABABU MUTU ANAPASWA KULINDA MALI YAKE. ‘Usingizi wa mutumishi ni mutamu, bila kujali [ao, kuhangaika] kama anakula kidogo ao kingi; lakini wingi alio nao tajiri haumuruhusu kulala.’​—Mhubiri 5:12.

KUVUNJIKA MOYO WAKATI MUTU HAPATE FURAHA YENYE ALITUMAINIA. Kwa upande moja, jambo hilo linatokea kwa sababu upendo wa feza ni tamaa yenye haiwezi kuisha. ‘Anayependa feza hatatosheka na feza, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.’ (Mhubiri 5:10) Pia, tamaa ya kupata mali inachochea mutu azarau mambo ya maana yenye yanaleta furaha, kama vile wakati wa maana sana wenye mutu anaweza kupitisha pamoja na familia na marafiki zake ao wakati wenye anaweza kutumia ili kufanya mambo ya kiroho.

HUZUNI NA KUVUNJIKA MOYO WAKATI FEZA ZINAPOTEZA MAFAA AO ZINAPOTEA KATIKA BIASHARA. ‘Usijitaabishe [ao, usijichokeshe] kutafuta utajiri. Acha kutegemea uelewaji wako mwenyewe. Je, umeukazia macho, nao si kitu? Kwa maana hakika huo unajifanyia mabawa kama yale ya tai na kuruka.’​—Methali 23:4, 5.

SIFA ZENYE KULETA FURAHA

KUTOSHEKA. ‘Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote inje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutarizika [ao, tutatosheka] na vitu hivyo.’ (1 Timotheo 6:7, 8) Watu wenye kutosheka mara nyingi hawana tabia ya kunungunika ao kulalamika, na hilo linawasaidia kuepuka wivu. Na kwa sababu hawana tamaa ya kupata vitu vingi kuliko uwezo wao, wanajiepusha na wasiwasi na mahangaiko yenye hayana maana.

UKARIMU. “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Watu wenye kuwa na roho ya kutoa wako na furaha kwa sababu wanapenda kufurahisha wengine, hata kama kile wanaweza kutoa tu ni wakati na nguvu yao. Mara nyingi wanapata kwa uwingi mambo yenye feza haiwezi kuuza, ni kusema, upendo, heshima, na marafiki wa kweli wenye wanawatolea pia kwa ukarimu!​—Luka 6:38.

KUTIA WATU PA NAFASI YA KWANZA KULIKO VITU. ‘Afazali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ngombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.’ (Methali 15:17) Andiko hili linatufundisha nini? Kuwa na urafiki wenye upendo pamoja na wengine ni jambo la maana zaidi kuliko utajiri. Na kama vile tutaona kisha, upendo ni wa lazima ili kuwa na furaha.

Sabina, mwanamuke mumoja mwenye kuishi katika Amerika ya Kusini, alijifunza kuwa kanuni za Biblia ni za maana sana. Bwana yake alimuacha, kwa hiyo Sabina alipaswa kupiganisha ili kupata mambo yenye alikuwa nayo lazima kwa ajili yake na watoto wake wawili wanamuke. Alikuwa na kazi mbili na alipaswa kuamuka kila siku na saa 10:00 ya usiku (4:00). Hata kama Sabina alikuwa na mambo mengi ya kufanya, aliamua kujifunza Biblia. Alipata matokeo gani?

Hali ya feza haikubadilika kabisa. Lakini maisha yake yalibadilika kwa njia kubwa! Kwa mufano, alipata furaha yenye inatokea wakati mutu anatimiza mahitaji yake ya kiroho. (Mathayo 5:3) Alipata marafiki wa kweli kati ya waamini wenzake. Na alipata furaha ya kutoa kwa kuwaelezea wengine mambo yenye alijifunza.

Biblia inasema hivi: ‘Hekima inaonyeshwa kuwa yenye uadilifu [ao, haki] kwa matendo yake.’ (Mathayo 11:19) Kulingana na maneno hayo, hekima ya kuwa mwenye kutosheka, mukarimu na kutia watu pa nafasi ya kwanza kuliko vitu vya kimwili ni ya maana sana!