Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAWAZO YA BIBLIA

Kuonyesha Shukrani

Kuonyesha Shukrani

Mambo mengi yanahakikisha kwamba kuonyesha shukrani kunaleta faida nyingi juu ya afya yetu ya kimwili, ya akili, na ya moyoni. Kwa hiyo, kuonyesha shukrani kunapaswa kuwa sehemu ya maisha yetu ya kila siku.

Namna gani kuonyesha shukrani kunatuletea faida?

MAMBO YENYE WANGANGA WANASEMA:

Habari moja ya kitabu Harvard Mental Health Letter inaonyesha kwamba “kuko uhusiano mukubwa kati ya kuonyesha shukrani na kuwa na furaha kubwa. Kuonyesha shukrani kunasaidia watu wakuwe na mawazo yenye kufaa, wafurahie mambo mazuri yenye walifanya, wafanye afya yao ikuwe muzuri zaidi, wavumilie magumu, na wakuwe na uhusiano muzuri na watu.”

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Biblia inatutia moyo kukomalisha roho ya kuonyesha shukrani. Mutume Paulo mwenye alikuwa mufano muzuri wa kuonyesha shukrani, aliandika hivi: ‘Mujionyeshe kuwa wenye shukrani.’ Kwa mufano, ‘alimushukuru Mungu bila kuacha’ kwa sababu watu walikubali ujumbe wenye aliwahubiria. (Wakolosai 3:15; 1 Wathesalonike 2:13) Furaha ya kweli haitokane tu na kusema aksanti wakati unataka, lakini inatokana na kuwa na moyo wenye shukrani sikuzote. Hilo linatulinda ili tusikuwe na wivu, kinyongo, na tabia ya kujisikia kwamba kila kitu wanatufanyia ni haki yetu; mambo hayo yanaweza kufanya watu wasitukaribie na kufanya tupoteze furaha yetu katika maisha.

Muumbaji wetu ametuwekea mufano muzuri kwa kuonyesha shukrani, hata kwa wanadamu! Andiko la Waebrania 6:10 linasema hivi: ‘Mungu hakose kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ Muumbaji wetu anaona kwamba kuwa bila shukrani ni kukosa uadilifu, ao haki.

‘Mushangilie sikuzote. Kuhusiana na kila jambo mutoe shukrani.’1 Wathesalonike 5:16, 18.

Namna gani kuonyesha shukrani kunafanya uhusiano wetu na wengine ukuwe muzuri zaidi?

YALE AMBAYO MAMBO UMEKWISHA KUJIONEA YANAKUFUNDISHA:

Wakati tunaonyesha shukrani kutoka moyoni, ikuwe kwa ajili ya zawadi, neno nzuri, ao musaada, tunafanya mutu mwenye alifanya hivyo ajisikie kuwa wa maana na mwenye kupendwa. Hata watu wenye hatujue wanafurahi wakati tunawashukuru kutoka moyoni kwa sababu ya tendo nzuri, kama vile kufungua mulango.

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Yesu alisema hivi: ‘Mukuwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwangia katika mufuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika.’ (Luka 6:38) Tufikirie mufano wa Rose, mutoto mumoja kiziwi mwenye kuishi katika Vanuatu, kisiwa cha Pasifiki ya Kusini.

Rose alienda kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova, lakini haikumuletea faida kabisa kwa sababu yeye ao mutu mwengine katika kutaniko hakujua luga ya ishara. Wakati ndugu moja na bibi yake wenye kujua muzuri kabisa luga ya ishara walitembelea kutaniko lao na kuona tatizo hilo, walianzisha masomo ya luga ya ishara. Rose alikuwa mwenye shukrani sana. Alisema hivi: “Ninafurahi kuwa na marafiki wengi wenye kunipenda.” Kuona namna anaonyesha shukrani na namna anatoa maelezo kwenye mikutano kunaletea furaha kubwa ndugu na bibi yake wenye walimusaidia. Rose anafurahia pia bidii ya wengine ya kujifunza luga ya ishara ili waweze kuzungumuza naye.—Matendo 20:35.

‘Yule anayetoa shukrani zikiwa zabihu yake ndiye anayemutukuza [Mungu].’—Zaburi 50:23.

Namna gani tunaweza kukomalisha roho ya kuonyesha shukrani?

MAMBO BIBLIA INASEMA:

Kuna uhusiano wa sana kati ya namna tunajisikia na mawazo yetu. Daudi, muandikaji mumoja wa Biblia, alisema hivi katika sala yake kwa Mungu: “Nimetafakari [ao, nimewaza sana] juu ya utendaji wako wote; kwa kupenda niliendelea kuhangaikia kazi ya mikono yako mwenyewe.” (Zaburi 143:5) Daudi hakuwa mutu mwenye kukengeushwa, ao mutu wa kuona mambo kijuu-juu. Roho yake ya kuonyesha shukrani ilitokana na kuchunguza kila siku njia za Mungu; alizoea kufanya hivyo maisha yake yote.—Zaburi 71:5, 17.

Biblia inatupatia shauri hili nzuri: ‘Mambo yoyote yaliyo ya kweli, ya kupendeka, yanayosemwa vema, wema wa adili wowote, na jambo lolote la kustahili sifa, muendelee kuyafikiria mambo hayo.’ (Wafilipi 4:8) Maneno ‘muendelee kuyafikiria’ yanaonyesha tena kwamba tunapaswa kutafakari kila siku, na jambo hilo litatusaidia kuonyesha shukrani.

“Moyo wangu utatafakari mambo ya uelewaji.”Zaburi 49:3.