Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | ELDAR NEBOLSIN

Mupigaji Muzuri wa Piano Anaeleza Imani Yake

Mupigaji Muzuri wa Piano Anaeleza Imani Yake

Eldar Nebolsin wa inchi ya Uzbekistani ni mupigaji wa piano mwenye kujulikana katika mataifa mengi. Alicheza piano ya solo, ni kusema, sehemu fulani ya muziki katika vikundi vya wanamuziki huko Londres, Moscow, Saint Petersburg, New York, Paris, Roma, Sydney, Tokyo, na Vienna. Eldar alikomalia katika Muungano wa Kisovieti na hakuamini kwamba kuna Mungu. Lakini baadaye alikubali kwamba wanadamu waliumbwa na Muumbaji mwenye upendo. Gazeti Amuka! lilimuuliza kuhusu kazi yake ya muziki na imani yake.

Ulifikia kuwa mwanamuziki namna gani?

Wazazi wangu wote wawili wanapiga piano. Walianza kunifundisha kupiga piano nilipokuwa na miaka tano. Mwishowe, nilisomea kwenye masomo yenye kufundisha muziki vizuri sana katika muji wa Tashkenti.

Tuambie kuhusu magumu ya kupiga piano ukiwa katika kikundi cha wanamuziki.

Hakuna vikundi viwili vya wanamuziki vinavyofanana. Vikundi vya wanamuziki ni kama vyombo vikubwa vya muziki ambavyo “vinachezwa” na viongozi wao. Labda tatizo kubwa la mupigaji wa solo ni kufuata vizuri ishara za kiongozi wa kikundi cha wanamuziki. Ni kama mazungumuzo kati ya marafiki, ambayo kila mumoja anapaswa kukubali maoni ya mwenzake, kuliko mutu mumoja tu kuchukua uongozi sikuzote. Mara nyingi, una kipindi kimoja tu ao vipindi viwili vya mazoezi ili kupatana na wengine.

Unafanya mazoezi kwa muda gani?

Ninafanya mazoezi kwa muda wa saa tatu hivi kila siku, na situmie muda huo ili tu kufanya mazoezi ya sehemu za muziki zilizo ngumu. Ninajifunza pia mupangilio wa wimbo ambao ninatayarisha, lakini bila kucheza wimbo huo. Jambo lingine ambalo ninafanya ni kusikiliza muziki uliotungwa na watu wengine, na jambo hilo linanisaidia kuelewa vizuri wimbo ambao ninatayarisha.

Unatambua mupigaji muzuri wa piano namna gani?

Ninamutambua kupitia uwezo wake wa kufanya piano itoe mulio. Acha nijieleze. Piano ni aina ya chombo kinachotoa mulio wakati kinagongwa. Noti fulani ya muziki inapogongwa, mulio unaweza kupunguka, tofauti na vyombo vinavyopulizwa ao sauti ya mwanadamu, ambavyo noti moja ya muziki inaweza kuendelezwa ao hata kuongezwa. Tatizo la wapigaji wa piano ni kushinda mwelekeo wa noti ya muziki kupoteza mulio. Wanafanya hivyo wanapotumia kwa ufundi wa hali ya juu vidole, vifungo vya mikono, na muguu wa kuume ukikanyaga wakati uleule kikanyagio cha upande wa kuume wa piano; kufanya hivyo kunaendeleza mulio wa noti na hata kuubadilisha. Ikiwa wapigaji wa piano wanaelewa ufundi huo mbalimbali ulio mugumu, wanaweza kufanya piano itoe mulio kama wa filimbi, baragumu, ao hata mulio wa kikundi cha wanamuziki. Wanaweza pia kuifanya piano itoe mulio kama wa chombo kizuri zaidi cha muziki kupita vyote, ni kusema, sauti ya mwanadamu.

Ni wazi kwamba unapenda muziki sana.

Mimi ninaona kwamba muziki ni luga ambayo inaeleza moja kwa moja na kuonyesha maoni ya moyoni ambayo ni vigumu kueleza, na hata ambayo haiwezekane kueleza kwa maneno.

Ni nini kilikuchochea upendezwe na mambo ya Mungu?

Sikuzote nyumba yetu ilijaa vitabu ambavyo baba yangu alinunua katika muji wa Moscow. Kitabu ambacho kilinivutia sana kilikuwa na habari za Biblia kuhusu mwanzo wa mwanadamu na mambo ambayo yaliwapata Waisraeli. Kitabu kingine ambacho nilipata ni kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, ambacho kilichapishwa na Mashahidi wa Yehova. * Nilivutiwa na namna kitabu hicho kinavyoonyesha waziwazi mafundisho ya Biblia. Nilipohamia Hispania katika mwaka wa 1991 ili kujifunza muziki, nilibeba kitabu hicho na nikakisoma mara nyingi. Nilivumbua imani ambayo haitegemee tu namna mutu anavyojisikia moyoni lakini pia mambo yenye kupatana na akili na yenye kusadikisha.

Fundisho ambalo lilinivutia kabisa ni ahadi ya Biblia kwamba wanadamu wanaweza kuishi milele duniani. Fundisho hilo lilikuwa lenye kueleweka kabisa! Lakini wakati huo nilikuwa sijakutana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, niliamua kwamba wakati nitakutana nao, nitawaomba wanifundishe Biblia.

Ulikutana namna gani na Mashahidi wa Yehova?

Siku chache kisha kuamua hivyo, niliwaona vijana wanawake wawili, kila mumoja akiwa na Biblia kwenye mukono. Nilifikiri, ‘Wanaonekana kama watu ambao nilisoma juu yao katika kitabu changu. Wanahubiri kama Wakristo wa zamani walivyokuwa wakifanya.’ Bila kukawia, nilianza kujifunza Biblia na Shahidi wa Yehova mumoja. Leo, ninapata furaha kubwa kwa kuwasaidia watu wengine wajifunze juu ya Muumbaji wetu.

Ni nini kilikusadikisha uamini kwamba kuna Muumbaji, wewe ambaye zamani haukuamini kuna Mungu?

Muziki wenyewe ulinisadikisha. Karibu kila mutu anapendezwa na muziki, lakini si hivyo kwa wanyama. Muziki unaweza kueleza furaha, usadikisho, upendo, na hata karibu namna yote ambayo mutu anajisikia moyoni. Kwa kawaida midundo ya muziki inachochea mioyo yetu. Lakini je, muziki ni wa lazima ili tuendelee kuishi? Je, unasaidia viumbe wenye nguvu zaidi kuendelea kuishi kama wanamageuzi wanavyofundisha? Ninawaza hapana. Kwa maoni yangu, si jambo lenye kupatana na akili kusema kwamba ubongo wa mwanadamu ulitokana na mageuzi, pamoja na uwezo wake wa kuunda vitu na kupendezwa na muziki kama ule muziki wa Mozart na wa Beethoven. Maelezo yenye kupatana na akili ni kwamba ubongo wetu uliumbwa na Muumbaji mwenye hekima na upendo.

Biblia ni kama muziki muzuri sana wenye mupangilio wa ajabu, na ina ujumbe wenye kuchochea kwa ajili ya wanadamu wote

Ni nini kilikuchochea uamini kwamba Biblia iliandikwa kwa kuongozwa na roho ya Mungu?

Biblia inaundwa na vitabu vidogo​-vidogo 66 ambavyo viliandikwa na wanaume karibu 40 katika kipindi cha miaka 1 600. Nilijiuliza, ‘Ni nani ambaye angeweza kupanga mambo ili kuandikisha kitabu ambacho kinapatana kwa namna ya ajabu kama Biblia?’ Jibu moja lenye kupatana na akili ni kwamba Biblia iliandikishwa na Mungu. Kwa mawazo yangu, Biblia ni kama muziki muzuri sana wenye mupangilio wa ajabu, na ina ujumbe wenye kuchochea kwa ajili ya wanadamu wote.

^ Mashahidi wa Yehova wanatumia sasa kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? ili kusaidia watu kujifunza Biblia. Unaweza kupata kitabu hicho kwenye adresi yetu ya Internete www.ps8318.com.