Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

Watu Wenye Wamekufa Wataishi Tena!

Watu Wenye Wamekufa Wataishi Tena!

Unaweza kukumbuka Gail, mwenye tulizungumuzia katika habari ya pili. Alikuwa na mashaka kama angeweza kushinda huzuni yenye alikuwa nayo juu ya kifo cha bwana yake, Rob. Lakini, anangojea kwa hamu kumuona tena katika dunia mupya yenye Mungu anaahidi. Anasema hivi: “Andiko lenye ninapenda sana ni Ufunuo 21:3, 4.” Linasema hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

Gail anasema hivi: “Ahadi hiyo inasema mambo yote. Kwa kweli, ninasikilia huruma watu wenye walifiwa na mutu mwenye wanapenda lakini hawajue kama kuko tumaini la kumuona tena.” Gail anatenda kupatana na mambo anaamini kwa kufanya kazi ya kujitolea. Yeye ni muhubiri wa wakati wote; anazungumuzia majirani wake ahadi ya Mungu ya wakati unaokuja ambapo “kifo hakitakuwapo tena.”

Ayubu alikuwa hakika kama angeishi tena

Pengine unaweza kusema, ‘Hiyo ni ndoto tu!’ Lakini fikiria mufano wa mwanaume mwenye kuitwa Ayubu. Alikuwa mugonjwa sana. (Ayubu 2:7) Hata kama Ayubu aliona kuwa ni muzuri kufa, alikuwa angali na imani kama Mungu ana nguvu ya kumufufua ili aishi tena kwenye dunia. Alisema kwa uhakika hivi: “Laiti [ingekuwa muzuri kama] ungenificha katika Kaburi . . . Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:13, 15) Ayubu alikuwa hakika kama Mungu angemukumbuka na kama angetamani kumurudishia uzima.

Hivi karibuni, Mungu atarudishia Ayubu na watu wengine wengi uzima, wakati dunia hii itageuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:42, 43) Katika andiko la Matendo 24:15, Biblia inahakikisha hivi: ‘Kutakuwa ufufuo.’ Yesu anatuhakikishia hivi: ‘Musistaajabie [musishangae] jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.’ (Yohana 5:28, 29) Ayubu ataona wakati ahadi hiyo itatimizwa. Atakuwa na tumaini la kuwa tena na “nguvu za ujana wake” na nyama ya mwili wake itabakia sikuzote “laini [teketeke] kuliko wakati wa ujana.” (Ayubu 33:24, 25) Itakuwa vile pia kwa watu wote wenye wanaonyesha shukrani kwa ajili ya mupango wa Mungu wenye huruma wa kufufua watu ili waishi tena duniani.

Kama umekwisha kuhuzunika sana kwa sababu ya kifo cha mutu mwenye unapenda, pengine mambo yenye tumezungumuzia hayatamaliza kabisa-kabisa huzuni yako. Lakini, ukiwaza sana juu ya ahadi za Mungu zenye kuwa katika Biblia, unaweza kupata tumaini la kweli na nguvu ya kuendelea na maisha.—1 Wathesalonike 4:13.

Unapenda kujua mengi juu ya namna ya kupiganisha huzuni? Ao uko na maulizo juu ya jambo hilo, kama vile “Sababu gani Mungu anaacha mambo mabaya na mateso yaendelee?” Tafazali, fungua adresi yetu ya Internete, jw.org, ili uone majibu ya Biblia yenye kufariji na yenye kusaidia.