Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tuige Imani Yao | Rebeka

‘Niko Tayari Kuenda’

‘Niko Tayari Kuenda’

REBEKA aliangalia eneo lenye milima na mabonde wakati kivuli kilikuwa kinaongezeka. Kisha majuma fulani ya safari, mwishowe alizoea mwendo wa ngamia mwenye aliikalia kwenye mugongo ambaye alikuwa anatikiswa-tikiswa na pepo. Alikuwa ameacha muji wa Harani kwenye alikomalia, mamia ya kilometre kaskazini-mashariki. Pengine hataonaka tena familia yao. Kwa kweli, akili yake ilijaa maulizo mengi juu ya wakati wake unaokuja, zaidi sana sasa, kwa sababu anakaribia kufika kwenye anaenda.

Kikundi chao cha wasafiri kilikuwa kimetambuka sehemu kubwa ya Kanaani na kilikuwa sasa katika eneo la mubaya sana la Negebu. (Mwanzo 24:62) Inawezekana Rebeka aliona kondoo. Pengine eneo hilo halikulimwa sana na halikukuwa na maji, lakini lilikuwa na sehemu nyingi za kukulishia wanyama. Mwanaume mwenye kuzeeka mwenye alikuwa anamuongoza alijua muzuri eneo hilo. Alikuwa na furaha sana kwa sababu alikuwa na habari za muzuri za kumuelezea Isaka. Rebeka angekuwa bibi ya Isaka! Lakini, Rebeka alipaswa kujiuliza ikiwa ataishi maisha ya namna gani katika eneo hilo. Bwana yake Isaka angekuwa wa namna gani? Walikuwa hawajakutana hata siku moja! Angefurahi wakati angemuona Rebeka? Na Rebeka mwenyewe angemupenda?

Katika maeneo mengi ya dunia leo, ndoa zenye kupangwa zinaweza kuonekana kuwa jambo la kushangaza. Lakini, jambo hilo ni kawaida katika maeneo mengine. Hata ukuwe wa desturi gani, unaweza kukubali kama Rebeka alikuwa anaelekea mahali kwenye hajue. Kwa kweli, alikuwa mwanamuke mwenye ujasiri wa pekee na imani ya pekee. Tuko na lazima ya sifa hizo mbili wakati tunapata mabadiliko katika maisha. Kuko sifa zingine za muzuri sana zenye watu wengi hawana zenye Rebeka alionyesha kwa sababu ya imani yake.

“NITATEKA MAJI PIA KWA AJILI YA NGAMIA ZAKO”

Badiliko kubwa lenye lilitokea katika maisha ya Rebeka, lilianza katika njia yenye pengine ilionekana tu kuwa ya kawaida kwake. Alikomalia katika Harani ao karibu na Harani, muji mumoja wa Mesopotamia. Wazazi wake hawakukuwa kama watu wengi wa muji wa Harani. Hawakuabudu mungu-mwezi mwenye kuitwa Sin. Lakini, Mungu wao alikuwa Yehova.—Mwanzo 24:50.

Rebeka alifikia kuwa kijana mwanamuke wa sura ya muzuri sana, lakini hakukuwa muvivu; uzuri wake haukukuwa wa bure. Alikuwa mwenye bidii sana na aliendelea kuwa na mwenendo safi. Familia yao ilikuwa na feza nyingi, kwa hiyo walikuwa na wanafanyakazi, lakini Rebeka hakubembelezwa sana ao kutendewa kama mutoto wa mufalme; alizoezwa kutumika kwa bidii. Kama wanawake wengi wa wakati huo, Rebeka alikuwa anafanya kazi fulani ngumu za nyumbani, kama vile kushota maji kwa ajili ya familia yao. Wakati wa mangaribi, alikuwa anatia mutungi wake kwenye mabega yake na kuenda kwenye kisima.—Mwanzo 24:11, 15, 16.

Siku moja mangaribi, kisha kujaza mutungi wake maji, mwanaume mumoja mwenye kuzeeka alikuja mbio kukutana naye. Mwanaume huyo alimuambia hivi: ‘Tafazali, unipe maji kidogo katika mutungi wako.’ Hilo lilikuwa ombi ndogo na la adabu! Rebeka aliona kama mwanaume huyo alikuwa amefanya safari ndefu. Kwa hiyo, alishusha haraka mutungi kwenye mabega yake na kumuacha mwanaume huyo akunywe. Hakukunywa tu maji kidogo, lakini alikunywa kabisa maji hayo ya baridi yenye hayakukuwa na chumvi. Kisha akatambua kama mwanaume huyo alikuwa na ngamia kumi wenye walikuwa wanapiga magoti karibu nao, na chombo cha kutilia wanyama maji hakikukuwa na maji. Rebeka aliona kama mwanaume huyo alikuwa anamuangalia kwa uangalifu, na alitaka kufanya yake yote ili amuonyeshe utoaji. Kwa hiyo, alisema hivi: ‘Nitateka [nitashota] maji pia kwa ajili ya ngamia zako mupaka wamalize kunywa.’—Mwanzo 24:17-19.

Ona kama Rebeka hakujitolea tu kushota maji kwa ajili ya ngamia kumi lakini alijitolea pia kuwashotea maji mupaka kiu yao iishe. Kama iko na kiu sana, ngamia mumoja anaweza kunywa litre 95 za maji! Kama ngamia wote hao kumi walikuwa na kiu, Rebeka angefanya kazi ngumu kwa saa nyingi. Lakini kama vile mambo yalitokea, inawezekana ngamia hao hawakukuwa na kiu sana. * Lakini, Rebeka alijua hilo wakati alijitolea kushota maji kwa ajili ya ngamia? Hapana. Alikuwa na nia, pia alikuwa tayari kufanya kazi kwa bidii kama vile iliomba ili kumuonyesha ukaribishaji mwanaume huyo mugeni mwenye kuzeeka. Mwanaume huyo aliitika jambo Rebeka alijitolea kufanya. Alimuangalia Rebeka kwa uangalifu wakati alikuwa anaenda na kurudia, kujaza tena na tena mutungi wake wa maji na kumwanga tena na tena maji hayo katika chombo cha kutilia wanyama maji.—Mwanzo 24:20, 21.

Rebeka alikuwa mwenye bidii na mukaribishaji-wageni

Mufano wa Rebeka unatufundisha mambo mengi leo. Tunaishi wakati wenye watu wanajifikiria sana. Kama vile ilitabiriwa, watu wamekuwa “wenye kujipenda wenyewe,” hawataki kufanya mambo kwa ajili ya wengine. (2 Timotheo 3:1-5) Ni muzuri kwa Wakristo wenye wanatafuta kupiganisha roho hiyo ya kujipenda, kuona katika akili picha ya kijana huyo mwanamuke wa zamani, mwenye alikuwa anaenda kushota maji tena na tena kwenye kisima.

Kwa kweli, Rebeka alitambua kama mwanaume huyo alikuwa anamuangalia sana. Hakukuwa na nia ya mubaya; alimuangalia kwa njia yenye kuonyesha kama alikuwa mwenye kushangaa, na mwenye furaha. Wakati Rebeka alimaliza, mwanaume huyo alimupatia zawadi, ni kusema, vitu vya mapambo vya bei sana! Kisha akamuuliza: ‘Wewe ni binti ya nani? Tafazali niambie. Je, muna nafasi yoyote nyumbani kwa baba yako tukae usiku huu?’ Wakati alimuambia juu ya familia yao, furaha ya mwanaume huyo iliongezeka. Pengine kwa sababu ya kuchangamuka, Rebeka aliongeza hivi: “Tuna majani na chakula kingi cha mifugo, pia mahali pa kukaa usiku.” Hizo zilikuwa zawadi nyingi, kwa sababu mwanaume huyo alikuwa na watu wengine. Kisha akakimbia na kutangulia mwanaume huyo ili kuambia mama yake jambo lenye lilitokea.—Mwanzo 24:22-28, 32.

Ni wazi kama Rebeka alifundishwa kuwa na sifa ya kukaribisha wageni wakati alikuwa anakomaa. Hiyo ni sifa ingine yenye inaonekana kuwa inaanza kupotea leo, na hiyo ni sababu ingine ya kuiga imani ya kijana huyo mwanamuke mwenye moyo muzuri. Imani kwa Mungu inapaswa kutuchochea tukuwe na sifa ya kukaribisha wageni. Yehova ni mukaribishaji-wageni, kwa sababu anatolea watu wote, na anataka watumishi wake wafanye vilevile. Wakati tunakaribisha hata watu wenye hawatatutolea kitu chochote, tunamufurahisha Baba yetu wa mbinguni.—Mathayo 5:44-46; 1 Petro 4:9.

‘UTAMUCHUKULIA MWANANGU MUKE [BIBI]’

Mwanaume huyo muzee mwenye alikuja kwenye kisima alikuwa nani? Alikuwa mutumishi wa Abrahamu, ndugu ya tate (nkambo) mwanaume wa Rebeka. Kwa hiyo, alikaribishwa katika nyumba ya Bethueli, baba ya Rebeka. Inawezekana jina la mutumishi huyo lilikuwa Eliezeri. * Familia ya Bethueli ilimutolea chakula, lakini alikataa kula mupaka aonyeshe sababu gani alikuja. (Mwanzo 24:31-33) Tunaweza kuwazia namna alizungumuza kwa uchangamufu, kwa sababu alitokea tu kuona jambo lenye lilimuhakikishia sana kama Yehova, Mungu wake, alikuwa anabariki safari yake ya maana. Namna gani?

Wazia Eliezeri anaeleza habari yake wakati Bethueli, baba ya Rebeka, na Labani ndugu ya Rebeka wanamusikiliza kwa uangalifu. Aliwaambia kama Yehova amebariki Abrahamu sana katika inchi ya Kanaani na kama Abrahamu na Sara walikuwa na mutoto, Isaka, mwenye anapaswa kuriti mali yao yote. Abrahamu alikuwa amepatia mutumishi huyo kazi ya maana sana: alipaswa kutafutia Isaka mwanamuke katika jamaa ya Abrahamu huko Harani.—Mwanzo 24:34-38.

Abrahamu alimuomba Eliezeri aape kama hatachagulia Isaka bibi kati ya wanawake wa Kanaani. Sababu gani? Kwa sababu Wakanaani hawakumuheshimia Yehova Mungu na hawakumuabudu. Abrahamu alijua kama Yehova alikusudia kupatia watu hao malipizi kwa wakati wenye kufaa kwa sababu ya matendo yao ya mubaya. Abrahamu hakutaka Isaka, mwana wake mupendwa, ajiunge na watu hao na njia zao za mubaya. Tena, alijua kama mwana wake alikuwa na daraka la maana katika kutimizwa kwa ahadi za Yehova.—Mwanzo 15:16; 17:19; 24:2-4.

Eliezeri aliendelea kuambia familia ya Bethueli kama wakati alifika kwenye kisima karibu na Harani, alisali kwa Yehova Mungu. Kwa kweli, alimuomba Yehova achague mwanamuke mwenye Isaka ataoa. Namna gani? Eliezeri aliomba Mungu aongoze mwanamuke mwenye anataka Isaka aoe akuje kwenye kisima. Wakati angemuomba maji ya kunywa, mwanamuke huyo angepaswa kujitolea kumupatia Eliezeri maji ya kunywa na apatie pia ngamia wake. (Mwanzo 24:12-14) Na ni nani alikuja na kufanya mambo hayo? Ni Rebeka! Wazia namna Rebeka angeweza kujisikia kama alikuwa anasikiliza habari yenye Eliezeri alikuwa anaambia watu wa familia yake!

Bethueli na Labani waliguswa moyo na habari ya Eliezeri. Walisema hivi: “Jambo hili limetoka kwa Yehova.” Kama vile desturi yao iliomba, walifanya mapatano ya ndoa, wakaoesha Rebeka kwa Isaka. (Mwanzo 24:50-54) Hilo linamaanisha kama Rebeka hakukuwa na jambo lolote la kusema?

Majuma fulani mbele ya hapo, Eliezeri alimuuliza Abrahamu jambo hilo, kwa kusema hivi: ‘Itakuwaje ikiwa mwanamuke huyo hatakuja pamoja nami?’ Abrahamu alikuwa amemujibia hivi: “Utakuwa bila wajibu kwangu kwa kiapo.” (Mwanzo 24:39, 41) Katika nyumba ya Bethueli pia, mawazo ya kijana huyo mwanamuke juu ya jambo hilo yalikuwa ya maana. Eliezeri alichangamuka sana kwa sababu safari yake ilipata matokeo ya muzuri. Kwa hiyo, asubui yenye ilifuata aliomba ikiwa angeweza kurudia Kanaani mara moja pamoja na Rebeka. Lakini, watu wa familia walipenda Rebeka abakie pamoja nao kwa siku zingine kumi hivi. Mwishowe, walikata maneno hivi: ‘Na tumuite huyo mwanamuke kijana tusikie kutoka kinywani mwake.’—Mwanzo 24:57.

Sasa, Rebeka alipaswa kukamata uamuzi mukubwa katika maisha yake. Angesema nini? Angeshawishi baba yake na ndugu yake wamusikilie huruma na kuwaomba sana ili asifanye safari hiyo ya kuenda mahali kwenye hajue? Ao angeona hilo kuwa pendeleo la kuchangia katika matukio yenye yalionekana waziwazi kuwa yaliongozwa na Yehova? Wakati alijibia, alionyesha namna aliona badiliko hilo la kushitukia, na pengine la kuogopesha lenye lilitokea katika maisha yake. Alisema tu hivi: ‘Niko tayari kuenda.’—Mwanzo 24:58.

Hiyo ilikuwa roho ya ujasiri kabisa! Leo, desturi zetu juu ya ndoa zinaweza kuwa tofauti kidogo na za wakati huo, lakini tunaweza kujifunza mambo mengi juu ya Rebeka. Hakuona mambo yenye anapenda kuwa ya maana, lakini mambo yenye kupendeza Yehova Mungu. Juu ya ndoa leo, Neno la Mungu lingali linatoa muongozo muzuri juu ya bibi ao bwana mwenye mutu anapaswa kuchagua na namna ya kuwa bibi ao bwana muzuri. (2 Wakorintho 6:14, 15; Waefeso 5:28-33) Ni muzuri kufuata mufano wa Rebeka na kufanya mambo vile Yehova anapenda.

‘ULE MWANAUME NI NANI?’

Watu wa familia ya Bethueli walibariki Rebeka, mupendwa wao. Kisha, yeye na Debora, mufanyakazi mwenye alikuwa anamutunza tangu utoto, na watumishi fulani wanawake, wakaondoka pamoja na Eliezeri na wanaume wake. (Mwanzo 24:59-61; 35:8) Bila kukawia, waliacha muji wa Harani, mbali sana nyuma yao. Safari ilikuwa ndefu, kilometre 800 hivi, na pengine ilifanya majuma tatu. Inawezekana haikukuwa safari ya muzuri. Rebeka alikuwa ameona ngamia wengi katika maisha yake, lakini hatuwezi kuwazia kama alikuwa mupandaji muzuri wa ngamia. Biblia inasema kama familia yao ilikuwa ya wachungaji, haiko ya wafanyabiashara wenye walifanya safari kwenye vikundi vya ngamia. (Mwanzo 29:10) Watu wenye hawazoee kupanda kwenye ngamia wanasemaka kama wanachoka, hata kisha kupanda kwenye ngamia kwa muda mufupi!

Rebeka aliangalia tu mbele, na kwa kweli, alijaribu kujifunza mambo mengi kutoka kwa Eliezeri juu ya Isaka na familia yake. Umuone katika akili mwanaume huyo mwenye kuzeeka wakati anazungumuza na Rebeka mangaribi pembeni ya moto, akimuambia juu ya ahadi ya Yehova na juu ya rafiki yake Abrahamu. Mungu angetokeza katika kizazi cha Abrahamu uzao wenye ungeletea wanadamu wote baraka. Wazia woga wenye Rebeka alisikia katika moyo wake wakati alitambua kama ahadi za Yehova zingetimizwa kupitia Isaka, mwenye angekuwa bwana yake, na hivyo kupitia yeye pia!—Mwanzo 22:15-18.

Rebeka alionyesha unyenyekevu wa maana sana wenye watu wengi hawana leo

Mwishowe siku yenye tulizungumuzia kwenye mwanzo wa habari hii ikafika. Wakati kikundi cha wasafiri kilipita katika eneo la Negebu na giza lilianza kuingia, Rebeka aliona mwanaume mumoja mwenye alikuwa anatembea katika mashamba. Mwanaume huyo alionekana kuwa mwenye kufikiri sana. Tunasoma hivi: “Akaruka chini kutoka kwenye ngamia.” Pengine hakungojea hata ngamia ipige magoti, na kisha akauliza kiongozi wake hivi: ‘Ule mwanaume anayetembea pale shambani kuja kutupokea, ni nani?’ Wakati aliambiwa kama mwanaume huyo alikuwa Isaka, alifunika kichwa chake na kitambaa. (Mwanzo 24:62-65) Sababu gani? Pengine kufanya vile ilikuwa alama ya kumuonyesha heshima mwenye atakuwa bwana yake. Watu wengi leo wanaweza kuona aina hiyo ya ujitiisho kuwa jambo la zamani. Lakini, kwa kweli, wanawake na pia wanaume wanaweza kujifunza jambo la maana kupitia unyenyekevu wa Rebeka, kwa sababu sisi wote tuko na lazima sana ya sifa hiyo ya muzuri.

Isaka, mwanaume wa miaka karibu 40, alikuwa angali na huzuni ya kifo cha mama yake, Sara, mwenye alikufa kulikuwa kumepita miaka tatu hivi. Kwa hiyo, tunaweza kusema kama Isaka alikuwa mwanaume mwenye upendo na huruma. Ilikuwa baraka sana kwa mwanaume huyo kupata bibi mwenye bidii, mukaribishaji-wageni, na munyenyekevu! Mambo yalikuwa namna gani? Biblia inasema tu hivi: ‘Naye akamupenda [Rebeka].’—Mwanzo 24:67; 26:8.

Leo, ni vyepesi kwetu kupenda Rebeka hata kama kumekwisha kupita miaka 3900 hivi. Kwa kweli, tunapendezwa na sifa yake ya ujasiri, bidii yake, ukaribishaji wake na unyenyekevu wake. Ni muzuri sisi wote, vijana na wazee, wanaume na wanawake, wenye kuoa ao kuolewa, wenye hawajaoa ao kuolewa, kuiga imani yake!

^ fu. 10 Tayari ilikuwa mangaribi. Katika habari hiyo, hakuna jambo lolote lenye kuonyesha kama Rebeka alibakia kwenye kisima kwa saa nyingi. Tena, haionyeshe kama watu wa familia yake walikuwa wamelala wakati alimaliza kushota maji ao kama mutu fulani alikuja kuangalia sababu gani alikawia.

^ fu. 15 Jina Eliezeri halitajwe katika habari hiyo, lakini inawezekana mutumishi mwenye kuzungumuziwa katika habari hiyo ni yeye. Wakati fulani Abrahamu alisema Eliezeri ariti mali yake yote ikiwa anakufa bila kuwa na muriti, kwa hiyo Eliezeri ndiye alikuwa mukubwa zaidi na mwenye kutumainika kati ya watumishi wa Abrahamu. Ni vile pia mutumishi mwenye kutajwa katika habari hiyo anaelezwa.—Mwanzo 15:2; 24:2-4.