Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Maoni Yako Kuwahusu Wengine Yanapaswa Kutegemea Jinsi Unavyowaona kwa Mara ya Kwanza?

Je, Maoni Yako Kuwahusu Wengine Yanapaswa Kutegemea Jinsi Unavyowaona kwa Mara ya Kwanza?

Je, Maoni Yako Kuwahusu Wengine Yanapaswa Kutegemea Jinsi Unavyowaona kwa Mara ya Kwanza?

DAKTARI fulani alikuwa ameketi sebuleni akitazama kipindi cha mazungumzo kwenye televisheni ambapo waziri mmoja wa serikali ya Ireland alikuwa akihojiwa. Baada ya kuutazama uso wa waziri huyo kwa makini, yule daktari aliona kitu alichofikiri kuwa dalili ya uvimbe fulani. Alimshauri yule waziri afanyiwe uchunguzi wa kimatibabu mara moja.

Uchunguzi ulionyesha kwamba alikuwa na uvimbe. Daktari huyo alikuwa na uwezo wa kipekee wa kitiba, uwezo wa kutambua ugonjwa kwa kumtazama tu mgonjwa. Hata hivyo, wengine wanafikiri wana uwezo kama huo wa kumtazama mtu na kujua utu wake, tabia zake, na kama ni mnyoofu.

Kwa karne nyingi, watafiti wamejaribu kutokeza mbinu za kisayansi za kutambua tabia za mtu kwa kuchunguza sura yake. Mbinu hizo zinaitwa physiognomy, yaani, kutambua tabia za mtu kwa kutazama uso wake. Encyclopædia Britannica inafafanua mbinu hizo kuwa “sayansi bandia ya kujaribu kujua tabia za utu ambazo inasemekana zinaweza kutambulika kwa kutazama uso au umbo la mwili.” Katika karne ya 19 wataalamu wa kuchunguza asili ya binadamu, kama vile Francis Galton, ambaye ni binamu ya Charles Darwin, na wataalamu wa uhalifu, kama vile Cesare Lombroso wa Italia, walipendekeza nadharia na mbinu kama hizo ambazo zimesahauliwa na wengi.

Hata hivyo, bado wengi wanaamini kwamba inawezekana kujua tabia za mtu kwa kutazama tu sura yake. Je, tunaweza kutegemea uwezo huo?

Kuhukumu kwa Kutazama Sura

Mfano unaojulikana wa kuhukumu, au kuhukumu isivyofaa, kwa kutazama sura unapatikana katika kitabu cha Biblia cha Samweli wa Kwanza. Yehova Mungu alimwagiza nabii Samweli amtie mafuta mshiriki wa familia ya Yese ili awe mfalme wa Israeli wakati ujao. Tunasoma hivi: “Ikawa kwamba [wana wa Yese] walipokuwa wakiingia naye akamwona Eliabu, mara moja akasema: ‘Hakika mtiwa-mafuta wake yuko mbele za Yehova.’ Lakini Yehova akamwambia Samweli: ‘Usiangalie sura yake wala urefu wa umbo lake, kwa maana nimemkataa. Kwa kuwa Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.’” Vivyo hivyo, Yehova aliwakataa wana wengine sita wa Yese. Mwishowe, kinyume na yale ambayo yule nabii na Yese walifikiri, Mungu alimchagua Daudi awe mfalme wa wakati ujao. Alikuwa mwana wa nane, kijana mdogo ambaye hakuna mtu aliyefikiria kumleta mbele ya Samweli.—1 Samweli 16:6-12.

Mambo si tofauti sana leo. Miaka michache iliyopita nchini Ujerumani, profesa mmoja wa uhalifu alifanya uchunguzi uliohusisha wanafunzi 500 wa sheria. Kulikuwa na “wageni” 12 wasiojulikana. Wageni hao walitia ndani kamanda wa polisi na kiongozi wa mashtaka, mweka-hazina wa chuo hicho na ofisa wa uhusiano na umma, mawakili fulani na maofisa wa mahakama, na wahalifu watatu waliohukumiwa. Wanafunzi waliombwa waamue kazi ambayo walifikiri kila mmoja wa wageni hao alikuwa akifanya na nani aliyepaswa kufungwa gerezani na wataje uhalifu aliokuwa amefanya. Uamuzi wao ulipaswa kutegemea sura na mambo ambayo wageni hao walisema wanapenda kufanya ili kujifurahisha.

Matokeo yalikuwa nini? Karibu asilimia 75 ya wanafunzi walifaulu kuwatambua wale wahalifu watatu. Lakini asilimia 60 ya wanafunzi walisema kwamba wale wageni wengine tisa walikuwa wahalifu, ingawa hawakuwa na hatia. Asilimia 14 ya wanafunzi walisema kiongozi wa mashtaka wa eneo hilo alikuwa mlanguzi wa dawa za kulevya, na asilimia 33 wakasema kamanda wa polisi alikuwa mwizi! Hivyo, maamuzi yanayofanywa kwa kutazama sura yanaweza kupotosha kwelikweli. Jinsi gani?

Sura Inaweza Kudanganya

Tunapokutana na mtu kwa mara ya kwanza, huenda tukawa na maoni fulani kumwelekea yanayotegemea mambo tuliyojionea zamani. Tuna mwelekeo wa kuamua mambo kijumla na kumhukumu kwa kutegemea maoni ya watu wengi. Mbali na sura, huenda tukamhukumu mtu huyo kwa msingi wa kitaifa, kikabila, kidini, au cheo chake katika jamii.

Ikiwa maoni tuliyo nayo kumwelekea mtu huyo yanathibitika kuwa ya kweli, tunajipongeza kwa sababu tuliamua vizuri, na hivyo kuwa na hakika hata zaidi kwamba tuna uwezo wa kuamua kwa kutazama sura. Hata hivyo, tunapotambua kwamba maoni yetu yalikuwa yenye makosa kabisa, tunatendaje? Ikiwa sisi ni wanyoofu, tunapaswa kubadili maoni hayo na kujaribu kutafuta ukweli. La sivyo, kwa sababu tu ya kiburi na kufikiri kwamba tuna uwezo wa kipekee wa kuhukumu, huenda tukawasababishia wengine madhara au hata kuwatendea isivyofaa kabisa.

Kumhukumu mtu kwa kutazama sura kunaweza kumdhuru yule anayehukumiwa na pia yule anayehukumu. Kwa mfano, katika karne ya kwanza, Wayahudi wengi hawakuamini kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa. Kwa nini? Kwa sababu maoni yao yalitegemea sura ya nje, walimwona Yesu kuwa mwana wa seremala wa mashambani. Ingawa walivutiwa na miujiza na maneno yake yenye hekima, hawakuamini kwamba alikuwa Masihi kwa kuwa walitegemea maoni yao. Mtazamo wao ulimfanya Yesu aende kuwahubiria watu wa maeneo mengine, na kusema: “Nabii hakosi kuheshimiwa ila katika eneo lake la nyumbani na katika nyumba yake mwenyewe.”—Mathayo 13:54-58.

Wayahudi hao walikuwa raia wa taifa ambalo lilikuwa limemngojea Masihi kwa karne nyingi. Kwa kuruhusu waongozwe na maoni yao yaliyotegemea kutazama sura, hawakumtambua Masihi alipokuja na hivyo wakapoteza kibali cha Mungu. (Mathayo 23:37-39) Wafuasi wa Yesu walibaguliwa kwa njia hiyohiyo. Watu wengi hawakuamini kwamba kikundi kidogo cha wavuvi maskini, waliodharauliwa na watu wenye elimu na viongozi wa dini kuu ya wakati huo, kingewafundisha jambo lolote la maana. Wale walioshikilia maoni yao walipoteza nafasi nzuri ya kuwa wafuasi wa Mwana wa Mungu.—Yohana 1:10-12.

Wengine Walibadili Maoni Yao

Kuna watu fulani walioishi siku za Yesu ambao walinyenyekea na kubadili maoni yao walipoona mambo ambayo Yesu alifanya. (Yohana 7:45-52) Baadhi yao ni watu fulani katika familia ya Yesu, ambao mwanzoni hawakufikiri ingewezekana kwamba mmoja wao angekuwa Masihi. (Yohana 7:5) Inapendeza kwamba baada ya muda walibadili maoni yao na wakamwamini. (Matendo 1:14; 1 Wakorintho 9:5; Wagalatia 1:19) Vivyo hivyo, miaka mingi baadaye huko Roma, wawakilishi fulani wa jamii ya Wayahudi walikuwa tayari kumsikiliza mtume Paulo badala ya kuamini uvumi ulioenezwa na maadui wa Ukristo. Baada ya kumsikiliza, baadhi yao wakawa Wakristo.—Matendo 28:22-24.

Leo, watu wengi wana maoni yasiyofaa kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa nini? Mara nyingi, si kwa sababu wamechunguza ukweli au wamethibitisha kwamba imani na matendo ya Mashahidi hayapatani na Maandiko. Badala yake, ni kwa sababu hawaamini kwamba Mashahidi wa Yehova wana ukweli wowote kuhusu mambo ya kidini. Kumbuka kwamba katika karne ya kwanza wengi walikuwa na maoni kama hayo kuhusu Wakristo wa wakati huo.

Haishangazi kuona watu wakisema mambo mabaya kuhusu wale wanaojitahidi kufuata mfano wa Yesu. Kwa nini? Kwa sababu Yesu aliwaonya wafuasi wake hivi: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” Lakini akawatia moyo kwa kuwaambia: “Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 10:22.

Kwa kutii amri ya Yesu, leo Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kuwahubiria watu ulimwenguni pote habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 28:19, 20) Wale wanaokataa kabisa kusikiliza wanakabili hatari ya kukosa nafasi ya kupata barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele. (Yohana 17:3) Namna gani wewe? Je, utafuata maoni yanayotegemea kutazama sura ya nje na maoni ambayo umekuwa nayo, au utakuwa tayari kuchunguza ukweli ukiwa na mtazamo unaofaa? Kumbuka: Sura inaweza kudanganya, na maoni yanaweza kuwa na makosa; lakini kuchunguza jambo ukiwa na mtazamo unaofaa kunaweza kuleta furaha nyingi.—Matendo 17:10-12.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Maoni ambayo Wayahudi wengi walikuwa nayo walipomwona Yesu kwa mara ya kwanza yalifanya wamkatae kuwa Masihi

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, maoni yako kuhusu Mashahidi wa Yehova yanategemea mambo ya kuwaziwa au mambo hakika?