Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani—Muchungaji

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani—Muchungaji

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani—Muchungaji

‘Atalichunga kundi lake mwenyewe kama muchungaji. Atawakusanya pamoja wana-kondoo kwa mukono wake; naye atawabeba katika kifua chake.’—ISAYA 40:11.

WACHUNGAJI wanatajwa mara nyingi sana katika Biblia, kuanzia kitabu cha kwanza mupaka kitabu cha mwisho. (Mwanzo 4:2; Ufunuo 12:5) Watu fulani wenye kujulikana sana, kama vile Abrahamu, Musa na Mufalme Daudi, walikuwa wachungaji. Mutunga zaburi Daudi alieleza vizuri kazi ya muchungaji muzuri na mambo ambayo alihangaikia. Na zaburi fulani inayosemwa kuwa iliandikwa na Asafu inaonyesha kama Daudi alikuwa muchungaji wa watu wa Mungu wa wakati wa zamani.​—Zaburi 78:70-72.

Wakati wa Yesu, kuchunga wanyama ilikuwa ingali kazi ya lazima. Yesu alijiita ‘muchungaji mwema’ na mara nyingi alitumia sifa za muchungaji muzuri ili kufundisha watu mambo ya lazima. (Yohana 10:2-4, 11) Hata Yehova, Mungu Mweza​-yote anafananishwa na ‘muchungaji.’​—Isaya 40:10, 11; Zaburi 23:1-4.

Wachungaji walichunga wanyama gani? Kazi yao iliomba pia kufanya nini? Na mufano wa wafanyakazi hao wenye bidii unaweza kutufundisha nini?

Kondoo na Mbuzi

Labda wachungaji katika Israeli la zamani walichunga aina nyingi za kondoo za huko Siria, kama vile kondoo zinazoitwa karakul, zilizo na manyoya mengi na mikia minene na yenye kunona. Kondoo dume za aina hiyo zina pembe lakini kondoo jike hazina pembe. Wanyama hao watulivu wanapotezwa kwa vyepesi na hawajitetee wanaposhambuliwa.

Wachungaji walichunga pia mbuzi. Mbuzi zilikuwa na rangi nyeusi ao ya kahawa ngozi nzima. Masikio yao marefu na yenye kupiga​-piga yaliumia​-umia kwa vyepesi katika miiba zilipopanda vilima vyenye majiwe na zilipokula majani katika misitu.

Sikuzote, wachungaji walikuwa na tatizo la kufundisha kondoo na mbuzi kutii maagizo yao. Hata hivyo, wachungaji wazuri walikuwa wavumilivu na walihangaikia wanyama waliokuwa wanachunga, na hata waliwapatia majina; na wanyama hao wangeweza kutambua majina yao.​—Yohana 10:14, 16.

Majira Ambamo Wachungaji Walitumika

Katika majira ya kuchipua, inawezekana kila siku muchungaji alipeleka kundi lake la wanyama kwenye malisho yaliyokuwa na majani mabichi katika kijiji cha karibu. Katika majira hayo, wanyama wao walizaa na kundi liliongezeka. Wakati huo pia, wachungaji walikata manyoya ya wanyama wao, na siku ya kukata manyoya ya wanyama ilikuwa sikukuu kwa muchungaji!

Inawezekana kila mukaaji wa kijiji alikuwa na kondoo chache tu. Kwa hiyo, alimulipa muchungaji fulani aliyekuwa na kondoo za watu wengine ili aongeze kondoo hizo kwenye kundi lake. Wachungaji waliolipwa hawakuhangaikia sana wanyama waliopewa kama vile walivyohangaikia wanyama wao wenyewe.​—Yohana 10:12, 13.

Muchungaji alipoona kama mashamba yaliyokuwa karibu na kijiji chake yamekwisha kuvunwa, alipeleka kondoo zake katika mashamba hayo ili zikule majani yaliyokuwa yanaota na mbegu zilizobaki katika maganda. Majira ya joto yalipoanza, muchungaji alihamishia kondoo zake katika malisho mazuri kwenye vilima. Kwa muda wa siku nyingi, wachungaji waliishi inje, wakati makundi yao yalikuwa yanakula majani kwenye miteremuko ya vilima, kila siku walipitisha usiku inje wakichunga makundi yao. Wakati fulani, inawezekana muchungaji aliingiza kundi lake la wanyama katika shimo kubwa lililokuwa chini ya udongo ao chini ya jiwe kubwa ili kuwalinda na mbwa wa mwituni ao wanyama wengine wakali. Ikiwa mulio wa munyama fulani uliogopesha kundi la kondoo katika giza la usiku, sauti pole ya muchungaji ilizituliza.

Kila mangaribi, muchungaji alihesabia kondoo zake na kuchunguza ikiwa zilikuwa na afya nzuri. Kila asubuhi, aliita kondoo zake, nazo zilimufuata kwenye malisho. (Yohana 10:3, 4) Katikati ya muchana, muchungaji alipeleka kondoo zake kwenye visima vya maji baridi ili zikunywe. Wakati visima hivyo vilikauka, muchungaji alipeleka kondoo zake kwenye chemichemi na alizishotea maji.

Kipwa kilipokaribia kumalizika, muchungaji alihamishia kundi lake la wanyama kwenye malisho yaliyokuwa katika mabonde karibu na bahari. Mvua ilipoanza kunyesha, alizirudisha ili kupitisha majira ya baridi nyumbani. Wakati huo, wanyama hawangebakia inje kwa sababu wangekufa na mvua, upepo mukali, na seluji (matone madogo-madogo ya mvua yaliyoganda kwa baridi). Kuanzia Mwezi wa 11 mupaka majira ya kuchipua, wachungaji hawakulisha makundi yao ya wanyama inje.

Vyombo vya Muchungaji

Mavazi ya muchungaji yalikuwa ya kawaida lakini ya nguvu. Ili kujilinda na mvua na baridi ya usiku, labda alivaa vazi lililofanywa na ngozi ya kondoo, sehemu ya manyoya ya vazi hilo iligeuziwa ndani. Alitia kanzu ndefu lisilo na mikono ndani ya vazi hilo. Pia, alivaa viatu ili majiwe na miiba visimuumize, na alifunika kichwa chake na kitambaa kilichofanywa na manyoya ya kondoo.

Kwa kawaida muchungaji alikuwa na vyombo vinavyofuata: (1) Mufuko wa ngozi uliokuwa na chakula kama vile mukate, mizeituni, matunda yenye kukaushwa, na fromaje; (2) kipande cha muti alichotumia kama silaha, kilichokuwa na fundo kubwa upande mumoja, kwa kawaida kilikuwa na urefu wa metre moja; (3) kisu; (4) fimbo, aliyotumia ili kutembea na kupanda milima; (5) chombo chake cha kubebea maji; (6) mbeketi ya ngozi ambayo ingeweza kukunjwa aliyotumia ili kushota maji katika visima virefu; (7) kombeo, ambalo alitumia ili kutupia majiwe kondoo ao mbuzi zilizotaka kupotea, alifanya hivyo ili kuzirudisha katika kundi, alitumia pia kombeo hilo ili kufukuza wanyama wakali; (8) chombo cha kupigia miziki alichotumia ili kujifurahisha na kutuliza wanyama wake.

Kazi ya muchungaji haikuwa ya bure, wanyama walimutolea vitu vya lazima katika maisha, kama vile maziwa na nyama. Manyoya na ngozi ya kondoo vilitumiwa kama feza, na vilifanya mavazi na vyombo vya kuwekea maji ao vitu vingine. Manyoya ya mbuzi pia yalifanya mavazi, na kondoo na mbuzi zilitolewa sadaka.

Mufano Muzuri wa Kufuata

Wachungaji wazuri walikuwa watu wenye bidii, wenye kutumainika, na wasio na woga. Na hata walihatarisha maisha yao ili kulinda kundi.​—1 Samweli 17:34-36.

Haishangaze kuona kama Yesu na wafuasi wake walionyesha kama wazee wa kutaniko wanapaswa kufuata mufano wa wachungaji. (Yohana 21:15-17; Matendo 20:28) Kama muchungaji muzuri wa wakati wa zamani, leo wazee wa kutaniko wanajikaza ‘kuchunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao, si kwa kulazimishwa, bali kwa kupenda; wala si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.’​—1 Petro 5:2.

[Picha katika ukurasa wa 28]

(Ona Kichapo)