Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA | NAMNA YA KUPIGANISHA MAHANGAIKO

Mahangaiko Juu ya Hatari

Mahangaiko Juu ya Hatari

Alona anasema hivi: “Wakati ninasikia kelele ya kuonya watu juu ya hatari, moyo wangu unapiga-piga haraka na ninakimbilia mahali pa kujilinda na bombe. Hata wakati niko mahali hapo ninaendelea kuhangaika. Ninahangaika hata zaidi wakati niko inje na sina mahali pa kujificha. Siku moja, wakati nilikuwa ninatembea katika barabara, nilisikia kelele hiyo, nikaanza kulia na sikuweza kupumua. Iliomba saa nyingi ili niweze kutulia. Kisha nikasikia tena kelele hiyo.”

Alona

Vita ni jambo moja tu kati ya mambo mengi yenye kuleta hatari. Kwa mufano, kutambua kuwa wewe mwenyewe ao mutu mwenye unapenda iko na ugonjwa hatari kunaweza kukuumiza sana. Pia watu wengine wanaweza kuwa na mahangaiko kwa sababu ya kuogopa wakati unaokuja. Wanajiuliza hivi: ‘Watoto wetu, ao watoto wa watoto wetu, wataishi katika dunia yenye vita, jeuri, mazingira yenye kuchafuliwa, hali ya hewa yenye kubadilika, na magonjwa yenye kuenea haraka?’ Namna gani tunaweza kupiganisha mahangaiko kama hayo?

‘Mutu mwerevu ambaye ameona musiba amejificha,’ kwa sababu anajua kuwa mambo mabaya yanatokea mara nyingi. (Methali 27:12) Kama vile tunajikaza kulinda afya yetu ya kimwili, tunapaswa pia kulinda afya yetu ya akili na ya moyoni. Mambo ya kujifurahisha yenye kuwa na jeuri ao hata habari zenye kuonyesha picha za kuogopesha zinaweza kuongeza mahangaiko yetu na ya watoto wetu. Kuepuka kuangalia picha zenye kuonyesha mambo ya jeuri hakumaanishe kuwa hatupendi kuona ukweli wa mambo. Mungu hakuumba akili yetu ili ikazie mambo mabaya. Lakini, tunapaswa kujaza katika akili yetu “mambo yoyote yaliyo ya kweli, . . . ya uadilifu, . . . yaliyo safi kiadili, . . . ya kupendeka.” Tukifanya hivyo, “Mungu wa amani” atatupatia amani ya akili na ya moyoni.—Wafilipi 4:8, 9.

FAIDA YA SALA

Imani ya kweli inatusaidia kupiganisha mahangaiko. Biblia inatutia moyo ‘tukeshe kuhusiana na sala.’ (1 Petro 4:7) Tunaweza kumuomba Mungu atusaidie na atupatie hekima na bidii ya kutusaidia tupambane na hali yetu ngumu. Tunapaswa kuwa hakika kuwa “anatusikia kwa habari ya jambo lolote tunaloomba.”— 1 Yohana 5:15.

Pamoja na Avi, bwana yake

Biblia inasema kuwa haiko Mungu lakini ni Shetani ndiye ‘mutawala wa ulimwengu huu’ na kuwa ‘ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’ (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, Yesu alisema mambo ya kweli kabisa wakati alitufundisha kusali hivi: ‘Utukomboe kutokana na yule muovu.’ (Mathayo 6:13) Alona anasema hivi: “Wakati ninasikia kelele ya kuonya watu juu ya hatari, ninamuomba Yehova anisaidie nitulie. Pia bwana yangu mupendwa ananiita kwenye telefone na anasali pamoja nami. Sala inanisaidia kabisa.” Juu ya jambo hilo Biblia inasema hivi: ‘Yehova yuko karibu na wote wanaomuitia, wote wanaomuitia yeye katika ukweli.’—Zaburi 145:18.

TUMAINI LETU JUU YA WAKATI UNAOKUJA

Katika mahubiri yake ya mulimani, Yesu alifundisha wafuasi wake kusali hivi: ‘Ufalme wako uje.’ (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu utamaliza milele mahangaiko yote yenye kuumiza. Mungu atatumia Yesu, ‘Mukuu wa Amani,’ ili ‘kukomesha vita mupaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Isaya 9:6; Zaburi 46:9) ‘Naye [Mungu] hakika atafanya hukumu kati ya vikundi vingi vya watu . . . Hawatainua upanga, taifa juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena. . . . Hakutakuwa na mutu yeyote anayewatetemesha.’ (Mika 4:3, 4) Watu wa familia wenye furaha “watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake.” (Isaya 65:21) ‘Na hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa.’—Isaya 33:24.

Leo hata tujilinde namna gani, haiwezekane kila mara kuzuia “tukio lisilotazamiwa” ao kuepuka kuwa mahali pasipofaa kwa wakati usiofaa. (Mhubiri 9:11) Tangu zamani, vita, jeuri, na magonjwa yanaua watu wazuri. Watu hao wasio na kosa wako na tumaini gani?

Watu wengi sana, ambao ni Mungu tu anajua hesabu yao, watafufuliwa. Kwa sasa, wanalala, na wako salama katika kumbukumbu kamilifu la Mungu, mupaka siku ‘wale wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho . . . watatoka.’ (Yohana 5:28, 29) Kuhusu ufufuo, Biblia inatuhakikishia hivi: “Tumaini hilo tunalo kama nanga ya nafsi ikiwa hakika na imara.” (Waebrania 6:19) Na Mungu ‘ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemufufua [Yesu] kutoka kwa wafu.’—Matendo 17:31.

Kwa sasa, hata watu wenye wanajikaza kumufurahisha Mungu wanapambana na mahangaiko. Paul, Janet, na Alona wanafikia kupiganisha mahangaiko yao kwa sababu wanafanya mambo haya ya maana: wanamukaribia Mungu kupitia sala, na wako na imani katika tumaini la Biblia juu ya wakati unaokuja. Kama vile ametendea watu hao, “Mungu anayetoa tumaini na awajaze ninyi shangwe yote na amani kwa kuamini kwenu.”—Waroma 15:13.