Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA TATU

Mungu Ana Kusudi Gani juu ya Dunia?

Mungu Ana Kusudi Gani juu ya Dunia?
  • Mungu ana kusudi gani juu ya wanadamu?

  • Mungu alipingwa namna gani?

  • Maisha yatakuwa namna gani duniani wakati ujao?

1. Mungu anakusudia kufanya dunia iwe namna gani?

MUNGU anakusudia kufanya dunia iwe mahali pazuri sana. Yehova anataka dunia ijae watu wenye furaha na wenye afya nzuri. Biblia inasema kama ‘Mungu alipanda bustani katika Edeni; alichipusha kila muti wenye kutamanika kwa macho ya mutu na ulio [muzuri] kwa chakula.’ Kisha kuumba Adamu na Eva, Aliwaweka katika makao hayo mazuri na akawaambia: ‘Zaeni, muwe wengi, mujaze dunia na kuitiisha.’ (Mwanzo 1:28; 2:8, 9, 15) Kwa hiyo, Mungu alikusudia wanadamu wazae watoto, waeneze paradiso hiyo duniani pote, na kuwatunza wanyama.

2. (a) Namna gani tunajua kama kusudi la Mungu juu ya dunia litatimia? (b) Biblia inasema watu wataishi milele wapi?

2 Unawazia kama kusudi hilo la Yehova Mungu la kufanya wanadamu waishi katika paradiso duniani litatimia siku fulani? Mungu anasema hivi: “Mimi nimesema hilo, pia nitalitenda.” (Isaya 46:9-11; 55:11) Hakika, Mungu atatimiza kabisa kusudi lake! Anasema kama ‘hakuiumba [dunia] bila sababu’ lakini “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Mungu alitaka watu wa namna gani waishi duniani? Naye alitaka waishi duniani kwa miaka ngapi? Biblia inajibu: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4.

3. Leo maisha yako namna gani duniani, na hilo linatokeza maulizo gani?

3 Ni wazi kama kusudi hilo halijatimia. Leo, watu wanagonjwa na kufa; na tena wanaendelea kupigana na kuuana. Kwa kweli, Mungu hakukusudia dunia iwe kama ilivyo leo! Kulitokea nini? Sababu gani kusudi la Mungu juu ya dunia halikutimia? Matatizo hayo yalianzia mbinguni, na kwa hiyo hakuna kitabu chochote cha historia kilichoandikwa na mwanadamu kinachoweza kututolea majibu.

MUPINZANI FULANI ANAJITOKEZA

4, 5. (a) Ni nani kwa kweli aliyezungumuza na Eva kupitia nyoka? (b) Namna gani mutu muzuri na mwaminifu anaweza kujifanya mwenyewe kuwa mwizi?

4 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinazungumuzia namna kiumbe fulani alimupinga Mungu katika bustani ya Edeni. Anaitwa “nyoka,” lakini kwa kweli yeye hakuwa nyoka. Katika kitabu cha mwisho cha Biblia yeye anaitwa “Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.” Tena anaitwa “yule nyoka wa zamani.” (Mwanzo 3:1; Ufunuo 12:9) Malaika huyo mwenye nguvu na asiyeonekana, alitumia nyoka ili kuzungumuza na Eva. Alifanya ionekane kama vile nyoka ndiye aliyekuwa akisema. Wakati Mungu alipotayarisha dunia kwa ajili ya wanadamu, kiumbe huyo wa kiroho aliona pia jambo hilo.​—Ayubu 38:4, 7.

5 Kwa kuwa kila kitu Yehova aliumba ni kikamilifu, basi ni nani aliyemufanya “Shetani Ibilisi”? Kwa kifupi, kati ya wana wa kiroho wa Mungu, mumoja alijifanya mwenyewe kuwa Ibilisi. Je, jambo hilo linawezekana? Ndiyo. Jua kama mutu muzuri na mwaminifu anaweza kujifanya mwenyewe kuwa mwizi. Hilo linaweza kutokea namna gani? Mutu anaweza kuacha tamaa mbaya iingie katika moyo wake. Basi akiacha tamaa hiyo iendelee kubaki katika moyo wake, tamaa hiyo inaweza kukomaa. Kisha, akipata nafasi, anaweza kutenda kulingana na tamaa hiyo mbaya ambayo amekomalisha moyoni mwake.​—Yakobo 1:13-15.

6. Namna gani mwana mumoja wa Mungu alijifanya mwenyewe Shetani Ibilisi?

6 Hilo ndilo jambo lililotokea kwa Shetani Ibilisi. Labda alisikia wakati Mungu aliwaambia Adamu na Eva wazae watoto na kuijaza dunia. (Mwanzo 1:27, 28) Kwa hiyo, Shetani aliwaza kama wanadamu wote wanaweza kumuabudu yeye kuliko kumuabudu Mungu. Basi tamaa hiyo mbaya ikaanza kukomaa katika moyo wake. Mwishowe, akatimiza tamaa yake kwa kumudanganya Eva na kumusingizia Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Kwa hiyo akajifanya “Ibilisi,” jina linalomaanisha “Musingiziaji.” Wakati huohuo, akajifanya pia “Shetani,” jina linalomaanisha “Mupinzani.”

7. (a) Kwa nini Adamu na Eva walikufa? (b) Kwa nini sisi watoto wa Adamu tunazeeka na kufa?

7 Kwa kutumia uongo na werevu, Shetani Ibilisi aliwafanya Adamu na Eva wakose kumutii Mungu. (Mwanzo 2:17; 3:6) Mwishowe, walikufa kama Mungu alivyosema. (Mwanzo 3:17-19) Adamu alipofanya zambi alipoteza ukamilifu, kwa hiyo, sisi watoto wake wote tuliriti zambi kutoka kwake. (Waroma 5:12) Hali hiyo inaweza kulinganishwa na chombo kinachotumiwa ili kutengeneza mikate. Ikiwa chombo hicho kina alama fulani, kila mukate unaotengenezwa humo utakuwa na alama hiyo, sivyo? Vilevile, kila mwanadamu ameriti kutokamilika kutoka kwa Adamu. Ndiyo sababu wanadamu wote wanazeeka na kufa.​—Waroma 3:23.

8, 9. (a) Inaonekana ni nini iliyokuwa mashitaka ya Shetani? (b) Kwa nini Mungu hakuwaua waasi hao mara moja?

8 Shetani alipowafanya Adamu na Eva watende zambi, hakika alianzisha uasi juu ya Mungu. Hivyo, alipinga namna ya Yehova ya kutawala. Ni kama vile Shetani alisema hivi: ‘Mungu ni mutawala mubaya. Anasema uongo na anawaima watu wake vitu vizuri. Wanadamu hawana lazima ya kutawaliwa na Mungu. Wanaweza kujichagulia mema na mabaya. Na mimi nikiwatawala watakuwa na maisha mazuri zaidi.’ Namna gani Mungu angejibu mashitaka hayo yenye kumuchafua? Watu fulani wanawaza kama ingekuwa vizuri Mungu awaue waasi hao mara moja. Lakini, je, kufanya hivyo kungejibu kweli mashitaka hayo ya Shetani? Je, kungeonyesha kama namna ya Mungu ya kutawala ndiyo nzuri?

9 Yehova hakuwaua waasi hao mara moja kwa sababu yeye ni mwenye haki. Aliona kama iliomba wakati fulani upite ili kujibu mashitaka hayo kwa njia nzuri na kuonyesha kabisa kama Shetani ni muongo. Kwa hiyo, Mungu aliona vizuri kuwaacha wanadamu wajitawale kwa wakati fulani wakiongozwa na Shetani. Sura ya 11 itaeleza kwa nini Yehova aliamua hivyo na kwa nini anaacha wakati wa kutosha upite mbele ya kukata mambo. Basi, ni vizuri kujiuliza: Adamu na Eva walikuwa na sababu yoyote ya kumuamini Shetani, aliyekuwa hajawafanyia jambo lolote nzuri? Je, walikuwa na sababu yoyote ya kuamini kama Yehova, aliyekuwa amewatolea vitu vyote walivyokuwa navyo, alikuwa mutu mubaya na muongo? Wewe ungefanya namna gani?

10. Namna gani unaweza kumujibu Shetani ili kuonyesha kama unamuunga Yehova mukono?

10 Ni vizuri kuwaza juu ya maulizo hayo kwa sababu kila mumoja wetu anapaswa pia kumujibu Shetani juu ya mashitaka hayo. Ndiyo, una nafasi ya kumujibu Shetani ili kuonyesha kama unamuunga Yehova mukono. Unaweza kumukubali Yehova kuwa Mutawala wako na kuonyesha kama Shetani ni muongo. (Zaburi 73:28; Methali 27:11) Inahuzunisha sana kuona kama leo ni watu wachache tu ndio wanaofanya hiyo. Hilo linatokeza ulizo hili la lazima, Je, Biblia inafundisha kama Shetani ndiye mutawala wa dunia hii?

NI NANI ANAYEITAWALA DUNIA HII?

Namna gani Shetani angeahidi kumupa Yesu falme zote za dunia ikiwa hazikuwa zake?

11, 12. (a) Namna gani Shetani alionyesha kama yeye ndiye mutawala wa dunia hii alipomushawishi Yesu? (b) Ni maandiko gani mengine yanayoonyesha kama Shetani ndiye mutawala wa dunia hii?

11 Yesu hakupinga kama Shetani ndiye anayeitawala dunia hii. Siku fulani, kwa njia ya muujiza Shetani alimuonyesha Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Kisha akamuahidi Yesu hivi: “Nitakupa mambo yote hayo ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” (Mathayo 4:8, 9; Luka 4:5, 6) Jiulize hivi: Ikiwa Shetani haiko mutawala wa falme zote za dunia, namna gani angeweza kumutolea Yesu falme hizo? Ikiwa Shetani hakuwa mutawala wa falme hizo, Yesu angepinga jambo hilo.

12 Kwa kweli, Yehova ndiye Mungu Mweza-Yote, Muumbaji wa ulimwengu wote wa ajabu. (Ufunuo 4:11) Lakini, hakuna andiko la Biblia linalosema kama Yehova Mungu ao Yesu Kristo ni watawala wa dunia hii. Yesu alimuita Shetani ‘mutawala wa ulimwengu huu.’ (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Hata Biblia inamuita Shetani Ibilisi ‘mungu wa mufumo huu wa mambo.’ (2 Wakorintho 4:3, 4) Mutume Yohana aliandika juu ya Shetani hivi: ‘Ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za yule muovu.’​—1 Yohana 5:19.

NAMNA UTAWALA WA SHETANI UTAKAVYOONDOLEWA

13. Sababu gani tunahitaji dunia mupya?

13 Dunia inaendelea kuwa mahali penye hatari, siku baada ya siku. Inajaa maaskari wenye kupigana vita, viongozi wa politike wanaodanganya watu, viongozi wa kidini wanafiki, na watu wanaokusudia kutenda mambo mabaya tu. Hakuna mutu anayeweza kuondoa mambo hayo. Biblia inasema kama hivi karibuni, kwenye vita yake ya Har-Magedoni, Mungu atayaondoa mambo yote yenye kuharibu dunia hii na atafanya dunia mupya ya haki.​—Ufunuo 16:14-16.

14. Mungu amemuchagua nani ili awe Mutawala wa Ufalme Wake, na juu ya hilo Biblia ilisema nini tangu zamani?

14 Yehova Mungu alimuchagua Yesu Kristo awe Mutawala wa Ufalme Wake wa mbinguni ao serikali Yake. Tangu zamani Biblia ilisema hivi: ‘Kwa maana kuna mutoto ambaye amezaliwa kwetu, kuna mwana ambaye tumepewa; na utawala wa ukuu utakuwa juu ya bega lake. Naye ataitwa Mukuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.’ (Isaya 9:6, 7) Juu ya serikali hiyo, Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Kama tutakavyojifunza, karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa serikali zote za dunia hii, nao utachukua nafasi ya serikali hizo. (Danieli 2:44) Kisha Ufalme wa Mungu utaifanya dunia yote kuwa paradiso.

DUNIA MUPYA INAKARIBIA!

15. ‘Dunia mupya’ inamaanisha nini?

15 Biblia inatuambia hivi: ‘Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mupya na dunia mupya, na humo [haki itakakaa].’ (2 Petro 3:13; Isaya 65:17) Nyakati fulani Biblia inatumia neno “dunia,” ili kumaanisha watu wanaoishi duniani. (Mwanzo 11:1) Kwa hiyo, ‘dunia mupya’ inamaanisha watu wanaokubaliwa na Mungu.

16. Wale wanaokubaliwa na Mungu watapata nini, na tunapaswa kufanya nini ili kupokea zawadi hiyo?

16 Yesu aliahidi kama katika dunia mupya, wale wanaokubaliwa na Mungu watapata “uzima wa milele.” (Marko 10:30) Tafazali, fungua Biblia yako kwenye Yohana 3:16 na 17:3, na usome yale ambayo Yesu alisema tunapaswa kufanya ili kupata uzima huo wa milele. Acha sasa tuone baraka watakazopata wale wanaostahili kuingia katika dunia itakayokuwa Paradiso.

17, 18. Sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kama kutakuwa amani na usalama duniani pote?

17 Hakutakuwa tena mambo mabaya, vita, uvunjaji wa sheria, na jeuri. ‘Mutu mubaya hatakuwako tena. Bali wapole wataimiliki dunia.’ (Zaburi 37:10, 11) Kutakuwa amani kwa kuwa ‘Mungu atakomesha vita mupaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 2:4) Kisha ‘muadilifu atachipuka, na wingi wa amani mupaka mwezi utakapokuwa haupo tena,’ yaani, milele!​—Zaburi 72:7.

18 Waabudu wa Yehova wataishi kwa usalama. Nyakati zote ambazo Waisraeli walimutii Mungu, waliishi kwa usalama. (Walawi 25:18, 19) Itakuwa ajabu sana kufurahia usalama kama huo katika Paradiso!​—Isaya 32:18; Mika 4:4.

19. Namna gani tunajua kama tutakuwa na chakula kingi katika dunia mupya ya Mungu?

19 Kutakuwa na chakula kingi. Mutunga-zaburi aliimba hivi: “Kutakuwa na wingi wa [chakula] duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.” (Zaburi 72:16) Yehova Mungu atawabariki waadilifu wake, na “hakika dunia itatoa mazao yake.”​—Zaburi 67:6.

20. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kama dunia nzima itakuwa paradiso?

20 Dunia nzima itakuwa paradiso. Wanadamu watajenga nyumba nzuri na watapanda bustani zenye kupendeza katika sehemu zilizoharibiwa na wanadamu wenye zambi. (Isaya 65:21-24; Ufunuo 11:18) Polepole, dunia nzima itafikia kuwa paradiso yenye kupendeza na kuzaa matunda sana kama bustani ya Edeni. Tena, Mungu ‘ataufumbua mukono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’​—Zaburi 145:16.

21. Ni nini kinachoonyesha kama wanadamu na wanyama wataishi pamoja kwa amani?

21 Wanadamu na wanyama wataishi pamoja kwa amani. Wanyama wa porini na wanyama wa kufugwa watakula pamoja. Hata mutoto mudogo hataogopa wanyama walio hatari leo.​—Isaya 11:6-9; 65:25.

22. Je, magonjwa yatakuwapo katika dunia mupya?

22 Magonjwa hayatakuwapo tena. Yesu, Mutawala wa Ufalme wa Mungu huko mbinguni, atawaponyesha watu wengi sana kuliko wale alioponyesha alipokuwa duniani. (Mathayo 9:35; Marko 1:40-42; Yohana 5:5-9) Kwa hiyo, ‘hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa.’​—Isaya 33:24; 35:5, 6.

23. Kwa nini ufufuo utatuletea furaha kubwa?

23 Watu tuliowapenda waliokufa watafufuliwa ili kuishi milele. Wale wote waliokufa walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa. “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”​—Matendo 24:15; Yohana 5:28, 29.

24. Je, wewe pia unafurahia wazo la kuishi katika Paradiso hapa duniani?

24 Mambo mazuri sana yanawangojea wale wanaoamua kujifunza juu ya Yehova Mungu, Muumbaji wetu Mukubwa, na kumutumikia! Paradiso itakayokuwa duniani wakati ujao ndio paradiso ambayo Yesu alimuahidi yule mutenda-mabaya aliyetundikwa pamoja naye. Alimuambia hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Ni jambo la lazima tujifunze mengi juu ya Yesu Kristo, kwa sababu tutapata baraka hizo zote kupitia Yesu.