Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA SITA

Watu Waliokufa Wako Wapi?

Watu Waliokufa Wako Wapi?
  • Ni jambo gani linalowapata watuwanapokufa?

  • Sabagu gani watu wanakufa?

  • Kujua ukweli juu ya kifo kunaweza kumufariji mutu?

1-3. Ni maulizo gani ambayo watu wanajiuliza juu ya kifo, na dini mbalimbali zinatoa majibu gani?

HAYO ni maulizo ambayo watu wamejiuliza kwa miaka mingi. Ni maulizo ya lazima. Kila mutu, iwe nani ao anaishi wapi, angependa kupata majibu ya maulizo hayo.

2 Katika Sura ya 5, tulijifunza namna zabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo ilivyofungulia wanadamu njia inayoongoza kwenye uzima wa milele. Tena tulijifunza kama Biblia ilisema kuna wakati ambapo “kifo hakitakuwapo tena.” (Ufunuo 21:4) Lakini kwa sasa, watu wanaendelea kufa. Sulemani, Mufalme mwenye hekima, alisema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa.” (Mhubiri 9:5) Tunafanya yote tuwezayo ili kuishi maisha marefu. Hata hivyo, tunajiuliza tutakuwa namna gani tutakapokufa.

3 Tunaomboleza tunapofiwa na watu tuliopenda sana. Labda tunaweza kujiuliza: ‘Wako wapi? Wanateseka mahali walipo? Wanaweza kutulinda? Tunaweza kuwasaidia? Tutawaona tena siku fulani?’ Dini zinatoa majibu tofauti kwa maulizo hayo. Dini fulani zinafundisha kama ikiwa ulikuwa mutu muzuri utaenda mbinguni, lakini, ikiwa ulikuwa mutu mubaya utaenda katika moto wa mateso. Dini zingine zinafundisha kama mutu anapokufa, anaenda kuishi pamoja na wazazi wa zamani waliokufa walio katika makao fulani yasiyoonekana. Lakini, zingine zinafundisha kama mutu anapokufa, anaenda mahali fulani ambako watu waliokufa wanangojea, ili ahukumiwe na kisha anazaliwa tena katika mwili mwingine.

4. Dini nyingi zina wazo gani moja la musingi juu ya kifo?

4 Dini zote hizo zinafundisha hivyo kwa sababu zina wazo moja la musingi, yaani, mwanadamu ana sehemu fulani ndani yake inayotoka na kuendelea kuishi mwili unapokufa. Dini karibu zote, za zamani na za sasa, zinafundisha kama tunaendelea kuishi milele kwa njia fulani na katika hali hiyo tunaendelea kuwa na uwezo wa kuona, kusikia, na kuwaza. Lakini, hiyo ni kweli? Ikiwa tuna uwezo wa kuona, kusikia, na kuwaza ni kwa sababu ubongo wetu unafanya kazi, sivyo? Lakini mutu anapokufa, ubongo wake unaacha kufanya kazi. Ubongo unapoacha kufanya kazi, mutu hawezi kukumbuka jambo lolote, hawezi kufurahi tena ao kuhuzunika, hawezi kusikia tena wala kuona.

KWA KWELI NI JAMBO GANI LINALOMUPATA MUTU ANAPOKUFA?

5, 6. Biblia inafundisha nini juu ya hali ya watu waliokufa?

5 Yehova, Muumbaji wa ubongo anajua kabisa jambo linalomupata mutu anapokufa, hilo si jambo ngumu kwake. Anajua kifo ni nini, na katika Biblia, Neno lake, anaeleza hali ya watu waliokufa. Biblia inafasiria waziwazi kama mutu anapokufa, haishi tena. Kifo ni kinyume cha uzima. Watu waliokufa hawaoni, hawasikii, wala kuwaza. Hakuna sehemu yoyote iliyo ndani ya mutu inayotoka na kuendelea kuishi mwili unapokufa. Mutu hana nafsi ao roho isiyoweza kufa. *

Moto wa buji ulienda wapi?

6 Kisha Sulemani kusema kama walio hai wanajua kama watakufa, yeye aliandika: “Wafu, hawajui lolote kamwe.” Kisha akaeleza fundisho hilo la lazima kwa kusema kama watu waliokufa hawawezi kupenda wala kuchukia na kama “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika kaburi.” (Mhubiri 9:5, 6, 10) Tena andiko la Zaburi 146:4 linasema kama mutu anapokufa, ‘mawazo yake yanapotea.’ Sisi wanadamu tunakufa na hakuna sehemu iliyo ndani ya mwandamu inayotoka na kuendelea kuishi mwili unapokufa. Maisha yetu ni kama moto wa buji. Moto huo unapozimika, hauendi mahali popote, haupo tena.

MAMBO AMBAYO YESU ALIFUNDISHA JUU YA KIFO

7. Yesu alifananisha kifo na nini?

7 Yesu Kristo alizungumuzia hali ya watu waliokufa. Wakati fulani, Yesu alipata habari kama rafiki yake Lazaro amekufa. Akawaambia wanafunzi wake hivi: ‘Lazaro rafiki yetu anapumuzika.’ Wanafunzi wake waliwaza kama Lazaro anapumuzika katika usingizi ili kupata nguvu kwa sababu alikuwa mugonjwa. Hawakuelewa maneno ya Yesu. Basi, Yesu akawaambia waziwazi hivi: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Unaona kama Yesu alifananisha kifo na usingizi ao kupumuzika. Lazaro hakuwa mbinguni wala katika moto wa mateso. Hakuwa pamoja na malaika ao pamoja na wazazi wa zamani waliokufa wala hakuwa akizaliwa tena katika mwili mwingine. Alikuwa akipumuzika katika kifo, kama vile mutu anayelala usingizi muzito bila kuota ndoto. Maandiko mengine yanafananisha pia kifo na usingizi. Kwa mufano, watu walipomuua mwanafunzi Stefano kwa kumupiga majiwe, Biblia inasema kama ‘alilala usingizi.’ (Matendo 7:60) Tena mutume Paulo alizungumuzia watu fulani wa siku zake ambao walikuwa “wamelala usingizi” katika kifo.​—1 Wakorintho 15:6.

Yehova aliumba watu ili waishi milele duniani

8. Namna gani tunajua kama Mungu hakuwaumba watu ili siku fulani wakufe?

8 Mungu alipoumba watu, je, aliwaumba watu hao ili siku fulani wakufe? Hapana! Yehova aliumba wanadamu ili waishi milele duniani. Kama tulivyojifunza katika kitabu hiki, Mungu alitia mwanaume na mwanamuke wa kwanza katika paradiso nzuri na yenye kupendeza. Walikuwa na afya kamilifu. Yehova aliwatakia tu mema. Je, kuna muzazi yeyote mwenye upendo ambaye angetaka kuona watoto wake wakiteseka kwa sababu ya uzee na kisha wakufe? Hakuna hata mumoja! Yehova alipenda watoto wake na alitaka waishi milele duniani katika furaha. Biblia inasema hivi juu ya wanadamu: “Wakati usio na kipimo [Yehova] ameuweka ndani ya moyo wao.” (Mhubiri 3:11) Hilo linaonyesha kama Mungu alituumba na tamaa ya kuishi milele. Na alichukua mipango ili kutimiza tamaa hiyo.

SABABU GANI WATU WANAKUFA?

9. Yehova alimukataza Adamu nini, na sababu gani haikuwa vigumu kutii amri hiyo?

9 Basi, sababu gani watu wanakufa? Ili kupata jibu, ni lazima tuchunguze yale yaliyotokea wakati kulikuwa tu mwanaume moja na mwanamuke moja duniani. Biblia inaeleza hivi: ‘Yehova Mungu akachipusha katika inchi kila muti wenye kutamanika kwa macho ya mutu na ulio [muzuri] kwa ajili ya chakula.’ (Mwanzo 2:9) Lakini, aliwakataza jambo moja. Yehova alimuambia Adamu hivi: ‘Matunda ya kila muti wa bustani unaweza kula mupaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya muti wa ujuzi wa mema na mabaya usikule, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.’ (Mwanzo 2:16, 17) Haikuwa vigumu kutii amri hiyo, kwa sababu kulikuwa miti mingine mingi ambayo Adamu na Eva wangeweza kula matunda yake. Lakini amri hiyo iliwatolea nafasi ya pekee ya kuonyesha shukrani yao kwa Yule aliyewapa kila kitu, kutia ndani uzima wao mukamilifu. Ikiwa wangetii amri hiyo, wangeonyesha pia kama Yehova ndiye Baba yao ambaye wanapaswa kuheshimu na kama wanafurahia uongozi wake wenye upendo.

10, 11. (a) Namna gani mwanaume na mwanamuke wa kwanza walifikia hatua ya kukosa kumutii Mungu? (b) Sababu gani kukosa utii kwa Adamu na Eva lilikuwa jambo nzito sana?

10 Jambo lenye kuhuzunisha ni kama mwanaume na mwanamuke wa kwanza walichagua kutomutii Yehova. Shetani aliongea na Eva kupitia nyoka, na alimuuliza hivi: ‘Je, ni kweli kwamba Mungu alisema musile matunda ya kila muti wa bustani?’ Eva akamujibu: “Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini kuhusu kula matunda ya muti ulio katikati ya bustani, Mungu amesema, ‘Musiyakule, wala musiyaguse ili musikufe.’”​—Mwanzo 3:1-3.

11 Shetani akamuambia hivi: ‘Hakika hamutakufa. Mungu anajua kwamba siku ileile mutakapokula matunda ya muti huo macho yenu yatafunguliwa, nanyi mutakuwa kama Mungu, mukijua mema na mabaya.’ (Mwanzo 3:4, 5) Shetani alimusadikisha Eva kama akikula tunda walilokatazwa, atafaidika. Kulingana na Shetani, Eva angejichagulia yaliyo mema na mabaya; angefanya kile anachotaka. Tena Shetani alimusingizia Yehova kama alisema uongo kwa kuwaambia kama watakufa wakikula tunda la muti huo. Eva alimuamini Shetani; kwa hiyo akachukua tunda la muti huo na akakula. Kisha akamupa bwana yake, naye akakula pia. Walijua vizuri kama walikuwa wakifanya jambo ambalo Mungu aliwakataza. Walipokula tunda la muti huo, walikosa kutii kwa makusudi amri iliyokuwa rahisi na isiyoomba mambo mengi. Walimuzarau Baba yao wa mbinguni na mamlaka yake. Hawakuwa na sababu yoyote ya kukosa kumutii Muumbaji wao mwenye upendo!

12. Ni mufano gani unaoweza kutusaidia tuelewe namna Yehova alivyojisikia Adamu na Eva walipomupinga?

12 Tuchukue mufano: Unaweza kujisikia namna gani ikiwa mutoto wako uliyetunza vizuri anakosa kukutii kwa kufanya jambo linaloonyesha kama hakuheshimu hata kidogo na hakupendi? Hilo linaweza kukuhuzunisha sana, sivyo? Basi, wazia namna Yehova alivyojisikia Adamu na Eva walipomupinga.

Adamu alitoka katika mavumbi, na alirudi katika mavumbi

13. Kulingana na maneno ya Yehova, Adamu angekuwa namna gani wakati angekufa, na maneno hayo yanamaanisha nini?

13 Yehova hakuwa na sababu ya kuwaacha Adamu na Eva waliokosa utii waendelee kuishi milele. Walikufa, kama vile tu Mungu alivyosema. Hawakuendelea kuishi. Hawakuenda kuishi katika makao fulani yasiyoonekana. Tunajua hivyo kwa sababu ya maneno ambayo Yehova alimuambia Adamu alipokosa kutii. Alimuambia hivi: ‘Utarudi katika udongo, kwa kuwa ulitolewa katika huo. Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi katika mavumbi.’ (Mwanzo 3:19) Mungu alimuumba Adamu kwa mavumbi ya udongo. (Mwanzo 2:7) Mbele ya kuumbwa, Adamu hakuwapo. Kwa hiyo, Yehova alipomuambia Adamu kama atarudi katika mavumbi, alimaanisha kama Adamu hatakuwapo tena. Adamu angekuwa tu kama vile mavumbi yaliyotumiwa kumuumba yalivyo, yaani, bila uzima.

14. Sababu gani watu wanakufa?

14 Adamu na Eva wangekuwa wazima mupaka leo, lakini walikufa kwa sababu walichagua kutomutii Mungu, walitenda zambi. Sisi watoto wa Adamu tunakufa kwa sababu sisi wote tuliriti zambi na kifo kutoka kwake. (Waroma 5:12) Zambi hiyo ni kama ugonjwa mubaya sana ulioritiwa ambao hakuna mutu anayeweza kuuepuka. Zambi ilileta kifo, na kifo ni laana. Kifo ni adui yetu, si rafiki. (1 Wakorintho 15:26) Sisi ni wenye shukrani sana kwa kuwa Yehova alitoa zabihu ya ukombozi ili kutuokoa kutokana na adui huyo asiye na huruma!

KUJUA UKWELI JUU YA KIFO KUNAFARIJI SANA

15. Sababu gani ni jambo lenye kufariji kujua ukweli juu ya kifo?

15 Mafundisho ya Biblia juu ya hali ya watu waliokufa yanafariji. Kama tulivyojifunza, watu waliokufa hawasikii maumivu wala huzuni. Hatuna sababu yoyote ya kuwaogopa, kwa kuwa hawawezi kututendea vibaya. Hatuwezi kuwasaidia, nao hawawezi kutusaidia. Hatuwezi kuzungumuza nao, wala wao hawawezi kuzungumuza na sisi. Viongozi wengi wa dini wanadanganya watu kwa kufundisha kama wao wanaweza kusaidia watu waliokufa, na watu wanaowaamini wanawapa feza. Lakini kujua ukweli juu ya kifo kunatulinda ili tusidanganywe na wale wanaofundisha uongo kama huo.

16. Mafundisho ya dini nyingi yanaongozwa na nani, na namna gani?

16 Je, dini yako inafundisha yale Biblia inafundisha juu ya hali ya watu waliokufa? Dini nyingi hazifundishi yale Biblia inafundisha. Sababu gani? Kwa sababu mafundisho ya dini hizo yanaongozwa na Shetani. Anatumia dini za uongo ili kufanya watu waamini kama baada ya mwili kufa, wataendelea kuishi katika makao fulani yasiyoonekana. Hilo ni fundisho moja kati ya mafundisho ya uongo ambayo Shetani anatumia ili kuwatenganisha watu na Mungu. Anafanya hivyo namna gani?

17. Sababu gani fundisho la mateso ya milele linamuvunjia Yehova heshima?

17 Kama tulivyoona, dini fulani zinafundisha kama ikiwa mutu alikuwa mubaya, anapokufa anaenda kuteseka milele katika moto wa mateso. Fundisho hilo linamuvunjia Mungu heshima. Yehova ni Mungu mwenye upendo na yeye hawezi hata kidogo kuwatesa watu hivyo. (1 Yohana 4:8) Kwa mufano: Ikiwa mutu fulani anamuazibu mutoto wake asiyetii kwa kumuunguza mikono katika moto, utawaza nini juu ya mutu huyo? Unaweza kumuheshimu? Utapendezwa naye? Utamuona kuwa mutu mubaya sana, sivyo? Shetani anataka tuamini kama Yehova anawatesa watu milele katika moto wa mateso!

18. Ni fundisho gani la uongo linalowachochea watu waabudu watu waliokufa?

18 Tena, Shetani anatumia dini fulani ili kufundisha kama watu wanaokufa wanakuwa viumbe vya kiroho na kwa hiyo watu walio wazima wanapaswa kuwaheshimu na kuwaabudu. Fundisho hilo linaonyesha kama roho za watu waliokufa zinaweza kuwa rafiki wazuri ao adui wenye kuogopesha. Watu wengi wanaamini uongo huo. Wanaogopa watu waliokufa, wanawaheshimu na kuwaabudu. Lakini Biblia inafundisha kama watu waliokufa wanalala usingizi na kama tunapaswa kumuabudu Yehova Mungu pekee yake, Muumbaji wetu anayetutolea kila kitu tunachohitaji.​—Ufunuo 4:11.

19. Kujua ukweli juu ya kifo kunatusaidia kuelewa vizuri fundisho lingine gani la Biblia?

19 Kujua ukweli juu ya kifo kunatulinda tusidanganywe na mafundisho ya dini za uongo. Kunatusaidia pia kuelewa mafundisho mengine ya Biblia. Kwa mufano, unapoelewa kama watu waliokufa hawaendi katika makao fulani yasiyoonekana, utaelewa vizuri ahadi ya Mungu ya uzima wa milele katika paradiso duniani.

20. Sura inayofuata itazungumuzia ulizo gani?

20 Zamani sana, Ayubu mutu mwenye haki aliuliza hivi: ‘Mutu akifa, je, anaweza kuishi tena?’ (Ayubu 14:14) Mutu anayelala usingizi katika kifo, je anaweza kuamuka? Sura inayofuata itazungumuzia fundisho hilo la Biblia, fundisho lenye kufariji sana.

^ fu. 5 Unaweza kupata habari zaidi juu ya neno “nafsi” na “roho” katika Nyongeza, ukurasa wa 208-211.