Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA KUMI NA KENDA

Alikuwa Baba Muzuri wa Familia, na Mwanaume Mwaminifu

Alikuwa Baba Muzuri wa Familia, na Mwanaume Mwaminifu

1, 2. (a) Yosefu na familia yake walipambana na tatizo gani? (b) Ni habari gani mbaya ambayo Yosefu alipaswa kumuelezea bibi yake?

YOSEFU anaweka muzigo wa mwisho kwenye mugongo wa punda. Wazia bado ni usiku katika Bethlehemu, Yosefu anaanza kufikiri, anatazama huku na huku akiwa mwenye kupapasa​-papasa punda huyo mwenye kubeba mizigo. Bila shaka, anafikiria safari ndefu ambayo yeye na familia yake wanataka kufanya ili kushuka Misri, inchi ya kigeni. Huko watu wanazungumuza luga tofauti na yao, watu wana desturi tofauti na zao; Yosefu anajiuliza namna gani familia yake itapambana na hali hizo!

2 Haikuwa vyepesi kwa Yosefu kumuelezea Maria, bibi yake mupendwa, habari hiyo, lakini alijipa moyo na akamuambia kuhusu ndoto ambayo aliota. Katika ndoto hiyo malaika alimutolea ujumbe wa Mungu kwamba Mufalme Herode anataka kumuua mutoto wao muchanga! Kwa hiyo, wanapaswa kuondoka haraka. (Soma Mathayo 2:13, 14.) Maria alihangaishwa sana na jambo hilo. Kwa nini mufalme anatafuta kumuua mutoto wake asiye na kosa lolote, asiyeweza kujilinda? Maria na Yosefu waliishiwa. Hata hivyo, waliamini yale Yehova alisema na kwa hiyo walitayarisha safari yao haraka.

3. Fasiria ni katika hali gani Yosefu na familia yake wanaondoka Bethlehemu. (Ona pia picha kwenye ukurasa unaofuata.)

3 Watu wa Bethlehemu wanalala usingizi muzito, hawajue mipango ya Herode; wakati huo wenye giza, Yosefu, Maria na Yesu wanaondoka katika muji bila mutu kujua. Yosefu anaelekeza familia yake upande wa kusini. Upande wa mashariki usiku unaanza kucha. Labda anaanza kujiuliza, namna gani seremala wa hali ya chini kama yeye ataweza kulinda familia yake yenye kushambuliwa na watu wenye nguvu zaidi? Atafanya nini ili kutimizia bibi yake na mutoto wao mahitaji yao? Ataweza kabisa kutimiza mupaka mwisho daraka hilo nzito ambalo Yehova Mungu amemupatia: kutunza na kukomalisha mutoto huyo wa pekee? Bila shaka, Yosefu iko mbele ya daraka lenye kuogopesha. Habari hii itatusaidia kuona jinsi alivyotimiza kwa uaminifu daraka lake, na hilo linaweza kuchochea baba wa familia leo na sisi wote kuiga imani ya Yosefu.

Yosefu Analinda Familia Yake

4, 5. (a) Namna gani maisha ya Yosefu yalibadilika kabisa? (b) Namna gani malaika alimutia moyo Yosefu ili akubali daraka lake nzito?

4 Miezi fulani mbele ya hapo, katika Nazareti muji wake wa kuzaliwa, maisha ya Yosefu yalibadilika kabisa kisha kumuchumbia Maria, binti ya Heli. Yosefu alimujua Maria kuwa ni binti mwaminifu na mwenye kupenda sheria za Yehova. Lakini siku fulani, akatambua kwamba ana mimba! Akakusudia kuvunja ndoa yao kwa siri ili asimupatishe Maria haya. * Lakini, katika ndoto malaika alimuelezea kwamba Maria amepata mimba kwa utendaji wa roho takatifu ya Yehova. Tena, alimuelezea kwamba mutoto ambaye Maria atazaa ‘atawaokoa watu wake kutoka katika zambi zao.’ Pia, ili kumuondoa Yosefu wasiwasi, akamuambia: ‘Usiogope kumuchukua Maria muke wako na kuenda naye nyumbani.’​—Mt. 1:18-21.

5 Kwa kuwa Yosefu ni mwanaume mwaminifu mwenye kumutii Mungu, alifanya kama vile malaika alivyomuambia. Alikubali daraka hilo lililo nzito kupita madaraka mengine, ni kusema, kumutunza mutoto asiyekuwa wake, lakini wa lazima sana machoni pa Mungu. Baadaye, kwa kutii sheria ya mufalme, Yosefu alimuchukua bibi yake aliyekuwa na mimba na kumupeleka Bethlehemu ili kujiandikisha. Na ni huko mutoto huyo anazaliwa.

6-8. (a) Ni matukio gani yanayobadilisha tena maisha ya Yosefu na familia yake? (b) Namna gani tunajua kwamba ni Shetani ndiye aliyekuwa ametuma ile “nyota”? (Soma pia maelezo ya chini.)

6 Yosefu harudishe familia yake Nazareti. Lakini, wanakaa Bethlehemu karibu kilometre 10 hivi kutoka Yerusalemu. Ni kweli kwamba wao ni masikini, lakini Yosefu anafanya yake yote ili Maria na mutoto wasikose mahitaji ya lazima wala wasipatwe na magumu. Bila kukawia wanapata mahali pa kuishi katika nyumba ndogo. Kisha, wakati Yesu anakuwa labda na zaidi ya mwaka mumoja, wakati huo yeye si kitoto kichanga tena, maisha yao yanabadilika tena kwa gafula.

7 Wanaume fulani, wanajimu (watu wanaofanya uaguzi kupitia nyota) waliotoka Mashariki wanafika, wanatoka mbali huko Babiloni. Walifuata “nyota” fulani iliyowaongoza mupaka kwenye nyumba ya Yosefu na Maria, na wanamutafuta huyo mutoto ambaye anapaswa kuwa mufalme wa Wayahudi. Wanaume hao ni watu wenye kuwa na heshima sana.

8 Iwe wanajimu hao wanajua ao hapana, wao ni wenye kuhatarisha maisha ya Yesu. Ile “nyota” waliyoona haikuwaongoza moja kwa moja Bethlehemu, lakini iliwapeleka kwanza Yerusalemu. * Walipofika huko walimuelezea Mufalme muovu Herode kwamba wanamutafuta mutoto ambaye anapaswa kuwa mufalme wa Wayahudi. Habari hiyo iliwasha hasira ya mufalme.

9-11. (a) Ni nini inayoonyesha kwamba kulikuwa na Yule aliye na nguvu zaidi kuliko Herode na Shetani, aliyekuwa anaongoza mambo? (b) Safari ya familia ya Yosefu kuenda Misri inatofautiana namna gani na hadisi za kuwazia tu?

9 Inapendeza kabisa kujua kwamba kulikuwa na Yule aliye na nguvu kuliko Herode na Shetani, aliyekuwa anaongoza mambo. Anafanya nini? Wageni hao wanapofika nyumbani mahali Yesu iko, na wanapomuona mama yake, wanatolea familia hiyo zawadi walizoleta, na hawaombe kitu chochote. Wazia namna Yosefu na Maria wanavyoshangaa kupata kwa gafula hivyo vitu vyenye bei sana: ‘zahabu na ubani na manemane!’ Wanajimu hao wanataka kurudi kwa Mufalme Herode ili wamuelezee mahali ambapo walimukuta mutoto huyo. Lakini, Yehova hawaruhusu. Kupitia ndoto, anawaagiza wanajimu hao warudi kwao kupitia njia nyingine.—Soma Mathayo 2:1-12.

10 Muda kidogo kisha wao kuondoka, malaika wa Yehova anamuonya Yosefu hivi: ‘Simama, muchukue huyo mutoto muchanga na mama yake mukimbie kuingia Misri, mukae huko mupaka nitakapokupa agizo; kwa maana Herode yuko karibu kumutafuta huyo mutoto amuangamize.’ (Mt. 2:13) Basi, kama tulivyoona hapo mwanzoni mwa sura hii, Yosefu anatii kwa haraka. Uzima wa mutoto huyo ndilo jambo la maana kuliko vitu vingine vyote, na kwa hiyo, anaondoka na familia yake na kuingia Misri. Kwa kuwa wanajimu hao wapagani walipatia familia hiyo zawadi hizo za bei sana, Yosefu alikuwa sasa na vitu ambavyo vingemusaidia kutimizia watu wa familia yake mahitaji yao huko Misri.

Yosefu alijinyima na alitenda bila kukawia ili kumulinda mutoto wake

11 Hadisi za kuwazia tu na maandishi ambayo hayakuongozwa na roho takatifu yaliyoongezwa baadaye kwenye Maandiko Matakatifu, yanapozungumuzia safari hiyo ya kuenda Misri, yanaitia chumvi sana. Kwa mufano, maandishi hayo yanasema kwamba mutoto Yesu alifupisha safari hiyo kimuujiza, kwamba aliwashinda wanyanganyi, na hata kwamba aliamuru matawi ya mutende yakunjame ili mama yake achume matunda. * Lakini ukweli ni kwamba safari yao ilikuwa ndefu, yenye kuchokesha na iliwaelekeza mahali wasipojua.

Yosefu alifanya kazi kwa bidii ili familia yake isikose mahitaji ya kimwili

12. Mufano wa Yosefu unaweza kuwafundisha wazazi nini?

12 Mufano wa Yosefu unaweza kuwafundisha wazazi mambo mengi. Alikuwa tayari kutia pembeni kazi yake, alijinyima mambo fulani ili kulinda familia yake isipatwe na hatari. Ni wazi kwamba aliona jambo hilo kuwa ni daraka takatifu alilopewa na Yehova. Leo, ulimwengu muovu wa Shetani unaweza kuwachochea vijana kufanya mambo mabaya, ambayo yanaweza kuwafanya wateseke sana na hata kuharibisha maisha yao. Ni jambo lenye kufurahisha sana kuona namna baba na mama wanavyomuiga Yosefu, wanafanya yao yote ili kuwalinda watoto wao na uvutano mubaya wa ulimwengu!

Yosefu Anatimizia Watu wa Familia Yake Mahitaji Yao

13, 14. Sababu gani Yosefu na Maria wanaamua kulea watoto wao katika Nazareti?

13 Inaonekana kwamba familia hiyo haikubaki muda murefu huko Misri, kwa sababu kisha muda kidogo malaika anamujulisha Yosefu kwamba Herode amekwisha kufa. Basi, Yosefu anarudisha familia yake katika inchi yao. Unabii fulani uliotabiriwa zamani ulisema kwamba Yehova ataita Mwana wake “kutoka Misri.” (Mt. 2:15) Kwa hiyo, Yosefu anashiriki katika utimizo wa unabii huo, lakini sasa atapeleka familia yake kuishi wapi?

14 Yosefu ni muangalifu sana. Kwa hekima yeye hamutumaini Arkelausi, mufalme aliyetawala kisha Herode, ambaye pia ni mutu mukorofi na muuaji. Mungu anamuongoza Yosefu kuipeleka familia yake Nazareti katika muji wa Galilaya, upande wa kaskazini mbali na Yerusalemu ili mutoto Yesu asiangamizwe. Ni huko ndiko yeye na Maria watalea watoto wao.—Soma Mathayo 2:19-23.

15, 16. Kazi ya Yosefu ya seremala ilikuwa kazi ya namna gani, na inawezekana alitumia vyombo gani?

15 Familia hiyo ina maisha ya hali ya chini, kwa hiyo, maisha yao hayakuwa rahisi. Biblia inaposema kwamba Yosefu alikuwa seremala, inatumia neno linaloonyesha kazi mbalimbali za mbao, kama vile, kukata miti, kuikokota, kuikausha na kuifanya kuwa mbao ili kuzitumia kujenga nyumba, kutengeneza mashua, vilalo vidogo, shario (shareti), magurudumu (mipeto), nira, na vifaa mbalimbali vya kulima mashamba. (Mt. 13:55) Ilikuwa kazi ngumu iliyoomba mutu awe na nguvu nyingi. Hapo zamani, mara nyingi seremala alifanya kazi karibu na mulango wa nyumba yake ndogo ao katika kibanda kilichojengwa pembeni ya nyumba yake.

16 Yosefu alitumia vyombo mbalimbali vya kazi ya seremala, na bila shaka aliriti vingine kutoka kwa baba yake. Tunaweza kufikiri kwamba alitumia vyombo kama vile hama ya chuma na ya mbao, shoka, kipande cha chuma chenye kuninginia kwenye uzi ili kupima usawa wa ukuta, kifaa cha kuchonga na kutoboa mashimo kwenye mbao, na labda misumari fulani, ingawa vifaa hivyo vilikuwa vya bei kali.

17, 18. (a) Yesu anajifunza nini anapoangalia jinsi baba yake mulezi anavyofanya kazi? (b) Sababu gani Yosefu anapaswa kufanya kazi yake kwa bidii kabisa?

17 Unaweza kuwazia namna kijana mudogo Yesu anavyomutazama baba yake mulezi anapofanya kazi. Anafungua kabisa macho na anatazama vizuri kila jambo Yosefu anafanya; bila shaka, anafurahia kuona mabega yenye nguvu ya baba yake, na vilevile mikono yenye kujaa mishipa na yenye kufanya kazi kwa ufundi, na namna anavyotumia macho yake kwa akili sana. Labda Yosefu pia anaanza kumufundisha kijana Yesu jinsi ya kufanya kazi rahisi kama vile kulainisha sehemu zenye kukwaruza za mbao kwa kutumia ngozi ya samaki iliyokaushwa. Anamufasiria tofauti kati ya miti mbalimbali anayotumia, kama vile, mukuyu, mutini ao muzeituni na miti mingine.

Yosefu alimufundisha mutoto wake kazi ya seremala

18 Yesu anajionea pia kwamba mikono hiyo yenye nguvu inayojua kukata miti, kuichonga vizuri, na kuunganisha mbao, ni hiyohiyo pia inayowatunza kwa upendo, yeye na mama yake na wadogo yake wengine. Ndiyo, familia ya Yosefu na Maria inaongezeka, kwa sababu mwishowe wanafikia kuwa na watoto saba kutia ndani na Yesu. (Mt. 13:55, 56) Kwa hiyo, Yosefu anapaswa kufanya kazi kwa bidii kabisa ili kuwatunza na kuwalisha watu hao wote wa familia yake.

Yosefu anaelewa kwamba kazi yake ya lazima sana ni kuwasaidia watu wa familia yake wawe na uhusiano muzuri na Yehova

19. Namna gani Yosefu alikuwa anasaidia watu wa familia yake kuwa na uhusiano muzuri na Yehova?

19 Hata hivyo, Yosefu anaelewa kwamba kazi yake ya lazima sana ni kuwasaidia watu wa familia yake wawe na uhusiano muzuri na Yehova. Kwa hiyo, anachukua wakati fulani kuwa pamoja na watoto wake ili kuwafundisha juu ya Yehova Mungu na juu ya sheria zake. Kwa ukawaida, yeye na Maria wanawapeleka kwenye sinagogi, ambako Sheria inasomwa kwa sauti na kufasiriwa. Labda, wanaporudi nyumbani Yesu anamuuliza Yosefu maulizo mengi juu ya Yehova na juu ya sheria zake, na Yosefu anajikaza kumujibia. Tena, Yosefu alikuwa anaipeleka familia yake Yerusalemu kuhuzuria sikukuu zilizoamuriwa na sheria. Ili kuhuzuria Pasaka ya kila mwaka, inawezekana Yosefu alikuwa akifanya safari ya majuma mawili, ni kusema, mwendo wa kilometre 120 hivi, na kisha wangerudi nyumbani.

Yosefu alipeleka familia yake kwa ukawaida huko Yerusalemu ili kuabudu kwenye hekalu

20. Namna gani baba wa familia za Kikristo wanaweza kuiga mufano wa Yosefu?

20 Leo, baba wa familia za Kikristo wanaiga mufano huo. Wanajitolea sana kwa ajili ya watoto wao, kwa sababu wanajua kwamba kufundisha watoto wao juu ya Yehova ndilo jambo la lazima sana kuliko mambo yote, kuliko hata mahitaji yao ya kimwili. Wanafanya yote wanayoweza ili kuongoza ibada ya familia na kuwapeleka watoto wao kwenye mikutano na mikusanyiko. Kama Yosefu, wanajua kama hiyo ndio njia nzuri kuliko zote ya kutayarisha wakati ujao wa watoto wao.

‘Walihangaika Katika Akili’

21. Yosefu na familia yake walikuwa wanaiona sikukuu ya Pasaka namna gani, na ni wakati gani walitambua kwamba Yesu haiko pamoja nao?

21 Yesu ana miaka 12, na kama kawaida Yosefu anapeleka familia yake Yerusalemu. Ni sikukuu ya Pasaka, na familia nyingi kubwa​-kubwa zinafanya safari pamoja, zinapitia maeneo ya vijijini yenye mashamba ya mimea yenye kuchipuka katika kipindi cha mvua nyingi. Wanapokaribia eneo lisilo na mimea kuelekea muji mukubwa wa Yerusalemu, wengi wanaanza kuimba zaburi zinazojulikana sana walizokuwa wakiimba wakati wa kupanda Yerusalemu. (Zab. 120-134) Inaonekana muji unajaa sana na mamia ya maelfu ya watu. Kisha sikukuu, familia zinaanza kurudi nyumbani. Labda kwa sababu Yosefu na Maria wana mambo mengi ya kufanya, wanafikiri Yesu ni mwenye kuwa pamoja na wasafiri wengine, labda hata na watu wengine wa jamaa. Lakini, kisha kutembea siku nzima ndipo wanashituka na kutambua kama Yesu haiko pamoja nao!—Lu. 2:41-44.

22, 23. Yosefu na Maria wanafanya nini wanapotambua kwamba mutoto Yesu haiko pamoja nao, na mwishowe wakati wanamupata Maria anamuambia nini?

22 Katika hali ya wasiwasi, wanarudi haraka Yerusalemu wakimutafuta Yesu kila mahali. Wanapofika huko katika muji, hakuna tena watu wengi, na mambo yote yanaonekana kwao kuwa tofauti sasa wanapovuka barabara za muji huku na huku, na kuita kwa sauti mutoto wao. Wanajiuliza, ni wapi anaweza kupatikana! Kisha siku tatu za kumutafuta, bila shaka, Yosefu anaanza kufikiri kwamba ameshindwa kutimiza mugao wake mutakatifu ambao Yehova alimupatia. Mwishowe, wanapata wazo la kuenda kwenye hekalu. Huko wanatafuta juu chini mupaka wanaingia katika chumba fulani kikubwa, ambamo wanakuta wanaume wengi wenye elimu waliojua Sheria ya Musa wanakusanyika, na mutoto Yesu anakaa katikati ya wanaume hao! Wazia namna Yosefu na Maria wanasikia mioyo yao inatulizana!​—Lu. 2:45, 46.

23 Yesu anawasikiliza wanaume hao wenye elimu na anawauliza maulizo mengi. Wanaume hao wanashangazwa sana na ufahamu wa mutoto huyo na majibu yake. Hata hivyo, Maria na Yosefu wanaishiwa. Yosefu haseme lolote. Lakini, Maria anasema maneno yanayoonyesha jinsi wote wawili wanavyojisikia: ‘Mutoto, kwa nini umetutendea hivi? Tazama, baba yako na mimi tumekuwa tukikutafuta tukiwa na hangaiko la akilini.’—Lu. 2:47, 48.

24. Namna gani Biblia inaonyesha ukweli kuhusu kazi ya wazazi?

24 Ni hivyo kwa maneno machache Neno la Mungu linatuonyesha ukweli kuhusu kazi ya wazazi. Kazi hiyo inaweza kuhangaisha sana hata ikiwa mutoto ni mutu mwenye kukamilika! Katika ulimwengu tunamoishi leo, kuwa muzazi kunaweza kumuletea mutu ‘mahangaiko ya akili’ sana, lakini baba na mama wanaweza kufarijiwa kwa kujua kwamba tayari Biblia inazungumuzia matatizo ambayo wanakutana nayo.

25, 26. Namna gani Yesu anawajibia wazazi wake, na Yosefu anajisikia namna gani?

25 Ikiwa Yesu alibaki katika hekalu ni kwa sababu hapo ni mahali pekee duniani ambapo angejisikia kuwa karibu sana na Baba yake wa mbinguni, Yehova, na kufurahia kujifunza juu yake. Na kwa hiyo, anawajibu wazazi wake hivi kwa upole: ‘Kwa nini mulilazimika kunitafuta? Hamukujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?’​—Lu. 2:49.

26 Bila shaka, Yosefu alifikiria maneno hayo tena na tena. Na labda maneno hayo yalimufanya ajisikie mwenye furaha sana. Kwa nini isiwe hivyo? Yeye alimufundisha mutoto wake kwa bidii ili awe na uhusiano kama huo na Yehova Mungu. Akiwa bado kijana, tayari Yesu alijua namna baba mwenye upendo alivyo, alijua hilo kwa kuishi pamoja na Yosefu.

27. Ikiwa wewe ni baba, ni pendeleo gani ulilo nalo, na namna gani unaweza kuiga mufano wa Yosefu?

27 Ikiwa wewe ni baba mwenye upendo na mwenye kulinda watoto wako vizuri, je, unaona namna unaweza kuwasaidia watoto wako wamuone Yehova kuwa Baba yao wa mbinguni na wajifunze kwamba anawapenda na kuwalinda? Vilevile, ikiwa unawalea watoto ambao wewe haukuzaa, kumbuka mufano wa Yosefu, usiwabague na umuone kila mumoja wao kuwa ni wa maana. Uwasaidie watoto hao wamukaribie sana Baba yao wa mbinguni, Yehova Mungu.Soma  Waefeso 6:4.

Yosefu Anavumilia kwa Uaminifu

28, 29. (a) Maneno yaliyo katika andiko la Luka 2:51, 52 yanatufundisha nini juu ya Yosefu? (b) Namna gani Yosefu alimusaidia mutoto wake kuwa na hekima?

28 Biblia inatuelezea habari kidogo sana kuhusu maisha ya Yosefu, lakini hata ikiwa habari hizo ni kidogo, ni za lazima na zinaombwa kuchunguzwa kwa uangalifu. Tunasoma kwamba Yesu ‘aliendelea kujitiisha’ kwa wazazi wake. Tena tunasoma kwamba ‘Yesu aliendelea kufanya maendeleo katika hekima na ukuzi wa kimwili, akipata kibali kwa Mungu na wanadamu.’ (Soma Luka 2:51, 52.) Maneno hayo yanatufundisha mengi juu ya Yosefu. Yanatufundisha kwamba Yosefu aliendelea kuiongoza familia yake, kwa kuwa kijana wake aliyekuwa mutu mukamilifu alikuwa anaheshimu mamlaka yake na alikuwa anajitiisha kwake.

29 Tunajifunza pia kwamba Yesu aliendelea kukomaa katika hekima. Bila shaka, Yosefu alimusaidia sana kijana wake kupata hekima hiyo. Siku hizo, Wayahudi walikuwa na mawazo yasiyofaa ambayo hata leo watu wengi wanayo: Kwamba ni wanaume matajiri na watu wenye uwezo ndio wangeweza kuwa na hekima ya kwelikweli, lakini wale wanaofanya kazi za mikono, kama vile waseremala, walimaji wa mashamba, wafuaji wa vyuma, hawawezi kujua sheria, wala hukumu; na hawangepatikana mahali ambapo maneno ya fumbo yalizungumuzwa. Lakini hekima ya Yesu ilionyesha wazi kwamba mawazo hayo ni ya uongo. Bila shaka, mara nyingi alikuwa anamusikia baba yake mulezi akimufundisha vizuri kuhusu “sheria na hukumu” za Yehova, ijapokuwa Yosefu alikuwa seremala na mutu masikini! Hakika, Yosefu alifanya hivyo mara nyingi.

30. Ni mufano gani muzuri Yosefu aliwaachia baba wa familia?

30 Pia, tunaweza kuona kwamba Yosefu alimusaidia Yesu kukomaa kimwili. Kwa sababu Yosefu alimutunza vizuri, Yesu alikomaa na kuwa mwanaume mwenye afya na nguvu. Jambo lingine ni kwamba, Yesu alikuwa seremala mwenye ufundi, kwa sababu Yosefu alimufundisha kazi hiyo ya mikono. Kwa hiyo, Yesu hakujulikana tu kuwa mwana wa seremala, lakini pia alijulikana kuwa “seremala.” (Mk. 6:3) Inaonekana wazi kwamba Yosefu alimulea Yesu vizuri kabisa. Kila baba wa familia ataonyesha kama ana hekima ikiwa anamuiga Yosefu, ni kusema, kuwatayarisha watoto wake vizuri ili watakapokuwa watu wazima waweze kujitegemeza kimwili.

31. (a) Inaonekana Yosefu alikufa wakati gani? (Chukua pia maelezo katika kisanduku.) (b) Ni mufano gani wa Yosefu tunapaswa kuiga?

31 Wakati Biblia inazungumuzia juu ya kubatizwa kwa Yesu alipokuwa na miaka 30 hivi, Yosefu hatajwe tena katika historia ya Biblia. Kwa hiyo, inaonekana Maria alikuwa mujane wakati Yesu alianza kazi ya kuhubiri. (Soma kisanduku  “Yosefu Alikufa Wakati Gani?”) Hata hivyo, yale Yosefu alifanya hayawezi kusahaulika. Yeye ni mufano muzuri wa baba anayelinda watu wa familia yake, anayewatimizia mahitaji yao, na anayevumilia kwa uaminifu mupaka mwisho. Kila baba, kila kichwa cha familia, ao Mukristo yeyote anapaswa kuiga mufano wa imani wa Yosefu.

^ fu. 4 Katika siku hizo, watu waliwaona wale wenye kuchumbiana kuwa wameoana ao kufunga ndoa.

^ fu. 8 “Nyota” hiyo haikuwa nyota ya kawaida, wala haikuwa imetumwa na Mungu. Bila shaka, huo ni mupango wa Shetani wa kumuua Yesu, kwa hiyo, alitumia kitu kilichoonekana kama nyota ili kufikia kusudi hilo.

^ fu. 11 Biblia inaonyesha wazi kwamba Yesu alifanya muujiza wake wa kwanza kisha kubatizwa.—Yoh. 2:1-11.