Hamia kwenye habari

Je, Dini Zote Ni Sawa? Je, Zote Zinaongoza kwa Mungu?

Je, Dini Zote Ni Sawa? Je, Zote Zinaongoza kwa Mungu?

Jibu la Biblia

 Hapana, dini zote si sawa. Biblia ina mifano mingi ya dini zinazomchukiza Mungu. Dini hizo zinaweza kuorodheshwa chini ya vikundi viwili vya msingi.

Kikundi cha 1: Wanaoabudu miungu ya uwongo

 Katika Biblia ibada ya miungu ya uwongo inaelezewa kwa maneno kama vile “pumzi,” na “ubatili,” kuonyesha kuwa ibada hiyo haina faida. (Yeremia 10:​3-5; 16:19, 20) Yehova a Mungu aliliamuru taifa la kale la Israeli hivi: “Usiwe na miungu mingine yoyote dhidi ya uso wangu.” (Kutoka 20:​3, 23; 23:24) Waisraeli walipoabudu miungu mingine, ‘hasira ya Yehova iliwaka.’​—Hesabu 25:3; Mambo ya Walawi 20:2; Waamuzi 2:​13, 14.

 Bado Mungu ana mtazamo uleule kuelekea ibada ya hao “wanaoitwa ‘miungu.’” (1 Wakorintho 8:​5, 6; Wagalatia 4:8) Anawaamuru wale wanaotaka kumwabudu waache kushirikiana na wale walio katika dini ya uwongo, akisema hivi: “Tokeni katikati yao, na mjitenge.” (2 Wakorintho 6:​14-​17) Ikiwa dini zote ni sawa na zinawaongoza watu kwa Mungu, basi kwa nini Mungu atoe amri kama hiyo?

Kikundi cha 2: Wanaomwabudu Mungu wa kweli kwa njia ambayo haikubali

 Nyakati nyingine, Waisraeli walimwabudu Mungu kwa kutumia imani na desturi walizokopa kutoka kwenye ibada ya miungu ya uwongo, lakini Yehova alikataa kitendo chao cha kuchanganya dini ya kweli na ya uwongo. (Kutoka 32:8; Kumbukumbu la Torati 12:​2-4) Yesu aliwashutumu viongozi wa kidini wa siku zake kwa sababu ya njia waliyotumia kumwabudu Mungu; walijionyesha kwa nje kuwa watu wa kidini, hata hivyo kwa unafiki ‘waliyapuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.’​—Mathayo 23:23.

 Vivyo hivyo leo, dini inayotegemea kweli ndiyo tu inayowaongoza watu kwa Mungu. Kweli hiyo inapatikana katika Biblia. (Yohana 4:​24; 17:17; 2 Timotheo 3:​16, 17) Dini ambazo mafundisho yake yanapingana na Biblia yanawaelekeza watu mbali na Mungu. Mafundisho mengi ambayo watu wanafikiri yanatoka katika Biblia​—kutia ndani Utatu, nafsi isiyoweza kufa, na moto wa mateso​—yalitokana na watu walioabudu miungu ya uwongo. Ibada inayoendeleza mafundisho kama hayo ni ya “bure,” kwa sababu inabadili matakwa ya Mungu na mapokeo ya kidini.​—Marko 7:​7, 8.

 Mungu anachukia unafiki wa kidini. (Tito 1:​16) Ili kuwasaidia watu kumkaribia Mungu, dini inapaswa kuathiri maisha yao ya kila siku na si tu ihusishe kufuata desturi za kidini. Kwa mfano, Biblia inasema: “Ikiwa mtu yeyote anajiona kuwa mwabudu anayeshikilia vizuri namna ya ibada na bado hauongozi ulimi wake, bali anaendelea kuudanganya moyo wake mwenyewe, namna ya ibada ya mtu huyo ni ya ubatili. Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.”​—Yakobo 1:26, 27.

a Yehova ni jina la Mungu wa kweli kama inavyofunuliwa katika Biblia.