Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Ni Biashara?

Je, Dini Ni Biashara?

 Je, umegundua kwamba dini nyingi hukazia fikira kupata pesa kuliko kutoa msaada wa kiroho? Wanatangaza na kuuza bidhaa na huduma mbalimbali. Viongozi wao wengi hulipwa mishahara mikubwa na wanaishi maisha ya starehe. Fikiria mifano michache:

  •   Upelelezi uliofanywa ulifunua kwamba askofu mmoja wa kanisa Katoliki alitumia pesa za kanisa katika kipindi cha miaka 13 kulipia safari 150 za ndege ya kibinafsi na safari 200 hivi za gari la kifahari. Pia, alitumia dola milioni 4 za Marekani ili kurekebisha nyumba anayoishi inayomilikiwa na kanisa.

  •   Mhubiri katika nchi moja ya Afrika hufanya mikutano ya kidini inayohudhuriwa na makumi ya maelfu ya watu. Katika eneo la kanisa lake kubwa anauza vitu mbalimbali—kama “mafuta ya kimuujiza” pamoja na mataulo na mashati yenye picha yake. Ingawa watu wengi wanaohudhuria ni maskini, yeye ni tajiri sana.

  •   Milima miwili kati ya minne mitakatifu ya Kibudha nchini China, imeandikishwa kisheria kuwa kampuni za kibiashara. Pia, Hekalu maarufu la Shaolin linajulikana sana kwa kujihusisha na miradi mingi ya kibiashara—mtawa mkuu wa hekalu hilo anaitwa pia “Mtawa Mkurugenzi.”

  •   Makampuni makubwa ya Marekani yameanza kutafuta washauri wa kidini. Kulingana na ripoti moja, wanaiga desturi za kidini kwa kuwapatia mwongozo wa kidini wafanyakazi wao.

 Unahisije kuhusu dini ambazo zinajihusisha na biashara? Je, umewahi kujiuliza Mungu anawaonaje watu ambao wanajitafutia faida za kifedha kupitia dini?

Mungu anawaonaje watu wanaochanganya dini na biashara?

 Mungu hapendezwi na watu wanaochanganya dini na biashara. Biblia inaonyesha kwamba, aliwachukia sana makuhani waliodai kumwakilisha yeye walipofundisha “ili wapate malipo.” (Mika 3:11) Mungu alishutumu mazoea yenye pupa katika biashara ambayo yalifanya mahali pake pa ibada kuwa “pango la wanyang’anyi.”—Yeremia 7:11.

 Yesu pia alichukizwa na wale ambao walitumia dini ili kujinufaisha wenyewe kifedha. Katika siku zake, viongozi wa kidini walifaidika kupitia wafanyabiashara wenye pupa waliowaruhusu kufanya biashara ndani ya hekalu la Yerusalemu. Waliwadhulumu watu wanyoofu walioenda kufanya ibada. Kwa ujasiri Yesu aliwafukuza wafanyabiashara hao nje ya eneo la hekalu akisema: “Acheni kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya biashara!”—Yohana 2:14-16.

 Yesu alikuwa na maoni ya Mungu katika huduma yake. (Yohana 8:28, 29) Hakuwahi kuwalipisha watu alipowafundisha kumhusu Mungu. Hakuomba malipo alipofanya miujiza, kama vile kulisha waliokuwa na njaa, kuponya wagonjwa na kuwafufua wafu. Yesu hakutumia kamwe huduma yake ili kujipatia utajiri—hata hakumiliki nyumba ya kuishi.—Luka 9:58.

Wakristo wa kwanza walifanyaje ili wasichanganye ibada na biashara?

 Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba wasitafute faida ya kifedha kupitia utendaji wao wa kidini. Alisema hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Wafuasi hao wa mapema, waliojulikana kuwa Wakristo, walitii maagizo ya Yesu. Fikiria mifano michache:

  •   Mwanamume anayeitwa Simoni ambaye alitaka kuwa na cheo na nguvu na mamlaka alitaka kumpa pesa Mtume Petro ambaye alikuwa pamoja na Yesu katika huduma yake. Petro alikataa moja kwa moja pesa hizo na kumkaripia vikali kwa kusema: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulidhani utanunua zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa.”—Matendo 8:18-20

  •   Mtume Paulo alikuwa mhudumu asafiriye aliyejulikana sana. Ingawa alifanya kazi kwa bidii kwa miaka mingi katika makutaniko mengi ya Kikristo, hakuwahi kujitafutia pesa kupitia kazi yake. Yeye pamoja na Wakristo wenzake hawakuwa “wachuuzi wa neno la Mungu kama watu wengi walivyo.” (2 Wakorintho 2:17) Badala yake, Paulo aliandika hivi: “Tulifanya kazi usiku na mchana, ili tusimpe yeyote kati yenu mzigo wenye gharama, tulipowahubiria habari njema ya Mungu.”—1 Wathesalonike 2:9.

 Bila shaka, Wakristo hao wa mapema walihitaji pesa za kutegemeza kazi yao ya kuhubiri kwenye maeneo ya mbali na kutoa misaada. Lakini hawakudai malipo kwa ajili ya kazi walizofanya ili kuwasaidia wengine kumwabudu Mungu. Watu wangeweza kuchangia ikiwa wangetaka, kwa kufuata utaratibu ufuatao:

  •   2 Wakorintho 8:12: “Kwa maana ikiwa utayari upo kwanza, hukubalika zaidi kulingana na kile ambacho mtu anacho, si kulingana na kile ambacho mtu hana.”

     Maana: Nia ya mtu katika kutoa ni jambo la muhimu zaidi kuliko kiasi anachotoa.

  •   2 Wakorintho 9:7: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”

     Maana: Mungu hapendi mtu yeyote ahisi analazimishwa kutoa. Anapendezwa na mtu anayetoa kwa sababu anataka kutoa.

Dini zenye pupa zitapatwa na nini hivi karibuni?

 Biblia inasema waziwazi kwamba Mungu hakubali njia zote za ibada na dini zote. (Mathayo 7:21-23) Katika unabii fulani unaostaajabisha, Biblia inafananisha mashirika yote ya dini za uwongo na kahaba kwa sababu yanashirikiana na serikali mbalimbali ili kupata fedha au misaada na kuwadhulumu watu wa mataifa yote. (Ufunuo 17:1-3; 18:3) Unabii huo unaendelea kuonyesha kwamba hivi karibuni Mungu ataangamiza dini ya uwongo.—Ufunuo 17:15-17; 18:7.

 Kwa sasa, Mungu anataka watu wasipotoshwe na mienendo mibaya ya dini ya uwongo au zisifanye watu washindwe kumkaribia. (Mathayo 24:11, 12) Anawasihi watu wenye mioyo minyoofu wajifunze jinsi ya kumtumikia kwa njia anayokubali na watoke katika dini ya uwongo.—2 Wakorintho 6:16, 17.