Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Wenye Furaha na Kuridhika

Jinsi ya Kuwa Wenye Furaha na Kuridhika

Sisi sote​—iwe ni waseja au tumefunga ndoa, vijana au wazee—tunataka kuwa na furaha na kuridhika. Muumba wetu anataka tuhisi hivyo pia, hivyo, ametupatia ushauri bora sana.

Fanya Kazi kwa Bidii

“Afanye kazi kwa bidii, akifanya kazi njema kwa mikono yake, ili awe na kitu cha kumgawia mtu mwenye uhitaji.”​​—WAEFESO 4:28.

Muumba wetu anatutia moyo tuwe na maoni yanayofaa kuhusu kazi. Kwa nini? Mtu anayefanya kazi kwa bidii ana furaha kwa sababu anaweza kujiandalia mahitaji yake na yale ya familia yake. Hata anaweza kumsaidia mtu mwingine mwenye uhitaji. Mwajiri wake atamthamini sana. Kwa hiyo, mfanyakazi mzuri anaweza kudumisha kazi yake. Maandiko yanaonyesha kwamba matokeo ya kufanya kazi kwa bidii ni “zawadi kutoka kwa Mungu.”​—Mhubiri 3:13.

Uwe Mnyoofu

“Tuna hakika kwamba tuna dhamiri nyoofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​​—WAEBRANIA 13:18.

Ikiwa sisi ni wanyoofu, tutajiheshimu, tutakuwa na amani ya akili, na tutalala usingizi mnono. Zaidi ya hilo, wengine watatuamini na kutuheshimu. Watu wasio wanyoofu wanajinyima wenyewe vitu hivyo vizuri. Pia, dhamiri zao zinaweza kuwasumbua, nao wanaishi kwa wasiwasi wakihofu kwamba siku moja watakamatwa kwa sababu ya kutokuwa wanyoofu.

Uwe na Maoni Yanayofaa Kuhusu Pesa

“Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.”​​—WAEBRANIA 13:5.

Tunahitaji pesa ili tununue chakula na mahitaji mengine ya msingi. Hata hivyo, kupenda pesa ni hatari sana. Kunaweza kumfanya mtu atumie wakati wake na nguvu zake zote kujitahidi kupata pesa nyingi zaidi. Kwa sababu anajitahidi sana kupata pesa zaidi, uhusiano wake na mwenzi wake wa ndoa unaweza kuharibika, anaweza kukosa muda wa kuwa pamoja na watoto wake, na hata kudhuru afya yake. (1 Timotheo 6:9, 10) Isitoshe, mtu anayependa pesa anaweza kushawishika kwa urahisi kutokuwa mnyoofu. Mwanamume mmoja mwenye hekima alisema hivi: “Mtu mwaminifu atapata baraka nyingi, lakini anayeharakisha kupata utajiri hatabaki bila hatia.”​—Methali 28:20.

Chagua Kupata Elimu Bora Zaidi

“Ilinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.”​​—METHALI 3:21.

Elimu bora inatusaidia tuwe watu wazima wenye kutegemeka na pia wazazi bora. Lakini elimu ya shuleni pekee haitoshi kutupatia kila kitu tunachohitaji na kuwa na furaha. Ili tufanikiwe kikweli katika nyanja zote za maisha, tunahitaji elimu ambayo Mungu anatupatia. Maandiko yanasema hivi kuhusu mtu anayemsikiliza Mungu: “Kila jambo analofanya litafanikiwa.”​—Zaburi 1:1-3.