Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maneno ya heshima ni kama mchanga uliochanganywa na saruji, ambao unaunganisha ndoa yenu

KWA WENZI WA NDOA

3: Heshima

3: Heshima

MAANA YAKE

Katika ndoa ya wenzi wanaoheshimiana, kila mmoja hujali hisia za mwenzake hata wanapokuwa hawaelewani kuhusu jambo fulani. “Wenzi wa aina hii hawang’ang’anii maoni yao. Badala yake, wao huzungumzia tatizo husika. Kila mmoja anasikiliza kwa makini maoni ya mwenzi wake, na wanafikia uamuzi ambao unawanufaisha wote.”—Ten Lessons to Transform Your Marriage.

KANUNI YA BIBLIA: “Upendo . . . hautafuti faida zake wenyewe.”—1 Wakorintho 13:4, 5.

“Kumheshimu mke wangu humaanisha ninatambua thamani yake na kwamba sitaki kufanya kitu chochote kitakachomdhuru yeye au ndoa yetu.”—Micah.

KWA NINI NI MUHIMU

Ikiwa wenzi wa ndoa hawaheshimiani, mazungumzo yao yatajaa kejeli, dharau, na maneno ya kushushiana heshima. Watafiti wanasema hiyo ni ishara ya kwamba wenzi hao wa ndoa watatalikiana.

“Kuzungumza kumhusu mke wako kwa njia inayomwaibisha kutafanya ahisi hafai, ashindwe kukuamini, na ndoa yenu itaathirika.”—Brian.

MAMBO YA KUFANYA

JICHUNGUZE

Chunguza mazungumzo yenu kwa kipindi cha wiki moja. Kisha jiulize:

  • ‘Nilimkosoa mwenzi wangu mara ngapi, na nilimpongeza mara ngapi?’

  • ‘Nilifanya mambo gani hususa kumwonyesha mwenzi wangu ninamheshimu?’

ZUNGUMZA NA MWENZI WAKO

  • Ni maneno na matendo gani ambayo yatafanya kila mmoja ahisi anaheshimiwa?

  • Ni maneno na matendo gani ambayo hufanya kila mmoja ahisi haheshimiwi?

MAPENDEKEZO

  • Ungependa kuonyeshwa heshima katika njia gani tatu? Ziorodheshe. Mwombe mwenzi wako afanye hivyo pia. Badilishaneni orodha hizo na kila mmoja ajitahidi kuonyesha heshima katika njia zilizotajwa.

  • Orodhesha sifa za mwenzi wako zinazokuvutia. Kisha mwambie unazithamini sifa hizo kwa kadiri gani.

“Kumheshimu mume wangu humaanisha kwamba ninamwonyesha kwa matendo kuwa ninamthamini na ninataka awe na furaha. Si lazima nifanye jambo kubwa; mara nyingi mambo madogo ninayosema au kufanya ndiyo humwonyesha ninamheshimu kutoka moyoni.”—Megan.

Kumbuka, suala si ikiwa wewe unahisi unamheshimu mwenzi wako au la, bali ni ikiwa yeye anahisi anaheshimiwa.

KANUNI YA BIBLIA: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu, upole, na subira.”—Wakolosai 3:12.