Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kuepuka Maneno Yenye Kuumiza

Jinsi ya Kuepuka Maneno Yenye Kuumiza

KIKWAZO

Kila mara mnapobishana, wewe na mwenzi wako mnatupiana maneno yenye kuchambua. Maneno yenye kuumiza yamekuwa ya kawaida katika ndoa yenu hivi kwamba sasa mmezoea kuwasiliana kwa njia hiyo.

Ikiwa ndoa yako iko hivyo, unaweza kuzuia hali hiyo isiendelee. Lakini, kwanza, unahitaji kuchunguza ni nini kinachosababisha tatizo hilo na kwa nini kufanya mabadiliko kutakuwa na manufaa kwenu.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Malezi. Waume na wake wengi walilelewa katika familia ambamo watu walizoea kutumia maneno yenye kuumiza. Huenda mwenzi mmoja au wote wawili wakawa wanatumia maneno ambayo waliwasikia wazazi wao wakitumia.

Uvutano mbaya wa burudani. Waigizaji wa filamu na televisheni hugeuza maneno ya kifidhuli kuwa jambo la kuchekesha, na hivyo kuwafanya watazamaji waone kuwa si vibaya kutumia maneno hayo.

Utamaduni. Jamii fulani hufundisha kwamba “wanaume halisi” huwakandamiza wengine na kwamba wanawake wanahitaji kuwa wakali sana ili wasionwe kuwa dhaifu. Mabishano yanapotokea, huenda wenzi wa ndoa walio na mitazamo kama hiyo wakawaona wenzi wao kuwa maadui badala ya marafiki na huenda wakatumia maneno yenye kuumiza badala ya maneno yenye kuponya.

Hata sababu iwe nini, maneno yenye kuumiza yanaweza kuongoza kwenye talaka na pia yanaweza kusababisha matatizo fulani ya afya. Hata wengine wanasema kwamba maneno yanaweza kuumiza zaidi kuliko kupigwa. Kwa mfano, mwanamke mmoja ambaye mume wake alikuwa na zoea la kumpiga na kumtukana anasema hivi: “Ilikuwa vigumu zaidi kuvumilia matusi kuliko kupigwa. Afadhali angenipiga kuliko kuniambia maneno yenye kuumiza.”

Mnaweza kufanya nini ikiwa uhusiano wenu umeharibika kwa sababu ya kutumia maneno yenye kuumiza?

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Onyesha hisia-mwenzi. Jiweke katika hali ya mwenzi wako, na ujaribu kuelewa jinsi maneno yako yanavyofanya ahisi. Ikiwezekana, fikiria pindi hususa ambayo mwenzi wako alihisi kuwa maneno uliyosema yalimuumiza. Usikazie fikira maneno uliyosema; jambo muhimu ni jinsi mwenzi wako anavyohisi kuhusu yale uliyosema. Je, unaweza kufikiria maneno yenye fadhili ambayo ungetumia badala ya maneno hayo yenye kuumiza? Biblia inasema: “Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.”—Methali 15:1.

Jifunze kutoka kwa wenzi wa ndoa wanaoheshimiana. Ikiwa uliiga mifano mibaya ya watu waliotumia maneno yenye kuumiza, tafuta mifano mizuri ya kuiga. Wasikilize wenzi wa ndoa ambao wanastahili kuigwa kwa sababu ya usemi wao.—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 3:17.

Amsha hisia mlizokuwa nazo. Mara nyingi maneno yenye kuumiza ni tatizo linaloanzia moyoni si kinywani. Kwa hiyo, jitahidi kuwa na hisia na mawazo yanayofaa kumhusu mwenzi wako. Zungumzieni mambo mliyofurahia zamani mkiwa pamoja. Angalieni picha zenu za zamani. Ni nini kilichowafanya mcheke? Ni sifa gani zilizomfanya kila mmoja wenu avutiwe na mwenzake?—Kanuni ya Biblia: Luka 6:45.

Tumia neno “mimi.” Badala ya kumshambulia mwenzi wako kwa maneno, mweleze jinsi mambo mbalimbali yanavyokuathiri. Kwa mfano, ni rahisi kwa mwenzi wako kukujibu kwa maneno mazuri ukimwambia, “Mimi huhisi kuwa nimepuuzwa unapofanya mambo bila kuomba maoni yangu” badala ya kusema, “Hiyo ni kawaida yako—kila wakati unafanya mambo bila kuomba maoni yangu!”—Kanuni ya Biblia: Wakolosai 4:6.

Jua wakati wa kunyamaza. Ikiwa hasira inaanza kupanda na mnashindwa kudhibiti maneno yenu, lingekuwa jambo bora kuahirisha mazungumzo. Kwa kweli, hakuna ubaya wowote kuondoka mabishano yanapokuwa makali na kusubiri hadi mtakapoweza kuzungumza kwa utulivu zaidi.—Kanuni ya Biblia: Methali 17:14.

Mara nyingi maneno yenye kuumiza ni tatizo linaloanzia moyoni si kinywani