Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ufahamu wa Mtu Hakika Hupunguza Hasira Yake”

“Ufahamu wa Mtu Hakika Hupunguza Hasira Yake”

Mwalimu fulani wa mchezo wa vikapu chuoni afutwa kazi kwa sababu ya hasira yake kali.

Mtoto akasirika sana kwa sababu hakupewa alichotaka.

Mama afokeana na mwanaye kwa sababu mwana huyo hajasafisha chumba chake.

SOTE tumewahi kuwaona watu wakikasirika na bila shaka sisi wenyewe tumewahi kukasirika. Huenda tukasema kwamba hasira ni mbaya na hivyo hatupaswi kukasirika, lakini mwingine anapotukosea huenda tukahisi tuna sababu nzuri ya kukasirika. Makala fulani iliyochapishwa na Chama cha Wataalamu wa Saikolojia nchini Marekani inasema kwamba “hasira ni hisia ya kawaida ya wanadamu na inafaa.”

Huenda tukakubaliana na maoni hayo hasa tunapofikiria maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo mtume Mkristo Paulo aliandika. Alikiri kwamba kuna wakati ambapo watu hukasirika aliposema hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Kwa hiyo, je, tunapaswa kuachilia hasira yetu, au tunapaswa kujitahidi kuidhibiti?

JE, INAFAA KUKASIRIKA?

Paulo alipotoa shauri hilo kuhusu hasira, inaelekea alikumbuka maneno haya ya mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Fadhaikeni, lakini msitende dhambi.” (Zaburi 4:4) Hata hivyo, maneno hayo ya Paulo yalimaanisha nini? Aliendelea kusema: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.” (Waefeso 4:31) Kwa kweli, Paulo alikuwa akiwahimiza Wakristo waepuke kuwaka hasira. Inapendeza kwamba, makala ya Chama cha Wataalamu wa Saikolojia nchini Marekani inaendelea kusema hivi: “Utafiti umeonyesha kwamba, mtu akiachilia hasira yake, huenda akatenda kwa hasira zaidi na kuwa mjeuri na hilo halitamsaidia . . . kutatua tatizo lake.”

Hivyo basi, tunawezaje ‘kuondolea mbali’ hasira na hivyo kuepuka madhara yake? Mfalme Sulemani mwenye hekima wa Israeli la kale aliandika hivi: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” (Methali 19:11) “Ufahamu wa mtu” unawezaje kumsaidia anapokasirika?

 JINSI UFAHAMU UNAVYOPUNGUZA HASIRA

Ufahamu ni uwezo wa kuelewa hali kwa kina. Mtu mwenye ufahamu huona mambo kwa undani. Ufahamu unatusaidiaje tunapokosewa au kukasirishwa?

Tunapokosewa, tunaweza kukasirika. Hata hivyo, tukifuata hisia zetu na kufanya fujo tunaweza kujiumiza wenyewe au kuwaumiza wengine. Kama vile tu moto usiodhibitiwa unavyoweza kuichoma nyumba, kuwaka hasira kunaweza kuharibu sifa yetu, kuharibu uhusiano wetu na wengine, na hata kuharibu uhusiano wetu na Mungu. Hivyo tunapohisi hasira ikipanda, tunahitaji kuelewa sababu zinazotufanya tukasirike. Tukizielewa sababu hizo, tutaweza kudhibiti hisia zetu.

Mfalme Daudi aliyekuwa baba ya Sulemani, alikuwa karibu kuangamiza familia nzima ya Nabali, lakini hakutenda hivyo kwa sababu alisaidiwa kuelewa kwa nini hakupaswa kuua. Daudi na watu wake walilinda kondoo wa Nabali katika nyika ya Yudea. Wakati ulipofika wa kuwakata manyoya kondoo, Daudi alimwomba Nabali chakula. Nabali alimjibu hivi: “Je, nichukue mkate wangu na maji yangu na nyama yangu ambayo nimewachinjia wakataji-manyoya wangu na kuwapa watu ambao sijui hata wanatoka wapi?” Ilikuwa dharau kubwa! Daudi aliposikia maneno hayo, yeye na wanaume 400 hivi walifunga safari ya kwenda kuwaangamiza Nabali na familia yake yote.—1 Samweli 25:4-13.

Abigaili, mke wa Nabali alijulishwa kuhusu yaliyotokea na akaenda kukutana na Daudi. Alipokutana na Daudi na watu wake, alianguka miguuni pake na kusema: “Mwache kijakazi wako aseme masikioni mwako, nawe uyasikilize maneno ya kijakazi wako.” Kisha, akamweleza Daudi jinsi Nabali alivyokuwa mpumbavu na akamtahadharisha Daudi kuwa angejuta ikiwa angejilipizia kisasi na kuua.—1 Samweli 25:24-31.

Ushauri wa Abigaili ulimsaidiaje Daudi kupunguza hasira yake? Kwanza, alitambua kwamba Nabali alikuwa mpumbavu, na pia akagundua kwamba angepata hatia ya damu ikiwa angelipiza kisasi. Wewe pia unaweza kukasirishwa na jambo fulani. Unapaswa kufanya nini? Makala fulani iliyotolewa na Kliniki ya Mayo kuhusu kudhibiti hasira ilipendekeza hivi: “Vuta pumzi kwa nguvu na uhesabu 1 hadi 10.” Naam, kwanza tulia na ufikirie chanzo cha tatizo na matokeo ya jambo unalotaka kufanya. Ufahamu utakusaidia kupunguza na hata kumaliza kabisa hasira yako.—1 Samweli 25:32-35.

Kwa njia kama hiyo, wengi leo wamefaulu kudhibiti hasira yao. Sebastian anaeleza jinsi kujifunza Biblia alipokuwa gerezani nchini Poland akiwa na umri wa miaka 23, kulivyomsaidia ajue jinsi ya kudhibiti hasira yake. Anasema, “Kwanza ninafikiria tatizo hilo, kisha ninajitahidi kutumia ushauri wa Biblia. Niligundua kwamba Biblia ni kitabu kinachotoa mwongozo bora zaidi.”

Kutumia ushauri wa Biblia kutakusaidia kudhibiti hasira

Setsuo pia alifuata ushauri huo. Anasema hivi: “Nilizoea kuwafokea wengine waliponiudhi kazini. Kwa kuwa sasa nimejifunza Biblia, badala ya kufoka mimi hujiuliza: ‘Ni nani mwenye makosa? Je, mimi ndiye niliyekosea?’” Kutafakari maswali hayo kulimsaidia apunguze hasira yake, na akaweza kuidhibiti.

Hasira ina nguvu, lakini ushauri wa Neno la Mungu una nguvu zaidi. Ukitumia ushauri wenye hekima wa Biblia na kumwomba Mungu akusaidie, wewe pia unaweza kuruhusu ufahamu upunguze na kudhibiti hasira yako.