Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?

Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?

Kwa Nini Watu Fulani Hutenda kwa Jeuri?

JOSEBA, anayeishi nchini Hispania, aliulizwa kwa nini alijiunga na kikundi cha wanamgambo. “Ukandamizaji na ukosefu wa haki tuliopatwa nao ulikuwa mwingi,” akasema. “Katika jiji kubwa la Bilbao, ambako nilikuwa nikiishi, polisi walikuwa wakija, wanawapiga watu, na kuwakamata.”

Joseba anaendelea kusema: “Asubuhi moja nilikamatwa kwa kueleza waziwazi hisia zangu kuhusu mbinu hizo za polisi. Nilikasirika sana hivi kwamba nilitaka kufanya jambo fulani—ujeuri wa aina fulani—ili kutuliza hali hiyo.”

Ukandamizaji na Kulipiza Kisasi

Bila kutetea jeuri, Biblia inakubali kwamba “uonevu mtupu unaweza kumfanya mtu mwenye hekima atende kiwazimu,” yaani, kwa njia isiyopatana na akili. (Mhubiri 7:7) Watu wengi hukasirika sana wanapotendewa kwa ukosefu wa haki kwa sababu ya jamii, dini, au taifa lao.

Kwa mfano, Hafeni, aliyetajwa katika habari inayotangulia alisema hivi: “Tulinyang’anywa ardhi yetu isivyo haki. Wanyama hupigana ili kutetea maeneo yao, kwa hiyo lilionekana kuwa jambo linalopatana na akili kupigania ardhi na haki zetu.” Mwanamgambo mmoja wa kujitoa mhanga alisema maneno haya yaliyochapishwa baada ya kifo chake: “Msipoacha kuwalipua watu wangu kwa mabomu, kuwaua kwa gesi, kuwafunga, na kuwatesa hatutaacha kupigana.”

Uchochezi wa Kidini

Ingawa kwa kawaida wanamgambo wanachochewa na sababu za kibinafsi, mara nyingi wao hutenda kwa jeuri kwa sababu za kidini. Kiongozi mmoja wa ulimwengu alipokea ujumbe huu kwenye faksi kutoka kwa msemaji wa wanamgambo: “Hatujarukwa na akili wala hatutamani mamlaka. Tunamtumikia Mungu na hilo ndilo linalotufanya tushikilie msimamo wetu kwa bidii.”

Daniel Benjamin na Steven Simon, waliandika hivi katika kitabu chao The Age of Sacred Terror kuhusu uchochezi wa kidini: “Katika ulimwengu unaozidi kuwa wa kidini, waumini wengi wa zile dini kubwa na wa madhehebu mapya wanaamini kwamba jeuri inapaswa kuwa sehemu ya utumishi wao kwa Mungu.” Baada ya kutaja kuhusu “matukio [kadhaa] yenye kustaajabisha ya ugaidi ulimwenguni pote,” mchunguzi mwingine alisema kwamba wote waliotekeleza matendo hayo waliamini kwamba matendo yao yaliruhusiwa, au kuamriwa, na Mungu.”

Lakini wanamgambo wengi wa kidini wana maoni yanayopita kiasi ambayo hayapatani na mafundisho wala na viwango vya msingi vya dini wanazoshirikiana nazo.

Hisia za Jeuri Zimekolea Mioyoni Mwao

Joseba aliyetajwa mapema, alitendewa vibaya sana alipokamatwa. Anasema: “Ukatili huo ulinihakikishia kwamba nilikuwa na haki ya kutenda kwa chuki. Iwapo ningekufa ili kuleta mabadiliko, ingekuwa sawa.”

Mara nyingi mambo yanayofundishwa katika vikundi hivyo huwachochea watu katika vikundi hivyo kujihusisha katika jeuri. “Tulipokuwa kwenye kambi za wakimbizi,” Hafeni anasema, “kulikuwa na mikutano ya wanamgambo iliyotufundisha kwamba kila wakati wazungu walikuwa wakitafuta njia za kuwakandamiza watu weusi.” Kulikuwa na matokeo gani?

Aliendelea kusema hivi: “Chuki yangu kuelekea wazungu iliongezeka. Sikumwamini yeyote kati yao. Mwishowe, singeweza kuvumilia zaidi na nikajiambia kwamba lazima kizazi chetu kichukue hatua.”

Kwa kushangaza, ingawa Joseba na Hafeni walikuwa na msimamo mkali hivyo, wote wawili waliacha kuwa na chuki na wakaanza kuwaamini watu wengine. Ni nini kilichogusa akili na moyo wao? Habari inayofuata itaeleza jinsi hilo litakavyotukia.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Ukatili huo ulinihakikishia kwamba nilikuwa na haki ya kutenda kwa chuki. Iwapo ningekufa ili kuleta mabadiliko, ingekuwa sawa.”—Joseba