Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Taarifa za Habari Zenye Kuogopesha Zinawaathiri Watoto Wako?

Je, Taarifa za Habari Zenye Kuogopesha Zinawaathiri Watoto Wako?

“Binti yangu mwenye umri wa miaka 11 hapendi kutazama habari. Mara nyingi yeye huota ndoto zenye kutisha kuhusu mambo ambayo ametazama. Pindi moja alitazama habari kuhusu mtu aliyemkata kichwa mtu wa familia yake. Usiku huo binti yangu aliota kwamba yeye pia alikuwa akikatwa kichwa.”—Quinn.

“Mpwa wangu wa kike mwenye umri wa miaka sita alitazama habari kuhusu vimbunga katika sehemu nyingine za nchi. Kwa majuma kadhaa baadaye alikuwa na hofu nyingi. Alikuwa akinipigia simu akisema kwamba alikuwa na hakika kuwa kimbunga kilikuwa karibu kupiga sehemu ambayo yeye yuko na kwamba angekufa.”—Paige.

JE, TAARIFA za habari zinamwogopesha mtoto wako? Katika uchunguzi mmoja uliofanywa, karibu asilimia 40 ya wazazi walisema kwamba watoto wao waliogopeshwa na jambo fulani waliloona katika habari na likawafanya wahofu kwamba tukio kama hilo lingewapata wao au wapendwa wao.

Kwa nini? Sababu moja ni kwamba mara nyingi watoto huelewa taarifa za habari kwa njia tofauti na watu wazima. Kwa mfano, huenda watoto wadogo wakaamini kuwa msiba mmoja unaoonyeshwa mara nyingi ni misiba tofauti inayotukia mara nyingi.

Sababu nyingine ni kwamba taarifa za mambo yenye kutisha yanayotokea kila siku zinaweza kumfanya mtoto awe na maoni yasiyofaa kuhusu ulimwengu. Ni kweli kwamba tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Lakini mtoto anapoona taarifa nyingi za habari zenye kutisha anaweza kuwa na woga unaomzuia kufanya mambo kwa njia ya kawaida. “Watoto ambao hutazama televisheni sana wana mwelekeo wa kufikiri kwamba ulimwengu ni hatari kuliko ulivyo kikweli,” inasema Taasisi ya Kaiser Family.

Ikiwa watoto wako wanaathiriwa na taarifa za habari zenye kutisha, unaweza kufanya nini? Yafuatayo ni mapendekezo machache.

Walinde.

Ikitegemea umri, ukomavu, na hisia za watoto wako, fikiria ni mipaka gani unayoweza kuwawekea kuhusiana na kutazama habari. Bila shaka, katika enzi hii ya usambazaji habari, watoto wanajua mengi kuhusu matukio ya ulimwengu. Hata watoto wadogo wanaweza kuona au kusikia mambo mengi kuliko unavyofikiri. Kwa hiyo, uwe macho kuona dalili za woga au wasiwasi ambao huenda watoto wako wakaonyesha.

Waelimishe.

Kadiri watoto wako wanavyokuwa wakubwa, mbona usitazame habari pamoja nao. Katika hali kama hiyo unaweza kutumia taarifa za habari kuwaelimisha. Jaribu kukazia mambo yanayofaa kuhusu taarifa fulani ya habari—kwa mfano, zungumzia kuhusu jitihada za kutoa msaada zinazofanywa ili kuwasaidia watu walioathiriwa na msiba fulani.

Waondolee hofu.

Habari zenye kuogopesha zinapotangazwa, waulize watoto wako maswali ili uone jinsi wanavyohisi kuhusu mambo yaliyotendeka. “Mimi na mke wangu humweleza mwana wetu, Nathaniel, kuhusu mambo ambayo ametazama kwenye habari, kutia na tahadhari ambazo tumechukua ili kuepuka misiba kama hiyo,” anasema baba anayeitwa Michael. “Pindi moja, Nathaniel alipoona picha za habari zinazoonyesha nyumba ikiteketea, aliogopa kwamba huenda nyumba yetu ikachomeka pia. Ili kumwondolea hofu, tulimwonyesha ving’ora vyote vya moto ndani ya nyumba. Anajua mahali vilipo na vina kusudi gani. Hilo lilimsaidia kujihisi akiwa salama.”

Dumisha maoni yenye usawaziko.

Watafiti wamegundua kwamba watu hufikiria kimakosa kwamba iwapo wanaweza kufikiria kuwa jambo fulani litatendeka, basi kuna uwezekano kwamba litatendeka. Kwa mfano, ikiwa umesikia hivi karibuni kwamba kuna mtoto aliyetekwa nyara, kuna uwezekano mkubwa kwamba utafikiria kwamba mtoto wako yuko hatarini kuliko ilivyo kweli. Bila shaka, ni vizuri kuwa macho kuhusiana na hatari zinazoweza kutokea. Hata hivyo, wataalamu wanasema kwamba taarifa za habari zinaweza kutufanya tuogope mambo ambayo huenda hata hayatawahi kutupata.​—Methali 22:3, 13.

Wazazi wanaposhindwa kudumisha maoni yenye usawaziko kuhusu taarifa za habari, huenda wakawa na hofu kupita kiasi. Hofu hiyo inaweza kuwapata watoto wao pia. Kwa mfano, katika mwaka wa 2005 mvulana mwenye umri wa miaka 11 alipotea katika milima ya Utah nchini Marekani. Kwa kuwa alikuwa akiogopa kutekwa nyara, alijificha kwa siku nne hivi kwamba waokoaji uhai hawakumwona. Mwishowe, waokoaji hao walipompata mvulana huyo, alikuwa dhaifu na maji yalikuwa yamekwisha mwilini mwake. Hata ingawa uwezekano wa kutekwa nyara ulikuwa mdogo sana, yaani, ni mtu 1 tu kati ya 350,000 ambaye angeweza kutekwa nyara, woga wa mvulana huyo ulimfanya aone kwamba afadhali afe njaa kuliko kukubali msaada.

“Watoto walio na umri wa miaka 3 hadi 7 wanaogopeshwa zaidi na taarifa za misiba ya asili na aksidenti, na wale walio na umri wa miaka 8 hadi 12 wanaogopeshwa zaidi na habari kuhusu uhalifu na jeuri.”—Taasisi ya Kaiser Family

Tunajifunza nini? Hakikisha kwamba wewe na watoto wako mnadumisha maoni yenye usawaziko kuhusu habari. Ukweli ni kwamba mambo mengi yanaonwa kuwa yanastahili kutangazwa katika habari kwa kuwa hayatukii mara nyingi—si eti kwa sababu ni mambo ya kawaida.

Uhalifu, jeuri, na misiba ya asili ni mambo halisi yanayotokea katika siku zetu. Hata hivyo, kama tulivyoona, jitihada zako za kuwalinda watoto wako, kuwaelimisha, kuwaondolea hofu, na kuwasaidia wawe na maoni yenye usawaziko zitawasaidia kukabiliana na taarifa zenye kuogopesha.