Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushinda Tatizo la Kunenepa Kupita Kiasi Miongoni mwa Vijana

Kushinda Tatizo la Kunenepa Kupita Kiasi Miongoni mwa Vijana

KULINGANA na Wizara ya Afya na Huduma za Jamii nchini Marekani, kati ya mwaka wa 1980 na 2002, idadi ya vijana wanaobalehe walionenepa kupita kiasi iliongezeka mara tatu na idadi ya watoto walionenepa kupita kiasi ikaongezeka zaidi ya maradufu. Matatizo yanayoweza kuwapata watoto kwa sababu ya kunenepa kupita kiasi yanatia ndani kupanda kwa shinikizo la damu, kisukari, magonjwa ya moyo, na aina kadhaa za ugonjwa wa kansa. *

Tatizo la watoto kunenepa kupita kiasi linaweza kusababishwa na mambo kadhaa kama vile, kutofanya mazoezi, matangazo ya biashara yanayowalenga vijana, na kupatikana kwa urahisi na kwa bei ya chini kwa vyakula visivyo na lishe. Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani vinasema: “Tatizo la watoto kunenepa kupita kiasi linasababishwa na tabia ya kula vyakula vyenye kalori nyingi kupita kiasi na kutofanya mazoezi ya kutosha.”

Watoto, vijana, na watu wazima wanapaswa kuchunguza mazoea yao ya kula. Bila kupita kiasi, kufuata hatua fulani rahisi kunaweza kutokeza mabadiliko. Kwa mfano, mfikirie kijana anayeitwa Mark, ambaye aligundua kwamba kubadili mazoea yake ya kula kulimletea faida za afya. Mark anasema hivi: “Wakati mmoja nilikula vyakula visivyo na lishe.” Mwandishi wa Amkeni! alizungumza na Mark ili kujua alifanyaje mabadiliko hayo.

Ulianza lini kula vyakula visivyo na lishe?

Nilipomaliza masomo yangu ya sekondari. Wakati huo, nilianza kula mara nyingi kwenye mikahawa. Kulikuwa na mikahawa miwili karibu na mahali nilipofanya kazi, kwa hiyo nilikula chakula cha mchana katika mojawapo ya mikahawa hiyo karibu kila siku. Niliona kwamba ilikuwa rahisi sana kula chakula kwenye mkahawa kuliko kujitayarishia chakula changu.

Ilikuwaje ulipohama nyumbani?

Mazoea yangu ya kula yalizidi kuharibika. Sikujua kupika, na sikuwa na pesa nyingi, lakini mkahawa nilioupenda ulikuwa karibu sana. Kwa maoni yangu ilikuwa rahisi na nafuu kwangu kula kwenye mkahawa. Zaidi tu ya kula chakula kisicho na lishe, nilikula kupita kiasi. Sikushiba nilipokula kiwango cha kawaida cha chakula kwenye mkahawa. Niliagiza chipsi nyingi zaidi, chupa kubwa zaidi ya soda, na mkate wa nyama wa ziada​—chochote ambacho ningeweza kulipia—​nilinunua kiasi kikubwa zaidi ambacho kingepatikana.

Ni nini kilichokuchochea kubadilika?

Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, nilianza kufikiri kwa uzito kuhusu afya yangu. Nilikuwa mzito kupita kiasi. Nilijihisi mzembe kila wakati, na nilishindwa kujiamini. Nilijua kwamba nilipaswa kufanya mabadiliko.

Ulidhibitije mazoea yako ya kula?

Nilifanya mabadiliko hatua kwa hatua. Kwanza, nilipunguza kiasi cha chakula nilichokula. Nilijiambia hivi, “Huu si mlo wangu wa mwisho, nitakula tena.” Pindi nyingine nilihitaji kuondoka mezani ili nisiendelee kula. Lakini nilipofanya hivyo nilijihisi vizuri, kana kwamba nilikuwa nimeshinda shindano.

Je, ulihitaji kufanya mabadiliko makubwa?

Nilihitaji kuacha kabisa vitu fulani. Kwa mfano, niliacha kunywa soda na nikaanza kunywa maji pekee. Hilo halikuwa rahisi. Nilipenda sana soda, na nilichukia maji. Baada ya kumaliza kunywa glasi ya maji, ningekunywa maji ya matunda, ili nipate ladha ya utamu kinywani. Baada ya muda, nikaanza kupenda maji.

Mbali na kuacha vyakula visivyo na lishe ulihitaji kufanya nini kingine?

Nilianza kula vyakula vyenye lishe. Nilianza kula matunda kama vile matofaa, ndizi, stroberi, blueberry, rasiberi, and matikiti. Pia nilianza kula nyama zisizo na mafuta mengi, kama vile kuku au samaki. Baada ya muda, nikaanza kupenda vyakula hivyo. Kwa sasa ninajitahidi kula mboga zaidi na kupunguza vyakula vingine. Nimegundua kwamba ninapokula vitafunio vyenye lishe kabla ya milo sili sana wakati wa mlo mkuu. Baada ya wakati kupita tamaa yangu ya kula vyakula visivyo na lishe imepungua kabisa.

Je, uliacha kabisa kula kwenye mkahawa?

Hapana, bado mimi huenda wakati fulani kula kwenye mkahawa. Lakini ninapofanya hivyo, mimi hudhibiti kiasi ninachokula. Ikiwa ninapewa chakula kingi kupita kiasi mimi huomba nusu ya chakula hicho kipakiwe ili nile baadaye. Kwa njia hiyo, nakula kiwango kinachofaa badala ya kulazimika kula chakula kingi kupita kiasi kwa sababu ya kuhofia kuacha chakula kwenye sahani.

Umefaidikaje kwa kufanya mabadiliko hayo?

Nimepunguza uzito wangu, na kwa sasa nina nguvu zaidi. Ninajisikia vizuri zaidi. Jambo bora hata zaidi ni kwamba kwa kutunza afya yangu ninajua ninamheshimu Mungu ambaye amenipa zawadi ya uhai. (Zaburi 36:9) Nilikuwa nikifikiri kwamba nitachoshwa kuishi maisha yanayozingatia afya. Lakini kwa sasa kwa sababu nimeanza kula vyakula vyenye lishe, maoni yangu yamebadilika kabisa! *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Wataalamu wanasema kwamba vijana walionenepa kupita kiasi wanakabili uwezekano mkubwa sana wa kuwa wanene kupita kiasi wanapokuwa watu wazima.

^ fu. 20 Gazeti Amkeni! halipendekezi aina fulani hususa ya chakula. Kila mtu anapaswa kuchunguza aina ya chakula kwa uangalifu na kuomba ushauri wa daktari kabla ya kufanya uamuzi wa kibinafsi unaohusu lishe. Epuka mazoea hatari ya kula yanayofuatwa na watu ili kupunguza uzito.