Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Silinda ya udongo ikiwa na jina la Belshaza

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Uvumbuzi wa vitu vya kale unathibitishaje kwamba Belshaza wa Babiloni alikuwa mtu halisi na alikuwa mfalme?

KWA miaka mingi, wachambuzi wa Biblia walidai kwamba Mfalme Belshaza, anayetajwa kwenye kitabu cha Danieli, hakuwa mtu halisi. (Dan. 5:1) Walikuwa na maoni hayo kwa sababu wavumbuzi wa vitu vya kale hawakupata uthibitisho wowote unaoonyesha kwamba aliwahi kuishi. Hata hivyo, mambo yalibadilika mwaka wa 1854. Kwa nini?

Katika mwaka huo, balozi Mwingereza aliyeitwa J. G. Taylor alifanya uchunguzi wa magofu fulani ya jiji la kale la Uru, ambalo kwa sasa liko kusini mwa nchi ya Iraki. Akiwa huko, mvumbuzi huyo alipata silinda kadhaa za udongo zilizokuwa kwenye mnara mkubwa. Silinda hizo zenye urefu wa sentimita 10, zilikuwa na maandishi yaliyochongwa ya kikabari. Maandishi yaliyo kwenye silinda moja yanatia ndani sala ya kumtakia maisha marefu Mfalme Nabonido wa Babiloni na Belshaza, mwana wake mkubwa. Hata wachambuzi walilazimika kukubali jambo hili: Uvumbuzi huu unathibitisha kwamba Belshaza alikuwa mtu halisi.

Hata hivyo, Biblia haitaji tu kwamba Belshaza alikuwa mtu halisi bali pia alikuwa mfalme. Lakini bado wachambuzi hawakuamini jambo hilo. Kwa mfano, William Talbot, mwanasayansi Mwingereza wa karne ya 19 aliandika kwamba baadhi ya watu wanasema kwamba “Bel-sar-ussur [Belshaza] alitawala kipindi kimoja na Nabonido baba yake. Lakini hakuna jambo lolote linalothibitisha hilo.”

Hata hivyo, utata huo ulisuluhishwa wakati maandishi yaliyokuwa kwenye silinda nyingine za udongo yalipofunua kwamba Mfalme Nabonido, baba ya Belshaza, hakuwepo Babiloni kwa vipindi kadhaa vya miaka. Ni nini kilichotukia wakati ambao hakuwepo? Kitabu Encyclopaedia Britannica kinasema hivi: “Nabonido alipoenda uhamishoni alimkabidhi Belshaza kiti chake cha ufalme na sehemu kubwa ya jeshi lake.” Hivyo Belshaza alitumikia akiwa mtawala wa Babiloni katika kipindi hicho. Ndiyo sababu mvumbuzi wa vitu vya kale na msomi wa lugha Alan Millard alisema kwamba lilikuwa jambo sahihi kwa “Kitabu cha Danieli kumwita Belshaza ‘mfalme.’”

Bila shaka, uthibitisho mkuu kwa watumishi wa Mungu kwamba kitabu cha Danieli kinatumainika na kimeongozwa na roho ya Mungu unapatikana katika Biblia yenyewe.—2 Tim. 3:16.