Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi

Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi

Ongeza Shangwe na Heshima ya Siku Yako ya Arusi

“SIKU yangu ya arusi ilikuwa mojawapo ya siku muhimu zaidi na yenye shangwe maishani mwangu,” akasema Gordon, ambaye amekuwa katika ndoa kwa karibu miaka 60. Ni nini kinachofanya siku ya arusi iwe muhimu kwa Wakristo wa kweli? Hiyo ni siku ambayo wanafanya nadhiri takatifu kwa wale ambao wanawapenda sana, yaani, mwenzi wao na Yehova Mungu. (Mathayo 22:37; Waefeso 5:22-29) Naam, watu wanaopanga kufunga ndoa wangependa kufurahia siku yao ya arusi, lakini pia wanataka kumheshimu Mwanzilishi wa ndoa.—Mwanzo 2:18-24; Mathayo 19:5, 6.

Bwana-arusi anaweza kuongezaje heshima ya pindi hiyo yenye furaha? Bibi-arusi anaweza kuonyeshaje heshima kwa mume wake na kwa Yehova? Wengine wanaohudhuria wanaweza kuongezaje shangwe ya siku ya arusi? Kuchunguza kanuni kadhaa za Biblia kutatusaidia kujibu maswali hayo, na kufuata kanuni hizo kutapunguza matatizo ambayo yanaweza kuvuruga pindi hiyo ya pekee.

Ni Nani Mwenye Daraka?

Katika nchi nyingi huenda mhudumu aliye Shahidi wa Yehova akafunganisha ndoa kisheria. Hata katika nchi ambako ni lazima ndoa ifunganishwe kisheria na ofisa wa serikali, huenda wenzi fulani wakataka hotuba inayotegemea Biblia itolewe kwa ajili yao. Kwa kawaida, hotuba hiyo humhimiza bwana-arusi afikirie wajibu aliopewa na Mungu akiwa kichwa cha familia. (1 Wakorintho 11:3) Kwa hiyo, bwana-arusi ndiye aliye na daraka kuu kuhusiana na mambo yanayotukia katika arusi. Bila shaka, kwa kawaida mipango ya arusi na tafrija ambayo huenda ikafuata hufanywa mapema. Kwa nini huenda ikawa vigumu kufanya mipango hiyo?

Sababu moja ni kwamba watu wa ukoo wanaweza kujaribu kuongoza mipango ya arusi. Rodolfo, ambaye amefunganisha ndoa nyingi, anasema: “Nyakati nyingine, bwana-arusi hubanwa sana na watu wa ukoo, hasa ikiwa wanasaidia kulipia gharama za karamu ya arusi. Huenda wakawa na kauli zenye nguvu kuhusu mambo yatakayofanywa katika arusi na kwenye karamu ya arusi. Hilo linaweza kumnyang’anya bwana-arusi daraka lake la Kimaandiko la kusimamia tukio hilo.”

Max, ambaye amekuwa akifunganisha ndoa kwa miaka zaidi ya 35, anasema hivi: “Nimeona kuna mwelekeo wa bibi-arusi kuongoza katika kuamua mambo yatakayotukia katika arusi na kwenye karamu ya arusi, huku bwana-arusi akinyimwa nafasi ya kutoa maoni yake.” David, ambaye pia amefunganisha ndoa nyingi anaeleza hivi: “Huenda mabwana-arusi hawajazoea kuongoza na kwa kawaida hawajihusishi sana katika matayarisho ya arusi.” Bwana-arusi anaweza kutimizaje ifaavyo daraka lake?

Mawasiliano Huongeza Shangwe

Ili bwana-arusi afaulu kutimiza kwa mafanikio daraka lake kuhusiana na matayarisho ya arusi, anapaswa kuwasiliana vizuri. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) Hata hivyo, ili mipango isivunjike, bwana-arusi anaweza kuzungumzia matayarisho ya arusi pamoja na bibi-arusi, watu wa familia, na wengine ambao wanaweza kutoa mashauri mazuri yanayotegemea Biblia.

Naam, ni muhimu wale wanaotarajia kufunga ndoa wazungumze kwanza pamoja kuhusu mipango na mambo yanayoweza kufanywa. Kwa nini? Kwa mfano, ona alichosema Ivan na mke wake, Delwyn, wanaotoka katika malezi tofauti lakini ambao wamefurahia maisha ya ndoa kwa miaka mingi. Akikumbuka mipango ya arusi yao, Ivan anasema hivi: “Nilikuwa na mawazo hususa kuhusu yale niliyotaka yafanywe katika arusi yangu, kutia ndani karamu pamoja na marafiki wangu wote, keki ya arusi, na bibi-arusi aliyevalia nguo nyeupe. Kwa upande mwingine, Delwyn, alitaka tuwe na arusi ndogo, na isiyo na mambo mengi wala keki ya arusi. Hata alifikiria kuvaa nguo ya kawaida badala ya nguo ya arusi.”

Wenzi hao walitatuaje tofauti hizo? Waliwasiliana kwa fadhili na unyoofu. (Methali 12:18) Ivan anaongeza hivi: “Tulijifunza makala zinazotegemea Biblia kuhusu arusi, kama zile zilizochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi toleo la Septemba 15, 1984, au Kiingereza, Aprili 15, 1984, au Kifaransa, Julai 15, 1984. * Makala hizo zilitusaidia kuwa na maoni ya kiroho kuhusu arusi. Kwa sababu ya malezi yetu tofauti, tulihitaji kukubaliana katika mambo kadhaa ya kibinafsi. Sote tulibadili mtazamo wetu.”

Aret na Penny walifanya vivyo hivyo. Aret anasema hivi kuhusu siku yao ya arusi: “Mimi na Penny tulizungumzia mapendezi yetu kuhusiana na arusi, na tuliweza kukubaliana. Tulisali ili Yehova abariki siku hiyo. Pia, nilitafuta mashauri ya wazazi wetu na baadhi ya wenzi walio wakomavu kutanikoni. Mapendekezo yao yalitusaidia sana. Kwa sababu hiyo, arusi yetu ilikuwa nzuri sana.”

Kudumisha Heshima Katika Mavazi na Mapambo

Ni jambo linaloeleweka kwa bibi na bwana-arusi kutaka kuvalia kwa njia iliyo nzuri siku yao ya arusi. (Zaburi 45:8-15) Huenda wakatumia wakati, jitihada, na pesa kununua mavazi yanayofaa. Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kuwasaidia kuchagua mavazi yenye heshima na yanayovutia?

Fikiria mavazi ambayo bibi-arusi anavaa siku hiyo. Mashauri ya Biblia yanafaa kila mahali, licha ya kwamba kila mtu ana mapendezi yake na kila nchi ina mitindo yake ya mavazi. Wanawake wanapaswa ‘kujipamba kwa mavazi yenye mpangilio mzuri, pamoja na kiasi na utimamu wa akili.’ Shauri hilo linawafaa wanawake Wakristo nyakati zote, na bila shaka linahusu pia siku ya arusi. Ukweli ni kwamba si lazima kuwa na “mavazi yaliyo ghali sana” ili arusi iwe yenye shangwe. (1 Timotheo 2:9; 1 Petro 3:3, 4) Inaridhisha kama nini kufuata shauri hilo!

David, aliyetajwa mwanzoni, anaeleza hivi: “Wenzi wengi hujitahidi kufuata kanuni za Biblia, na wanastahili kupongezwa. Hata hivyo, nyakati nyingine, mabibi-arusi na waandamani wao huvaa nguo zisizo na kiasi ambazo hazifichi sehemu kubwa ya kifua au nguo nyepesi zinazoonyesha mwili.” Mzee fulani ambaye ni Mkristo mkomavu anapozungumza na bibi na bwana-arusi kabla ya arusi, huwasaidia kuwa na mtazamo wa kiroho. Jinsi gani? Kwa kuwauliza ikiwa nguo watakazovaa zitakuwa zenye kiasi hivi kwamba zinaweza kuvaliwa kwenye mikutano ya Kikristo. Ni kweli kwamba mtindo wa nguo za arusi unaweza kuwa tofauti na ule wa nguo zinazovaliwa kwenye mikutano ya kawaida na nguo hizo zinaweza kupatana na desturi za mahali, lakini zinapaswa kuwa zenye kiasi kulingana na viwango vya Kikristo vyenye heshima. Hata ikiwa watu fulani ulimwenguni wanaona viwango vya maadili vya Biblia kuwa vyenye kubana mno, Wakristo wa kweli huwa tayari kupinga jitihada za ulimwengu za kuwafinyanga wafanane nao.—Waroma 12:2; 1 Petro 4:4.

Penny anasema: “Badala ya kuona mavazi au karamu ya arusi kuwa ndiyo mambo muhimu zaidi, mimi na Aret tulikazia fikira sehemu ya kiroho ya tukio hilo. Hiyo ndiyo iliyokuwa sehemu muhimu zaidi ya siku hiyo. Mambo ya pekee ninayokumbuka si, nguo nilizovaa au chakula nilichokula, bali ni watu nilioshirikiana nao siku hiyo na furaha niliyopata kwa sababu ya kuolewa na mwanamume ninayempenda.” Ni vizuri wenzi Wakristo wakumbuke mambo hayo wanapopanga arusi yao.

Jumba la Ufalme—Mahali Panapoheshimiwa

Inapowezekana, wenzi wengi Wakristo hupendelea arusi yao ifanyiwe katika Jumba la Ufalme. Kwa nini wao hupendelea Jumba la Ufalme? Wenzi fulani walieleza sababu yao: “Tulitambua kwamba ndoa ni mpango mtakatifu wa Yehova. Kufunga ndoa katika Jumba la Ufalme, mahali petu pa ibada, kulikazia akilini mwetu tangu mwanzo kwamba Yehova anapaswa kuwa sehemu ya ndoa yetu. Faida nyingine ya kufanyia arusi katika Jumba la Ufalme badala ya mahali pengine ni kwamba watu wetu wa ukoo wasio waamini ambao walihudhuria waliona jinsi tunavyothamini sana ibada ya Yehova.”

Wazee wa kutaniko wanaohusika wakikubali Jumba la Ufalme litumiwe kwa ajili ya arusi, wenzi hao wanapaswa kuwajulisha mapema kuhusu matayarisho yatakayofanywa. Njia moja ambayo bibi na bwana-arusi wanaweza kuonyesha kwamba wanawaheshimu wale walioalikwa kwenye arusi ni kuazimia kabisa kufika kwa wakati. Na bila shaka, wanapaswa kuhakikisha kwamba mambo yote yanafanywa kwa njia ya heshima. * (1 Wakorintho 14:40) Hivyo, wataepuka vituko vinavyofanywa katika arusi nyingi za kilimwengu.—1 Yohana 2:15, 16.

Pia, wale wanaohudhuria arusi wanaweza kuonyesha kwamba wana maoni ya Yehova kuhusu ndoa. Kwa mfano, hawapaswi kutarajia arusi hiyo iwe bora kuliko arusi nyingine za Kikristo, kana kwamba kuna mashindano ya arusi iliyokuwa kubwa. Wakristo wakomavu wanatambua pia kwamba kuwa katika Jumba la Ufalme kwa ajili ya hotuba inayotegemea Biblia ni jambo muhimu na lenye faida zaidi kuliko kuhudhuria karamu ya arusi au tafrija ambayo huenda ikafuata. Ikiwa wakati au hali zinamruhusu Mkristo kuhudhuria tukio moja tu kati ya matukio hayo mawili, bila shaka itafaa kuwa katika Jumba la Ufalme. Mzee anayeitwa William anasema hivi: “Ikiwa wageni wanakosa kwenda katika Jumba la Ufalme bila sababu lakini wanaenda kwenye karamu ya arusi baadaye, hilo linaonyesha kwamba hawathamini utakatifu wa tukio hilo. Hata ikiwa hatukualikwa kwenye karamu, tunaweza kuonyesha kwamba tunawaunga mkono bibi na bwana-arusi na kutoa ushahidi mzuri kwa watu wa ukoo wasio waamini kwa kuhudhuria arusi katika Jumba la Ufalme.”

Shangwe Inayodumu Hata Baada ya Siku ya Arusi

Wafanya-biashara hujipatia faida kubwa kutokana na sherehe za arusi. Ripoti moja ya hivi karibuni inasema kwamba arusi ya kawaida nchini Marekani “hugharimu dola 22,000 za Marekani, au nusu ya mshahara wa wastani wa [mwaka nzima] katika familia ya Kimarekani.” Wenzi wengi wapya na familia zao hushawishiwa na matangazo ya biashara na hivyo kujiingiza katika deni kubwa kwa ajili ya siku hiyo moja, deni ambalo wanalipa kwa miaka mingi. Je, hiyo ni njia ya busara ya kuanzisha ndoa? Huenda wale wasiojua au wasiojali kanuni za Biblia wakaamua kutumia pesa nyingi hivyo, lakini Wakristo wa kweli wako tofauti kama nini!

Wenzi wengi Wakristo wamefanya arusi ndogo zenye usawaziko na gharama ndogo huku wakikazia sehemu ya kiroho ya tukio hilo. Hivyo, wameweza kutumia wakati na mali zao kulingana na wakfu wao kwa Mungu. (Mathayo 6:33) Fikiria mfano wa Lloyd na Alexandra, ambao wamekuwa katika huduma ya wakati wote kwa miaka 17 tangu wafunge ndoa. Lloyd anasema hivi: “Huenda watu fulani waliona arusi yetu kuwa tukio ndogo, lakini mimi na Alexandra tuliifurahia sana. Tulihisi kwamba arusi yetu haipaswi kutulemea kifedha, bali inapaswa kuwa siku ya kusherehekea mpango wa Yehova wa kuwaletea watu wawili furaha kubwa.”

Alexandra anaongezea hivi: “Kabla ya kufunga ndoa nilikuwa painia, na sikutaka kuacha pendeleo hilo ili nifanye arusi kubwa. Arusi yetu ilikuwa ya pekee sana. Hata hivyo, ilikuwa siku ya kwanza tu ya sisi kuishi pamoja. Tulifuata mashauri ya kuepuka kukazia sana sherehe ya kufunga ndoa na tumetafuta mwongozo wa Yehova katika maisha yetu ya ndoa. Bila shaka, hilo limetuletea baraka za Yehova.” *

Naam, siku yenu ya arusi ni pindi ya pekee. Mitazamo na matendo yanayofanywa katika siku ya arusi yanaweza kuwa na uvutano katika maisha yenu ya ndoa miaka ijayo. Kwa hiyo, mtegemee Yehova ili akuongoze. (Methali 3:5, 6) Kazia akilini umuhimu wa kiroho wa tukio hilo. Mtegemezane katika kutimiza madaraka yenu mliyopewa na Mungu. Mkifanya hivyo, mtaiwekea ndoa yenu msingi imara, na mkiwa na baraka za Yehova, mtakuwa na shangwe itakayodumu kwa muda mrefu hata baada ya siku ya arusi.—Methali 18:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Habari zaidi zinapatikana katika gazeti la Amkeni! la Februari 8, 2002, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 20 Ikiwa wenzi wa ndoa wanapanga mtu fulani awapige picha au kurekodi tukio hilo katika Jumba la Ufalme, wanapaswa kuhakikisha mapema kwamba hakuna jambo lolote ambalo litafanya arusi yao isiheshimiwe.

^ fu. 25 Ona ukurasa wa 26 wa kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Wenzi wanapaswa kuwasiliana waziwazi lakini kwa heshima wanapopanga arusi yao

[Picha katika ukurasa wa 31]

Kazia akilini umuhimu wa kiroho wa tukio hilo