Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutenga na Ushirika Ni Mpango Wenye Upendo

Kutenga na Ushirika Ni Mpango Wenye Upendo

“NILIPOSIKIA tangazo kwamba mwanangu ametengwa na ushirika, nilihisi ni kana kwamba huo ndio mwisho wa mambo yote,” anakumbuka Julian. “Alikuwa mwanangu wa kwanza, na tulikuwa marafiki wa karibu sana; tulifanya mambo mengi pamoja. Sikuzote aliweka mfano mzuri, kisha ghafla akaanza kutenda kwa njia isiyokubalika. Mke wangu alilia mara nyingi, na sikujua jinsi ya kumfariji. Mara zote tulijiuliza ikiwa tulishindwa kuwa wazazi wazuri.”

Tunawezaje kusema kwamba kumtenga na ushirika Mkristo ni mpango wenye upendo, ilhali unasababisha maumivu makali? Kuna sababu gani za Kimaandiko za kuchukua hatua hiyo kali? Na kwa nini mtu anatengwa na ushirika?

SABABU MBILI ZINAZOFANYA MTU ATENGWE NA USHIRIKA

Kuna mambo mawili ambayo ni lazima yatukie pamoja na hivyo kumfanya Shahidi wa Yehova atengwe na ushirika. Kwanza, Shahidi aliyebatizwa ametenda dhambi nzito. Pili, hatubu dhambi yake.

Ingawa Yehova hatazamii tuwe wakamilifu, ana viwango vya utakatifu ambavyo anatazamia watumishi wake watimize. Kwa mfano, Yehova anatuhimiza tuepuke dhambi nzito kama vile upotovu wa maadili katika ngono, ibada ya sanamu, wizi, unyang’anyi, uuaji, na kuwasiliana na pepo.—1 Kor. 6:9, 10; Ufu. 21:8.

Je, hukubali kwamba viwango safi vya Yehova ni vyenye usawaziko na vimekusudiwa kutulinda? Ni nani asingependa kuishi miongoni mwa watu wenye amani na maadili mazuri ambao unaweza kuwatumaini? Tunaona hali hiyo miongoni mwa ndugu na dada zetu wa kiroho. Jambo hilo linawezekana kwa kuwa tulijiweka wakfu kwa Mungu ili tuishi kupatana na maagizo yaliyo kwenye Neno lake.

Hata hivyo, namna gani ikiwa Mkristo aliyebatizwa ametenda dhambi nzito kwa sababu ya udhaifu wa kibinadamu? Zamani, watumishi waaminifu wa Yehova walifanya makosa kama hayo, lakini Mungu hakuwakataa kabisa. Mfano mmoja ni Mfalme Daudi. Daudi alifanya uzinzi na kuua; hata hivyo nabii Nathani alimwambia hivi: “Yehova . . . ameacha dhambi yako ipite.”—2 Sam. 12:13.

Mungu alimsamehe Daudi kwa sababu alitubu kikweli. (Zab. 32:1-5) Vivyo hivyo, mtumishi wa Yehova leo atatengwa na ushirika ikiwa tu hatubu au anaendelea kufanya mambo mabaya. (Mdo. 3:19; 26:20) Ikiwa wazee wanaotumikia wakiwa halmashauri ya hukumu hawajaona toba ya kweli, wanapaswa kumtenga na ushirika mtu huyo.

Mwanzoni, huenda tukahisi kwamba uamuzi wa kumtenga na ushirika mkosaji ni mkali sana au si wenye fadhili, hasa kama tuna uhusiano wa karibu na mtu huyo. Hata hivyo, Neno la Yehova linatupatia sababu nzuri zinazofanya tuamini kwamba uamuzi huo ni wenye upendo.

MANUFAA YA KUTENGA NA USHIRIKA

Yesu alisema kwamba “hekima huonyeshwa kuwa yenye uadilifu kwa matendo yake.” (Mt. 11:19) Uamuzi wenye hekima wa kumtenga na ushirika mkosaji asiyetubu unaleta matokeo au matendo ya uadilifu. Fikiria mambo haya matatu:

Kumtenga na ushirika mkosaji hulitukuza jina la Yehova. Kwa kuwa tunaitwa kwa jina la Yehova, kwa hakika tabia zetu zinaweza kuliletea jina lake sifa nzuri au mbaya. (Isa. 43:10) Kama vile tu matendo ya mtoto yanavyoweza kuwafanya wazazi wapate sifa nzuri au mbaya, vivyo hivyo maoni ya watu kumhusu Yehova kwa kadiri fulani yatategemea mfano mzuri au mbaya wa watu wanaoitwa kwa jina lake. Jina zuri la Mungu linatukuzwa ikiwa watu wanaoitwa kwa jina hilo wanatimiza viwango vya maadili vya Yehova. Kwa kiasi fulani hali ilikuwa hivyo katika siku za Ezekieli, wakati watu wa mataifa walipolihusianisha sana jina la Yehova na Wayahudi.—Eze. 36:19-23.

Tungekuwa tukililetea sifa mbaya jina takatifu la Mungu ikiwa tuna maadili mapotovu. Mtume Petro aliwashauri hivi Wakristo: “Kama watoto watiifu, acheni kufanyizwa kulingana na tamaa mlizokuwa nazo hapo zamani katika hali yenu ya kutojua, bali, kwa kupatana na Mtakatifu aliyewaita, ninyi wenyewe pia iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote, kwa sababu imeandikwa: ‘Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.’” (1 Pet. 1:14-16) Matendo safi na matakatifu hulitukuza jina la Mungu.

Hata hivyo, ikiwa Shahidi wa Yehova anazoea kufanya mambo mabaya, inaelekea kwamba rafiki zake na watu wengine wanaomfahamu watajua jambo hilo. Mpango wa kutenga na ushirika unaonyesha kwamba Yehova ana watu safi ambao wanakubali kufuata maagizo yake ya Kimaandiko ili kuendeleza utakatifu huo. Siku moja, mtu fulani alihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme nchini Uswisi na kusema kwamba alitaka kuwa mshiriki wa kutaniko. Dada yake alikuwa ametegwa na ushirika kwa sababu ya upotovu wa maadili. Alisema kwamba alitaka kujiunga na dini ambayo “haivumilii mwenendo mbaya.”

Kumtenga na ushirika mkosaji hulilinda kutaniko safi la Kikristo. Mtume Paulo aliwaonya Wakorintho kuhusiana na hatari ya kuendelea kushirikiana na watu wanaotenda dhambi kimakusudi. Alilinganisha ushawishi mbaya wa watu hao na chachu ambayo husababisha donge lote la unga kuumuka. “Chachu kidogo huchachisha donge lote,” akasema. Kisha akawashauri hivi: “Ondoeni yule mtu mwovu kati yenu.”—1 Kor. 5:6, 11-13.

Inaonekana kwamba “mtu mwovu” anayetajwa na Paulo alikuwa na mazoea mapotovu kimaadili. Hata baadhi ya washiriki wa kutaniko walianza kutetea matendo yake. (1 Kor. 5:1, 2) Ikiwa dhambi hiyo nzito ingeachiliwa, huenda Wakristo wengine wageshawishika kufuata mazoea hayo mapotovu waliyoona katika jiji la Korintho. Watu wanaotenda dhambi kimakusudi wasipochukuliwa hatua, wengine wanaweza kuchochewa kupuuza viwango vya Mungu. (Mhu. 8:11) Isitoshe, watenda dhambi wasiotubu wanafananishwa na “miamba iliyofichwa chini ya maji,” na hivyo wanaweza kuvunja imani ya wengine kutanikoni.—Yuda 4, 12.

Kumtenga na ushirika mkosaji kunaweza kumfanya arudiwe na fahamu. Wakati fulani Yesu aliongea kuhusu kijana mmoja ambaye aliondoka nyumbani kwa baba yake, na akaenda kuutumia urithi wake katika maisha mapotovu. Hali ngumu aliyopitia mwana huyo mpotevu ilimfundisha kwamba maisha yalikuwa magumu sana mbali na nyumbani kwa baba yake. Hatimaye mwana huyo alirudiwa na fahamu, alitubu, na akachukua hatua ya kurudi kwa familia yake. (Luka 15:11-24) Tunaelewa hisia za Yehova kutokana na jinsi Yesu alivyomfafanua yule baba mwenye upendo ambaye alishangilia kuona mwanaye amebadili mtazamo wake. Yehova anatuhakikishia hivi: “Ninapendezwa, si na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.”—Eze. 33:11.

Vivyo hivyo, wale ambao wametengwa na ushirika na sasa si washiriki wa kutaniko la Kikristo (ambalo ndilo familia yao ya kiroho), huenda wakatambua jambo wanalokosa maishani. Matokeo mabaya ya dhambi walizotenda, pamoja na kumbukumbu za shangwe waliyopata walipokuwa na uhusiano mzuri na Yehova na watu wake, zinaweza kuwafanya warudiwe na fahamu.

Upendo na msimamo thabiti unahitajika ili kupata matokeo mazuri. “Mwadilifu akinipiga, zingekuwa fadhili zenye upendo,” akasema mtunga-zaburi Daudi, “naye akinikaripia, hiyo ingekuwa mafuta juu ya kichwa.” (Zab. 141:5) Kwa mfano: Wazia mtu fulani anakula chakula na mara kipande cha nyama kinakwama kooni mwake. Anashindwa kupumua vizuri, na anaishiwa nguvu. Pia hawezi hata kuongea. Atakufa ikiwa mtu fulani hatamsaidia haraka. Hivyo, rafiki yake anampiga mgongoni. Huenda akaumia kwa sababu ya kupigwa, lakini kufanya hivyo kumeokoa uhai wake. Vivyo hivyo, Daudi alitambua kwamba ili anufaike, mtu fulani mwadilifu alihitaji kumrekebisha vikali.

Katika visa vingi, kutenga na ushirika humsaidia mkosaji. Baada ya miaka kumi, mwana wa Julian, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alisafisha maisha yake, alirudi kutanikoni, na sasa ni mzee wa kutaniko. “Nilipotengwa na ushirika nililazimika kukabiliana na matokeo ya matendo yangu,” anakiri. “Nilihitaji nidhamu kama hiyo.”—Ebr. 12:7-11.

JINSI YA KUSHUGHULIKA NA WATU WALIOTENGWA NA USHIRIKA

Ni kweli kwamba kutengwa na ushirika ni janga la kiroho, hata hivyo si lazima janga hilo liwe mwisho wa mambo yote. Sote tuna wajibu wa kuhakikisha kwamba mpango wa kutenga na ushirika unatimiza kusudi lake.

Jitihada nyingi hufanywa ili kuwasaidia waliotubu wamrudie Yehova

Wazee ambao wana wajibu mzito wa kushiriki katika kufanya uamuzi wa kumtenga mtu na ushirika hujitahidi sana kuiga upendo wa Yehova. Wanapomweleza mtu huyo uamuzi wao, wanamfafanulia kwa upole na waziwazi hatua anazopaswa kuchukua ili arudishwe tena kutanikoni. Ili kuwakumbusha watu waliotengwa na ushirika jinsi wanavyoweza kumrudia Yehova, huenda kila baada ya muda fulani wazee wakawatembelea wale ambao wameonyesha kwa kiwango fulani kwamba wamebadili njia zao. *

Washiriki wa familia wanaweza kuonyesha kwamba wanalipenda kutaniko na mkosaji kwa kuheshimu uamuzi wa kutenga na ushirika. “Bado alikuwa mtoto wangu,” anaeleza Julian, “lakini matendo yake yalikuwa kama ukuta uliotutenganisha.”

Washiriki wote wa kutaniko wanaweza kuonyesha upendo kwa kuepuka kuwasiliana na kuzungumza na mtu aliyetengwa na ushirika. (1 Kor. 5:11; 2 Yoh. 10, 11) Hivyo, wanaunga mkono nidhamu iliyotolewa na Yehova kupitia wazee. Isitoshe, inafaa waonyeshe kwamba wanawapenda na kuwategemeza washiriki wa familia ya yule aliyetengwa, ambao wanaumizwa sana na jambo hilo, ili wasihisi kwamba wao pia wametengwa na waamini wenzao.—Rom. 12:13, 15.

“Tunauhitaji mpango wa kutenga na ushirika, kwani unatusaidia tuishi kupatana na mapenzi ya Yehova,” anasema Julian. “Licha ya maumivu, mwishowe matokeo huwa mazuri. Ikiwa ningevumilia matendo mabaya ya mwanangu, hangebadilika kamwe.”

^ fu. 24 Tazama Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 1991, ukurusa wa 21-23.