Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtegemee Yehova Sikuzote!

Mtegemee Yehova Sikuzote!

“Mtegemeeni nyakati zote.”—ZAB. 62:8.

1-3. Kwa nini Paulo alikuwa na uhakika kwamba anaweza kumtegemea Yehova? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

ILIKUWA hatari sana kuwa Mkristo huko Roma katika karne ya kwanza. Waroma waliwalaumu Wakristo kwa kuwasha moto ulioharibu sehemu kubwa ya jiji la Roma katika mwaka wa 64 W.K., na kuwashutumu kwamba waliwachukia watu. Hivyo, wafuasi wa Kristo walichukiwa sana. Ikiwa ungekuwa Mkristo wakati huo, huenda kila siku ungekabili hatari ya kukamatwa na kuteswa. Labda baadhi ya ndugu na dada zako wangekuwa wameraruliwa na wanyama, au wametundikwa mtini na kuchomwa wakiwa hai ili kuwa mwangaza wakati wa usiku.

2 Inawezekana kwamba mtume Paulo alifungwa huko Roma kwa mara ya pili kulipokuwa na hali hizo ngumu. Je, Wakristo wengine wangekuja kumsaidia? Huenda mwanzoni Paulo alihangaishwa na jambo hilo, kwani alimwandikia hivi Timotheo: “Katika kujitetea kwangu mara ya kwanza hakuna yeyote aliyekuja upande wangu, bali wote waliniacha—hilo lisihesabiwe kwao.” Hata hivyo, Paulo alitambua kwamba hakuwa peke yake. Aliandika hivi: “Lakini Bwana alisimama karibu nami na kutia nguvu ndani yangu.” Naam, Bwana Yesu alimpa Paulo nguvu alizohitaji. Msaada huo ulikuwa na matokeo gani kwa Paulo? Alisema hivi: “Nilikombolewa kutoka katika kinywa cha simba.”—2 Tim. 4:16, 17. *

3 Paulo alikumbuka jinsi Yehova alivyomsaidia awali, na hilo lilimwimarisha, na kumsaidia awe na imani kwamba Yehova atamtegemeza ili avumilie majaribu aliyokuwa akikabili, na hali ngumu yoyote ambayo huenda ingejitokeza baadaye. Kwa kweli, hiyo ndiyo sababu alisema hivi: “Bwana atanikomboa kutoka katika kila tendo la uovu.” (2 Tim. 4:18) Naam, Paulo alijifunza kwamba hata kama wanadamu hawangemsaidia, kwa hakika Yehova na Yesu wangemsaidia!

NAFASI ZA ‘KUMTEGEMEA YEHOVA’

4, 5. (a) Ni nani anayeweza kukupa msaada wowote unaohitaji? (b) Unaweza kuimarishaje uhusiano wako na Yehova?

4 Je, umewahi kujihisi upweke ulipokabili hali fulani ngumu? Huenda hali hizo zilisababishwa na kukosa ajira, mikazo shuleni, matatizo ya afya, au hali nyingine ngumu. Labda uliwaomba watu fulani wakusaidie, lakini ukavunjika moyo sana waliposhindwa kukupa msaada uliohitaji. Ni wazi kwamba matatizo fulani hayawezi kusuluhishwa na mwanadamu. Utafanya nini ukikabili hali kama hizo? Biblia inatushauri hivi: “Mtegemee Yehova.” (Met. 3:5, 6) Je, kuna manufaa yoyote ya kufanya hivyo? Bila shaka! Kwa hakika Yehova anaweza kukusaidia, kama vile inavyoonyeshwa katika masimulizi mengi ya Biblia.

5 Hivyo basi, badala ya kuweka kinyongo inapoonekana wanadamu hawawezi kutoa msaada unaohitajika, zione hali hizo kama mtume Paulo alivyoziona, yaani, nafasi za kumtegemea Yehova kwa ukamili na kujionea jinsi anavyokujali. Hilo litaimarisha imani yako na kufanya uhusiano wako na Yehova uwe halisi zaidi.

NI MUHIMU SANA KUMTEGEMEA YEHOVA

6. Kwa nini huenda nyakati fulani ikawa vigumu kumtegemea Yehova tunapokabili tatizo gumu?

6 Je, inawezekana kumweleza Yehova katika sala tatizo gumu unalokabili na baada ya kumweleza upate amani ya akili, ukijua kuwa umefanya yote uliyoweza na kuacha mambo mikononi mwake? Bila shaka, inawezekana! (Soma Zaburi 62:8; 1 Petro 5:7.) Kumtegemea Yehova ni muhimu sana ili kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye. Lakini si rahisi sikuzote kuwa na imani kwamba Yehova atatimiza mahitaji yako. Kwa nini? Huenda sababu moja ni kwamba si mara zote Yehova hujibu sala papo hapo.—Zab. 13:1, 2; 74:10; 89:46; 90:13; Hab. 1:2.

7. Kwa nini si mara zote Yehova hujibu sala zetu papo hapo?

7 Kwa nini Yehova hajibu papo hapo kila jambo tunaloomba? Biblia inalinganisha uhusiano wetu na Yehova na ule wa baba na mtoto. (Zab. 103:13) Baba hampi mtoto wake kila kitu anachoomba, na si lazima ampe kile anachoomba papo hapo. Baba anajua kwamba mtoto anaweza kuomba kitu fulani ghafla na baada ya muda mfupi asikitake tena. Pia, baba anajua jambo linalomfaa zaidi mtoto wake, na jinsi linavyoweza kuwaathiri wengine. Anajua kitu ambacho mtoto anahitaji na wakati wa kumpa. Isitoshe, ikiwa baba anampa papo hapo mtoto wake kila kitu anachoomba, basi uhusiano wao utageuka na kuwa wa bwana na mtumwa, yaani mtoto akiwa bwana na baba mtumwa. Vivyo hivyo, Yehova anatutakia mema na hivyo anaweza kuruhusu wakati upite kabla ya kujibu sala zetu. Ana haki ya kufanya hivyo kwa kuwa yeye ni Muumba wetu, Bwana mwenye upendo, na Baba yetu wa mbinguni. Kujibu maombi yetu yote papo hapo kunaweza kuharibu uhusiano wetu mzuri pamoja naye.—Linganisha na Isaya 29:16; 45:9.

8. Yehova anatuahidi nini kuhusiana na mambo tunayoweza na tusiyoweza kuvumilia?

8 Sababu nyingine ni kwamba Yehova anajua vizuri mambo tunayoweza na tusiyoweza kuvumilia. (Zab. 103:14) Hivyo, hatarajii tuvumilie kwa nguvu zetu wenyewe, badala yake akiwa Baba yetu, yeye hutusaidia. Bila shaka, nyakati nyingine huenda tukahisi kwamba uvumilivu wetu umefikia mwisho. Lakini Yehova anatuhakikishia kwamba hataruhusu kamwe watumishi wake wajaribiwe kupita wanavyoweza kuvumilia. Naam, “ataifanya pia njia ya kutokea.” (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Hivyo basi, tuna sababu nzuri ya kumtegemea Yehova kwa kuwa anajua vizuri mambo tunayoweza na tusiyoweza kuvumilia.

9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa maombi yetu hayajajibiwa haraka?

9 Ikiwa hatujapata msaada wa haraka hata baada ya kumwomba Yehova, acheni tuendelee kumngojea, kwani anajua vizuri sana wakati wa kutusaidia. Kumbuka kwamba yeye pia anaonyesha subira, kwani anatamani sana kutusaidia. “Yehova ataendelea kutarajia kuwaonyesha ninyi kibali, na kwa hiyo atasimama ili kuwaonyesha ninyi rehema. Kwa maana Yehova ni Mungu wa hukumu. Wenye furaha ni wale wote wanaoendelea kumtarajia.”—Isa. 30:18.

“KINYWA CHA SIMBA”

10-12. (a) Ni hali gani zinaweza kufanya mambo yawe magumu wakati wa kumuuguza mtu wa familia? (b) Uhusiano wako na Yehova unaathiriwaje unapomtegemea ukiwa katika hali ngumu? Toa mfano.

10 Unapokabili hali ngumu sana, huenda ukahisi kama mtume Paulo alivyohisi, yaani, uko katika au unakaribia kuwa katika “kinywa cha simba.” Ni muhimu sana kumtegemea Yehova nyakati kama hizo, ingawa si rahisi kufanya hivyo. Kwa mfano, wazia unamuuguza mtu wa familia anayeumwa ugonjwa usio na tiba. Labda umemwomba Yehova akupe hekima na nguvu. * Kwa kuwa umefanya yote unayoweza, je, huhisi umepata amani kwa kujua kwamba Yehova anaona na atakupa msaada unaohitaji ili ubaki mwaminifu na uendelee kuvumilia?—Zab. 32:8.

11 Huenda hali zikafanya uhisi kwamba Yehova hakusaidii. Huenda maoni ya madaktari yanatofautiana kuhusu jambo la kufanya. Au labda watu wako wa ukoo ambao ungetarajia wakufariji ndio wanaofanya hali yako iwe ngumu zaidi. Endelea kumtegemea Yehova ili akuimarishe. Endelea kumkaribia zaidi. (Soma 1 Samweli 30:3, 6.) Baadaye, utakapotambua jinsi Yehova alivyokusaidia, uhusiano wenu utaimarika.

12 Hivyo ndivyo Linda * anavyohisi. Aliwauguza wazazi wake kwa miaka kadhaa kabla hawajafa. Anasema hivi: “Tulipokabili hali hiyo, ilikuwa vigumu sana kwangu, kwa mume wangu, na kaka yangu kujua jambo la kufanya. Nyakati fulani tulihisi kwamba hatuna msaada wowote. Hata hivyo, tunapokumbuka hali hiyo, kwa kweli tunaona waziwazi jinsi Yehova alivyotusaidia. Alituimarisha na kutupatia msaada tuliohitaji, hata ilipoonekana kwamba hatukuwa na jambo la kufanya.”

13. Kumtegemea Yehova kulimsaidiaje Rhonda kukabiliana na majanga?

13 Kumtegemea Yehova kwa ukamili kunaweza kutusadia pia tunapokumbwa na majanga. Fikiria mambo yaliyompata Rhonda: Mume wake, ambaye si Shahidi, alipokuwa akimtaliki, ndugu yake mdogo alianza kusumbuliwa na ugonjwa unaoitwa lupus, ugonjwa hatari sana unaoweza kusababisha kifo. Miezi michache baadaye, mke wa kaka yake alikufa. Rhonda alipohisi kwamba ameanza kupata ahueni kutokana na maumivu yaliyosababishwa na matatizo hayo, alianza kufanya upainia wa kawaida. Baada ya muda mfupi mama yake akafa. Ni nini kilimsaidia Rhonda kukabiliana na matatizo hayo? Anaeleza hivi: “Niliwasiliana na Yehova kila siku, hata nilipotaka kufanya uamuzi mdogo. Kwa kufanya hivyo nilimwona Yehova kuwa halisi kwangu. Nilijifunza kumtegemea Yehova badala ya kujitegemea au kuwategemea watu wengine. Kwa kweli alinipa msaada niliohitaji—alitosheleza mahitaji yangu yote. Matokeo ni kwamba nimekuwa na uhusiano wa karibu sana na Yehova.”

Hata katika familia, hali ngumu inaweza kutokea ambayo itajaribu uhusiano wetu na Yehova (Tazama fungu la 14-16)

14. Yehova anaweza kukusaidiaje mtu wa ukoo anapotengwa na ushirika?

14 Fikiria hali nyingine. Wazia kwamba mtu fulani wa ukoo unayempenda ametengwa na ushirika. Unajua vizuri yale ambayo Biblia inasema kuhusu jinsi tunavyopaswa kumtendea mtu aliyetengwa na ushirika. (1 Kor. 5:11; 2 Yoh. 10) Hata hivyo, huenda nyakati fulani ikaonekana kuwa vigumu sana, au haiwezekani kuunga mkono uamuzi wa kutenga na ushirika. * Je, utamtegemea Baba yako wa mbinguni akupe nguvu unazohitaji ili utii mwongozo wa Biblia unaohusu kutenga na ushirika? Je, utatumia nafasi hiyo kuimarisha zaidi uhusiano wako na Yehova?

15. Kwa nini Adamu hakutii amri ya Yehova?

15 Kuhusiana na jambo hilo, hebu mfikirie mwanadamu wa kwanza, Adamu. Je, kweli aliamini kwamba angeendelea kuishi pasipo kumtii Yehova? La hasha! Maandiko yanatuambia kwamba Adamu “hakudanganywa.” (1 Tim. 2:14) Basi, kwa nini hakutii? Adamu alikula tunda alilopewa na Hawa kwa sababu alimpenda zaidi mke wake kuliko Yehova. Aliisikiliza sauti ya mke wake badala ya sauti ya Mungu wake, Yehova.—Mwa. 3:6, 17.

16. Ni nani tunayepaswa kumpenda zaidi, na kwa nini?

16 Je, hilo linamaanisha kwamba tusiwapende sana watu wetu wa ukoo? Hapana. Hata hivyo, tunapaswa kumpenda zaidi Yehova. (Soma Mathayo 22:37, 38.) Ni wazi kwamba kufanya hivyo kutawanufaisha watu wetu wa ukoo, iwe sasa wanamtumikia Yehova au la. Kwa hiyo, endelea kuimarisha uhusiano wako na Yehova na umtegemee. Ikiwa unahangaishwa na hali ya mtu wako wa ukoo aliyetengwa na ushirika, sali kwa Yehova na umweleze hisia zako zote. * (Rom. 12:12; Flp. 4:6, 7) Tumia nafasi hiyo kuimarisha zaidi uhusiano wako na Yehova. Kufanya hivyo kutakusaidia umtegemee Yehova na hatimaye utapata matokeo mazuri.

TUNAPOMNGOJEA YEHOVA

Onyesha kwamba unamtegemea Yehova kwa kushiriki kwa bidii katika kazi yake (Tazama fungu la 17)

17. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamtegemea Yehova?

17 Kwa nini Paulo ‘alikombolewa kutoka katika kinywa cha simba’? Anaeleza hivi: “Ili kupitia mimi kazi ya kuhubiri itimizwe kwa ukamili na mataifa yote yaisikie.” (2 Tim. 4:17) Kama Paulo, sisi pia tukiwa na bidii katika kazi ya kuhubiri, tuna hakika kwamba Yehova ‘atatuongezea’ mahitaji yetu mengine yote ya msingi. (Mt. 6:33) Tukiwa wahubiri wa Ufalme, Yehova ametukabidhi “habari njema,” na anatuita “wafanyakazi wenzi.” (1 The. 2:4; 1 Kor. 3:9) Tukishiriki kwa bidii katika kazi ya Mungu, itakuwa rahisi kumngojea Yehova ajibu sala zetu.

18. Tunapaswa kufanya nini ili tumtegemee Yehova kikamili na kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye?

18 Basi, acheni tutumie wakati huu kuimarisha uhusiano wetu na Mungu. Ikiwa hali fulani inakuhangaisha, tumia nafasi hiyo kumkaribia zaidi Yehova. Naam, soma kwa bidii Neno la Mungu, sali bila kuacha, na jihusishe kikamili katika mambo ya kiroho. Ukifanya mambo hayo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakusaidia kuvumilia hali zako sasa, na jambo lolote linaloweza kutokea wakati ujao.

^ fu. 2 “Kinywa cha simba” ambacho Paulo alikombolewa huenda kilimaanisha kinywa cha simba halisi au ulikuwa mfano tu.

^ fu. 10 Makala kadhaa zimechapishwa ili kuwasaidia Wakristo kukabiliana na ugonjwa, na kuwasaidia wale wanaouguza. Tazama gazeti la Amkeni! la Februari 8, 1994; Februari 8, 1997; Mei 22, 2000; na Januari 22, 2001.

^ fu. 12 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 14 Tazama makala yenye kichwa “Kutenga na Ushirika Ni Mpango Wenye Upendo,” katika gazeti hili.

^ fu. 16 Makala kadhaa zimechapishwa ili kutusaidia kufuata mwogozo wa Biblia mshiriki wa familia tunayempenda anapomwacha Yehova. Tazama gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 2006, ukurasa wa 17-21, na Januari 15, 2007, ukurasa wa 17-20.