Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Anaelewa Maumivu Yetu

Anaelewa Maumivu Yetu

Mkaribie Mungu

Anaelewa Maumivu Yetu

Yohana 11:33-35

‘KUWA na hisia-mwenzi ni kuhisi maumivu yako moyoni mwangu.’ Hivyo ndivyo mmishonari mzee ambaye ni Shahidi wa Yehova alivyofafanua sifa hiyo ya maana sana. Yehova Mungu anatuwekea kielelezo bora zaidi cha kuonyesha hisia-mwenzi. Watu wake wanapoteseka, anahisi uchungu. Tunajuaje? Yesu alipokuwa duniani, maneno na matendo yake yalionyesha kikamili hisia-mwenzi ya Yehova. (Yohana 5:19) Kwa mfano, fikiria kisa kinachosimuliwa katika Yohana 11:33-35.

Rafiki ya Yesu, Lazaro, alipokufa ghafula, Yesu alienda kwenye kijiji ambacho Lazaro aliishi. Inaeleweka kwa nini dada za Lazaro, Maria na Martha, walilemewa na huzuni. Yesu aliipenda sana familia hiyo. (Yohana 11:5) Basi, angechukua hatua gani? Simulizi linasema hivi: “Yesu alipomwona [Maria] akilia na Wayahudi waliokuja pamoja naye wakilia, akaugua rohoni na kutaabika; naye akasema: ‘Mmemlaza wapi?’ Wakamwambia: ‘Bwana, njoo uone.’ Yesu akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33-35) Kwa nini Yesu alilia? Ni kweli kwamba rafiki yake mpendwa Lazaro alikuwa amekufa, lakini muda si muda Yesu angemfufua. (Yohana 11:41-44) Je, kuna jambo lingine lililogusa hisia za Yesu?

Angalia tena maneno yaliyotajwa juu. Ona kwamba Yesu alipomwona Maria na wale waliokuwa pamoja naye wakilia, ‘aliugua rohoni’ na “kutaabika.” Maneno ya lugha ya awali yaliyotumiwa katika mstari huo yanaonyesha hisia nyingi sana. * Yesu aliguswa moyo sana na mambo aliyoyaona. Hisia nyingi alizokuwa nazo zilionekana wazi alipotokwa na machozi. Kwa wazi, moyo wa Yesu uliguswa na maumivu ya wengine. Je, umewahi kutokwa na machozi kwa sababu mtu fulani unayemjali alikuwa akilia?—Waroma 12:15.

Hisia-mwenzi ya Yesu inatusaidia kuelewa zaidi sifa na matendo ya Baba yake, Yehova. Kumbuka kwamba Yesu aliiga sifa za Baba yake kikamili hivi kwamba angeweza kusema: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Kwa hiyo, tunaposoma kwamba ‘Yesu alitokwa na machozi,’ tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anahisi uchungu wakati waabudu wake wanapoteseka. Kwa kweli, waandikaji wengine wa Biblia wanathibitisha jambo hilo. (Isaya 63:9; Zekaria 2:8) Yehova ni Mungu mwenye huruma kama nini!

Tunavutiwa na watu wenye hisia-mwenzi. Tunapovunjika moyo au kushuka moyo, tunavutiwa na mwanadamu mwenzetu anayeweza kuelewa hali zetu na kutambua uchungu wetu. Tunavutiwa hata zaidi na Yehova, Mungu mwenye huruma anayehisi maumivu yetu na kuelewa sababu ya machozi yetu!—Zaburi 56:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “akatokwa na machozi” mara nyingi linamaanisha “kulia kimyakimya,” lakini neno linalotumiwa kufafanua kilio cha Maria na cha watu wale wengine linaweza kumaanisha “kulia kwa sauti, kuomboleza.”