Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msiba Wakumba Visiwa Vya Solomon

Msiba Wakumba Visiwa Vya Solomon

Msiba Wakumba Visiwa Vya Solomon

Mnamo Jumatatu (Siku ya 1), Aprili 2, 2007 (2/4/2007), tetemeko la nchi la kipimo cha 8.1 lilitikisa maeneo fulani ya Visiwa vya Solomon, ambavyo ni visiwa vyenye joto vilivyo kaskazini-mashariki ya Australia. Baada ya dakika chache, wimbi la maji ambalo inasemekana lilikuwa na urefu wa mita kumi lilipiga visiwa hivyo katika Jimbo la Magharibi. Wimbi hilo lilisababisha vifo vya watu 52 na 6,000 wakabaki bila makao.

Mji wa Gizo ulio katika pwani ya Kisiwa cha Ghizo, ambao una wakaaji 7,000 hivi uliharibiwa sana na maji hayo. Mji huo uko umbali wa kilomita 45 tu kutoka chanzo cha tetemeko hilo. Jioni hiyo, kutaniko dogo la Mashahidi wa Yehova katika mji wa Gizo lilikuwa likitazamia kuadhimisha Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu. (1 Wakorintho 11:23-26) Siku ilianza kama kawaida kwa mapambazuko maridadi, nayo bahari ilikuwa imetulia. Kisha, saa 1:39 asubuhi, tetemeko la nchi likatokea.

Tetemeko la Nchi!

Ron Parkinson, mzee wa kutaniko, na mke wake, Dorothy, walikuwa wakitayarisha kiamsha-kinywa tetemeko hilo lilipotokea. Ron anasema hivi: “Nyumba yetu nzee iliyumbayumba kama mnazi lakini haikuanguka. Kulikuwa na kelele nyingi sana. Makabati, vyombo vya mbao, piano, sahani, vikombe, na vifaa vingine vilianguka chini kwa kishindo. Baada ya kujitahidi sana, tulifaulu kutoka nje. Dorothy hakuwa amevaa viatu, hivyo miguu yake ilikatwa-katwa na glasi zilizovunjika.”

Tony na Christine Shaw, ambao ni wamishonari wanaoishi karibu, walikimbia pia nje ya nyumba yao. Christine anasema: “Nchi ilitetemeka kwa nguvu sana hivi kwamba nilianguka chini na singeweza kusimama. Nyumba zilizosombwa na maji zilikuwa zikielea baharini. Nyumba hizo ziling’olewa na wimbi kubwa kutoka kwenye misingi yake. Watu walizunguka kote kwa mitumbwi katikati ya mchafuko huo wote huku wakitafuta waokokaji. Kisha, tetemeko lingine kubwa likatokea na kufuatwa na lingine. Matetemeko mengine madogo yaliendelea kwa siku tano. Ilikuwa hali yenye kutisha!”

Tsunami Inakuja

Patson Baea alikuwa kwenye kisiwa chao cha Sepo Hite, kilomita sita hivi kutoka Gizo, wakati tetemeko la nchi lilipotokea. Ni nini kilichowapata Patson na familia yake wakati wa msiba huo?

Patson anasema hivi kuhusu tukio hilo: “Nilikimbia kwenye ufuo kuelekea mahali ambapo mke wangu, Naomi, na watoto wetu wanne walipokuwa. Waliangushwa chini na tetemeko hilo lakini walikuwa salama. Watoto walikuwa wakitetemeka, na wengine wao walikuwa wakilia. Mara moja mimi na Naomi tuliwatuliza.

“Niligundua kwamba bahari ilikuwa ikisukasuka kwa njia isiyo ya kawaida. Ilikuwa wazi kwamba tsunami inakuja. Kisiwa chetu kidogo kilikabili hatari ya kufagiliwa na maji. Mama yangu, Evalyn, ambaye aliishi kwenye kisiwa kidogo cha karibu, alikuwa pia hatarini. Mara moja niliamuru familia yangu iingie ndani ya mtumbwi wetu ili twende kumwokoa.

“Baada ya kusafiri kwa muda mfupi, wimbi kubwa sana la maji lilipita chini ya mtumbwi wetu. Bahari iliyumbayumba na kusukasuka. Tulipofika, mama alikuwa ameshtuka na kuchanganyikiwa sana hivi kwamba aliogopa kuingia ndani ya maji. Naomi na Jeremy, mwana wetu mwenye umri wa miaka 15, waliingia ndani ya maji hayo yenye nguvu na kumsaidia kuogelea ili afike kwenye mtumbwi. Kisha, tuliendesha mtumbwi huo kwa kasi sana kurudi baharini.

“Kufikia sasa maji ya bahari yalikuwa yamepungua sana hivi kwamba miamba ya bahari ilikuwa inaonekana katika visiwa vyote. Kwa ghafula, wimbi kubwa sana la maji lilikuja na kufurika kwenye visiwa vyote viwili. Nyumba yetu ya wageni iliyo kando ya bahari iling’olewa kutoka kwenye misingi yake na kuvunjwa-vunjwa kabisa. Maji yaliingia katika nyumba yetu na kuharibu vitu vyetu vingi. Maji ya bahari yalipopungua, tuliokoa Biblia na vitabu vya nyimbo kutoka katika nyumba yetu iliyoharibika, kisha tukarudi Gizo.”

Vitu viliharibiwa kwenye ufuo na watu wengi walikufa. Upande wa magharibi wa Kisiwa cha Ghizo ndio ulioharibiwa zaidi. Vijiji 13 hivi vya upande huo vilifagiliwa na wimbi la maji lenye urefu wa mita tano!

Usiku huo, watu 22 walikusanyika katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova huko Gizo ili kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu. Inafurahisha kwamba hakuna yeyote kati yao aliyeumia sana kutokana na msiba huo. Ron aliyetajwa mwanzoni anasema hivi: “Hakukuwa na umeme, na taa zetu za mafuta zilikuwa zimevunjika. Kwa hiyo, Ndugu Shaw alitoa hotuba akitumia tochi. Tukiwa gizani, tuliimba nyimbo za kumshukuru Yehova kwa sauti kubwa mbalimbali zenye kuvutia.”

Kazi ya Kutoa Misaada

Habari za msiba huo zilipofika mji mkuu, Honiara, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko ilianza kupeleka misaada ya dharura haraka. Ofisi ya tawi ilipiga simu haraka ili kuhakikisha kwamba Mashahidi wengi walioishi katika maeneo hayo walikuwa salama. Watu wenye kutegemeka walitumwa ili wamtafute Shahidi fulani aliyeishi mbali katika Kisiwa cha Choiseul. Walifaulu kumpata akiwa salama salimini. Pia, pesa zilitumwa huko Gizo ili kununua vitu vya dharura.

Wawakilishi wa ofisi ya tawi walifika Gizo Alhamisi (Siku ya 4) kwa ndege ya kwanza. Craig Tucker, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi anasema: “Tulibeba masanduku mengi yenye misaada. Mizigo ya wasafiri wengine iliachwa kwa sababu ndege haingebeba mizigo yote, lakini tulifurahi kwamba masanduku yetu yote yalifika salama. Masanduku hayo yalikuwa kati ya mizigo ya kwanza ya misaada kufika katika eneo la msiba. Misaada zaidi ililetwa siku mbili baadaye kwa boti.”

Tony Shaw na Patson Baea, pamoja na Mashahidi wengine kutoka Gizo, walisafiri muda wa saa mbili kwa mtumbwi kwenda kuwasaidia Mashahidi walioishi mbali kwenye kisiwa cha Ranongga. Nguvu za tetemeko hilo zilifanya kisiwa hicho chenye urefu wa kilomita 32 na upana wa kilomita 8, kiinuke kwa zaidi ya mita 2 juu ya bahari! Inaonekana kwamba msukosuko wa maji yaliyozunguka kisiwa hicho ulisababisha tsunami hiyo ambayo ilipiga visiwa vya karibu.

Tony anasema: “Washiriki wa kutaniko walifurahi sana kutuona. Walikuwa salama salimini nao waliishi nje kwa sababu waliogopa mitetemeko midogo iliyofuata. Boti yetu ndiyo iliyokuwa ya kwanza kuleta misaada. Kabla ya kuondoka, tulitoa sala ya kutoka moyoni ya kumshukuru Yehova.”

Patson anasema: “Siku kadhaa baadaye, tulirudi Ranongga kupeleka misaada zaidi na kuitafuta familia fulani ya Mashahidi ambayo iliishi katika sehemu ya mbali sana ya kisiwa hicho. Mwishowe, tulimpata Matthew Itu na familia yake wakiwa wamepiga kambi porini. Walilia kwa furaha, kwa kuwa waliona kwamba hatukuwasahau! Tetemeko la nchi liliharibu nyumba yao pamoja na majengo mengi katika kijiji chao. Hata hivyo, hangaiko lao kubwa lilikuwa kupata Biblia mpya kwa ajili ya familia yao kwa sababu Biblia zao zilipotea wakati wa msiba huo.”

Watazamaji Waliwasifu Mashahidi

Watu wengine waliona upendo huo wa Kikristo. Craig Tucker anasema hivi: “Mwandishi mmoja wa habari ambaye alishutumu jitihada za ujumla za kuandaa misaada alishangaa na kuvutiwa aliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova waliwapa washiriki wao chakula, vyandarua, na vitu vingine muhimu siku chache tu baada ya tetemeko hilo.” Patson anaongeza hivi: “Wanakijiji wa Ranongga walisifu jitihada zetu za haraka za kutoa misaada na kulaumu kanisa lao kwa sababu halikuwasaidia.” Mwanamke mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Tengenezo lenu lilichukua hatua ya haraka ya kutoa msaada!”

Mashahidi waliwasaidia pia majirani wao. Christine Shaw anasema: “Tulipotembelea hospitali ya muda huko Gizo, tuliona wenzi wa ndoa ambao tulikuwa tumewahubiria siku chache mapema. Wote wawili walikuwa wameumia na walikuwa wameshtuka sana. Mjukuu wa mwanamke huyo alikuwa amekufa maji wakati tsunami ilipomfagilia kutoka mikononi mwake. Tulirudi haraka nyumbani ili kuwaletea chakula na mavazi. Walishukuru sana.”

Kwa kweli, watu wanaokumbwa na misiba ya asili hawahitaji misaada ya kimwili tu. Wanahitaji hasa faraja ambayo inatoka tu katika Neno la Mungu, Biblia. Ron anasema: “Wahudumu fulani wa kidini walisema kwamba Mungu alikuwa akiwaadhibu watu hao kwa sababu ya dhambi zao. Lakini tuliwaonyesha kupitia Biblia kwamba Mungu hasababishi kamwe uovu. Wengi walitushukuru kwa sababu ya kuwapa faraja ya kiroho.”—2 Wakorintho 1:3, 4; Yakobo 1:13. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 24 Ona habari yenye kichwa “‘Kwa Nini?’—Kujibu Swali Gumu Zaidi,” katika toleo la Amkeni! la Novemba 2006, ukurasa wa 3–9. Mamia ya nakala za toleo hilo zilisambazwa huko Gizo baada ya msiba.

[Mchoro/Ramani katika ukurasa wa 13]

 

Choiseul

Ghizo

Gizo

Ranongga

HONIARA

AUSTRALIA

[Picha katika ukurasa wa 15]

Familia ya Baea katika mtumbwi wao

[Picha katika ukurasa wa 15]

Uharibifu uliosababishwa na tsunami huko Gizo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Jumba hili la Ufalme ndilo jengo pekee ambalo halikuharibiwa huko Lale kwenye Kisiwa cha Ranongga