Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Misiba ya Asili Ni Adhabu Kutoka Kwa Mungu?

Je, Misiba ya Asili Ni Adhabu Kutoka Kwa Mungu?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Misiba ya Asili Ni Adhabu Kutoka Kwa Mungu?

Mungu hatumii misiba ya asili kuwaadhibu watu wasio na hatia. Hajawahi kufanya hivyo, naye hatafanya hivyo kamwe. Kwa nini? Kwa sababu katika 1 Yohana 4:8, Biblia inasema “Mungu ni upendo.”

Matendo yote ya Mungu yanachochewa na upendo. Upendo hauwaumizi wale wasio na hatia, kwa kuwa Biblia inasema kwamba “upendo haumfanyii uovu jirani ya mtu.” (Waroma 13:10) Biblia inasema hivi katika Ayubu 34:12: “Kwa kweli, Mungu hatendi kwa uovu.”

Ni kweli kwamba Biblia ilitabiri kungekuwa na misiba katika nyakati zetu, kama vile “matetemeko makubwa ya nchi.” (Luka 21:11) Lakini Yehova hapaswi kulaumiwa kwa sababu ya uharibifu unaosababishwa na matetemeko hayo kama vile mtabiri wa hali ya hewa hapaswi kulaumiwa kwa sababu ya uharibifu unaosababishwa na dhoruba aliyotabiri. Ikiwa Mungu hasababishi mateso yanayowapata wanadamu kutokana na misiba ya asili, ni nani anayefanya hivyo?

Biblia inasema kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu,” Shetani Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Amekuwa muuaji tangu alipoasi katika siku za wanadamu wa kwanza. (Yohana 8:44) Shetani haoni uhai wa wanadamu kuwa wenye thamani au wa maana. Anaongozwa na tamaa ya makuu ya uchoyo. Kwa hiyo, si ajabu kwamba ameanzisha mfumo wa ulimwenguni pote unaokazia uchoyo. Katika ulimwengu wa leo, wanadamu wamewalazimisha wanadamu wenzao wasio na uwezo waishi katika maeneo hatari, mahali ambako misiba ya asili au ile inayosababishwa na wanadamu inaweza kutukia. (Waefeso 2:2; 1 Yohana 2:16) Hivyo, wanadamu wenye pupa wanapaswa kulaumiwa kwa misiba fulani ambayo imewapata wanadamu wenzao. (Mhubiri 8:9) Kwa nini?

Idadi kubwa ya misiba inasababishwa kwa kadiri fulani na wanadamu. Kwa mfano, fikiria taabu zilizowakumba wakaaji wa jiji la New Orleans, Marekani, ambalo lilipigwa na kimbunga kilichosababisha mafuriko, au nyumba zilizoharibiwa na maporomoko ya udongo kando ya milima ya pwani huko Venezuela. Katika visa hivyo na vinginevyo, vitu vya asili, kama vile upepo na mvua, vilisababisha misiba hasa kwa sababu ya ukosefu wa ujuzi, kazi mbaya ya uinjinia, mipango mibaya, kutotii maonyo, na makosa ya wenye madaraka.

Fikiria msiba uliotukia nyakati za Biblia. Katika siku za Yesu, watu 18 walikufa mnara fulani ulipoporomoka ghafula. (Luka 13:4) Huenda msiba huo ulisababishwa na makosa ya wanadamu, “wakati na tukio lisilotazamiwa,” au yote mawili—lakini haikuwa hukumu kutoka kwa Mungu.—Mhubiri 9:11.

Je, Mungu amewahi kusababisha misiba fulani? Ndiyo, lakini tofauti na misiba ya asili na ile inayosababishwa na wanadamu, misiba hiyo iliwapata watu fulani hususa, ilikuwa na kusudi fulani, na ilitukia mara chache sana. Gharika ya ulimwenguni pote katika siku za Noa na uharibifu wa majiji ya Sodoma na Gomora katika siku za Loti ni mifano miwili ya misiba hiyo. (Mwanzo 6:7-9, 13; 18:20-32; 19:24) Hukumu hizo kutoka kwa Mungu zilifagilia mbali wanadamu waovu wasiotubu, lakini wanadamu waadilifu machoni pa Mungu waliokolewa.

Kwa hakika, Yehova Mungu ana uwezo, anataka, na ana nguvu za kukomesha mateso yote na madhara ya misiba ya asili. Zaburi 72:12 ilitabiri hivi kumhusu Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa na Mungu: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi.”