Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tunapaswa Kumuuliza Mungu Maswali?

Je, Tunapaswa Kumuuliza Mungu Maswali?

WATU fulani husema kwamba ni makosa kumuuliza Mungu maswali. Huenda wakahisi kwamba ni kukosa heshima kumuuliza Mungu kwa nini anaruhusu au kutoruhusu mambo fulani yafanyike. Je, una maoni kama hayo?

Ikiwa ndivyo, huenda ukashangaa kujua kwamba watu wengi wazuri wamewahi kumuuliza Mungu maswali. Kwa mfano, ona maswali yafuatayo ambayo wamemuuliza:

Mwanamume mwaminifu Ayubu aliuliza: “Kwa nini waovu wanaendelea kuishi, wamezeeka, pia wamekuwa na mali nyingi zaidi?”Ayubu 21:7.

Nabii mwaminifu Habakuki aliuliza: “Kwa nini unawatazama wale wanaotenda kwa hila, na kukaa kimya wakati mtu mwovu anapommeza mtu aliye mwadilifu kuliko yeye?”Habakuki 1:13.

Yesu Kristo aliuliza: “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”Mathayo 27:46.

Ukisoma muktadha wa maandiko hayo, utaona hakuna jambo linaloonyesha kwamba Yehova * Mungu alikasirika alipoulizwa maswali hayo ya unyoofu. Kwa kweli, haishangazi kwamba alikubali kuulizwa maswali. Kwa mfano, Mungu hakasiriki tunapomwomba atosheleze mahitaji yetu ya kimwili ambayo yanatusaidia kuwa na afya nzuri. Anafurahia kutosheleza mahitaji hayo. (Mathayo 6:11, 33) Vivyo hivyo, kwa kupenda anatupatia habari ambazo zinaweza kutusaidia kuwa na hali nzuri kiakili na kihisia. (Wafilipi 4:6, 7) Hata Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa.” (Mathayo 7:7) Maneno yanayozunguka ahadi hiyo ya Yesu yanaonyesha kwamba hakuwa akizungumzia tu kupokea vitu vya kimwili bali pia kupata majibu ya maswali muhimu.

Kama ungepewa nafasi, ungependa kumuuliza Mungu swali gani kati ya maswali yafuatayo?

  • Je, maisha yangu yana kusudi?

  • Ni nini kitakachonipata nitakapokufa?

  • Kwa nini unaruhusu niteseke?

Kwa kuwa “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu,” utapata majibu ya maswali hayo katika Neno lake, Biblia. (2 Timotheo 3:16) Ona kwa nini watu fulani wameuliza maswali yaliyo hapo juu na pia majibu ambayo Biblia inatoa.

^ fu. 7 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.