Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, imani ya kidini ni kama tu kitulizo cha kihisia?

Je, imani ya kidini ni kama tu kitulizo cha kihisia?

Kitulizo cha kihisia ni mawazo ambayo mtu hujidanganya nayo na yanayomfanya apuuze uhalisi wa mambo na hivyo kukosa kufikiri kwa njia inayopatana na akili. Kwa mfano, watu fulani hutumia pombe ili kutuliza hisia zao. Mwanzoni, pombe inaweza kuwafanya wajiamini zaidi na wakabiliane na matatizo ya maisha. Lakini mwishowe watu wanaotegemea pombe ili kutuliza hisia hupata madhara. Je, inaweza kuwa hivyo kuhusiana na imani ya kidini?

Watu fulani hulinganisha imani na kufuata jambo bila kufikiri. Wanasema kwamba watu wanaofuata imani hawataki kufikiria wenyewe wala kuruhusu mambo yaliyothibitishwa yaongoze itikadi zao. Watu kama hao wenye shaka hudai kwamba wale walio na imani thabiti ya kidini hupuuza uhalisi wa mambo.

Biblia inasema mambo mengi kuhusu imani. Hata hivyo, haitutii moyo tuamini mambo bila kufikiri. Pia, haituhimizi tuamini mambo kijuujuu. Badala yake, inasema kwamba watu wanaoamini kila neno wanalosikia hawana uzoefu, na ni wapumbavu. (Methali 14:15, 18) Kwa kweli, ni jambo la kipumbavu kukubali mawazo bila kuchunguza mambo yanayohusika! Kufanya hivyo, ni kama kufumba macho na kujaribu kuvuka barabara yenye magari mengi kwa sababu tu mtu fulani ametuambia tufanye hivyo.

Badala ya kutuhimiza tuamini mambo bila kufikiri, Biblia inatuhimiza tuwe macho ili tusidanganywe. (Mathayo 16:6) Kuwa macho kunamaanisha kutumia “nguvu [zetu] za kufikiri.” (Waroma 12:1) Biblia inatuzoeza kufikiri kwa kuchunguza uthibitisho na kufanya maamuzi yanayotegemea mambo yaliyothibitishwa. Fikiria mifano fulani katika maandishi ya mtume Paulo.

Paulo alipowaandikia washiriki wa kutaniko la Roma, hakutaka wamwamini Mungu kwa sababu tu aliwaambia wafanye hivyo. Badala yake, aliwatia moyo wachunguze uthibitisho wa kwamba Mungu ni halisi. Aliandika hivi: “Sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu, hivi kwamba [wale wanaokataa mamlaka yake] hawana sababu ya kujitetea.” (Waroma 1:20) Paulo alitumia njia hiyohiyo ya kufikiri alipoandika barua yake kwa Waebrania. “Bila shaka, kila nyumba hujengwa na mtu fulani,” akasema, “lakini yeye aliyevijenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Katika barua yake kwa Wakristo walioishi jijini Thesalonike, Paulo aliwatia moyo wawe waangalifu kuhusu mambo waliyoamini. Alitaka ‘wahakikishe mambo yote.’—1 Wathesalonike 5:21.

Imani ni ngao inayoweza kutulinda

Imani ya kidini ambayo haitegemei mambo yaliyothibitishwa inaweza kuwa kitulizo cha kihisia, ambacho kinaweza kumpotosha mtu na kumletea madhara. Paulo aliandika hivi kuhusu watu fulani waliofuata dini wakati wake: “Nawatolea ushahidi kwamba wana bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Kwa hiyo, ni jambo muhimu kama nini kufuata shauri la Paulo kwa kutaniko la Roma! Aliandika: “Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu.” (Waroma 12:2) Imani inayotegemea ujuzi sahihi wa Mungu si kitulizo cha kihisia, bali ni “ngao kubwa” ambayo hutulinda kutokana na madhara ya kihisia na kiroho.—Waefeso 6:16.