Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka Katika Neno La Mungu

Kwa Nini Mungu Alimtuma Yesu Duniani?

Kwa Nini Mungu Alimtuma Yesu Duniani?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Yesu alikuwa wapi kabla Mungu hajamtuma duniani?

Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho kabla hajazaliwa huko Bethlehemu. Alikuwa kiumbe wa kwanza kuumbwa na Mungu na ndiye pekee aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. Kwa hiyo, kwa kufaa anaitwa Mwana mzaliwa pekee wa Mungu. Akiwa mbinguni, mara nyingi alikuwa msemaji wa Mungu. Hii ndiyo sababu anaitwa Neno. Pia, alikuwa msaidizi wa Mungu na alishiriki kuumba vitu vingine vyote. (Yohana 1:2, 3, 14) Yesu aliishi mbinguni kwa maelfu ya miaka kabla wanadamu hawajaumbwa.—Soma Mika 5:2; Yohana 17:5.

2. Mungu alimtumaje Mwanaye duniani?

Yehova alihamisha uhai wa Yesu kutoka mbinguni na kuuingiza katika tumbo la uzazi la Maria kupitia roho takatifu. Hivyo, Yesu hakuzaliwa kupitia nguvu za baba wa kibinadamu. Malaika walitangaza kuzaliwa kwake kwa wachungaji fulani waliokuwa nje wakati wa usiku wakichunga makundi yao. (Luka 2:8-12) Hivyo, Yesu hakuzaliwa wakati wa majira ya baridi kali lakini huenda alizaliwa mwanzoni mwa Oktoba wakati bado kulikuwa na majira ya joto. Baadaye, Maria na mume wake Yosefu, walimpeleka Yesu Nazareti, mji wa kwao, na kumlea huko. Yosefu alimtunza Yesu akiwa baba mlezi.​—Soma Mathayo 1:18-23.

Yesu alipokuwa na umri wa miaka 30 hivi, alibatizwa; na Mungu akatangaza waziwazi kwamba alikuwa Mwana wake. Kisha Yesu akaanza kufanya kazi ambayo Mungu alimtuma afanye.​—Soma Mathayo 3:16, 17.

3. Kwa nini Mungu alimtuma Yesu duniani?

Mungu alimtuma Yesu ili awafundishe watu ukweli. Yesu alifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu, serikali ya mbinguni itakayoleta amani duniani kote. Aliandaa msingi wa tumaini la uzima wa milele. (Yohana 4:14; 18:36, 37) Yesu pia aliwafundisha watu mambo mengi kuhusu kupata furaha ya kweli. (Mathayo 5:3; 6:19-21) Alifundisha kwa kuweka mfano. Kwa mfano, alionyesha jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu hata katika hali ngumu. Alipotendewa vibaya hakulipiza kisasi.​—Soma 1 Petro 2:21-24.

Yesu aliwafundisha wafuasi wake jinsi ya kuwa na upendo wa kujidhabihu. Alifurahia mapendeleo mengi alipokuwa akiishi mbinguni pamoja na Baba yake, hata hivyo, kwa unyenyekevu alimtii Baba yake na kuja duniani kuishi pamoja na wanadamu. Hakuna mtu angetuwekea mfano bora zaidi wa upendo kuliko Yesu.​—Soma Yohana 15:12, 13; Wafilipi 2:5-8.

4. Yesu alitimiza nini alipokufa?

Pia, Mungu alimtuma Yesu aje afe kwa ajili ya dhambi zetu. (Yohana 3:16) Sote ni watenda dhambi, ikimaanisha kwamba hatujakamilika na tuna mwelekeo wa kutenda dhambi. Ndiyo sababu tunakuwa wagonjwa na kufa. Kinyume na hilo, mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikuwa mkamilifu. Hakuwa na dhambi na hangekuwa mgonjwa wala kufa kamwe. Lakini alipoteza ukamilifu wake alipokosa kumtii Mungu. Tulirithi kutoka kwa Adamu dhambi na mshahara wake, yaani, kifo.​—Soma Waroma 5:12; 6:23.

Yesu ambaye alikuwa mwanadamu mkamilifu hakufa kwa sababu ya dhambi zake. Alikufa kwa ajili ya dhambi zetu. Kifo cha Yesu hufanya iwezekane kwetu kufurahia uzima wa milele na kubarikiwa na Mungu.​—Soma 1 Petro 3:18.