Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi?

Kwa nini watu fulani hawasherehekei Krismasi?

Ulimwenguni pote, karibu watu bilioni mbili husherehekea Krismasi kila Desemba 25, na watu wapatao milioni 200 husherehekea siku ya kuzaliwa kwa Yesu Januari 7. Hata hivyo, pia kuna mamilioni ya watu ambao wameamua kutosherehekea Krismasi kabisa. Kwa nini?

Sababu moja ni kwamba huenda ni washiriki wa dini ambayo si sehemu ya dini zinazodai kuwa za Kikristo. Kwa mfano, wanaweza kuwa Wayahudi, Wahindu, au Washinto. Wengine kama vile, watu wanaoamini hakuna Mungu, wanaoamini kwamba mambo yake hayawezi kujulikana, wanaopinga mambo ya kidini, au wale wanaoshikilia imani zao bila kujihusisha na dini yoyote, huona hadithi ya Krismasi kuwa hekaya.

Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba idadi fulani ya watu wanaomwamini Yesu wanapinga tamaduni za majira ya Krismasi. Kwa nini? Wanatoa sababu nne hivi.

Kwanza, hawaamini kwamba Yesu alizaliwa Desemba au Januari. Biblia haitaji tarehe hususa. Inasema hivi: “Katika nchi hiyo kulikuwako pia wachungaji wakiishi nje, wakichunga makundi yao usiku. Na kwa ghafula malaika wa Yehova akasimama kando yao, na . . . akawaambia: ‘. . . Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.’”​—Luka 2:8-11.

Hoja zenye kuaminika zinaonyesha kwamba Yesu alizaliwa karibu mwanzoni mwa mwezi wa Oktoba wakati wachungaji walikuwa wakiishi nje wakichunga makundi yao usiku. Katika miezi ya Desemba na Januari, maeneo ya mashambani yanayozunguka Bethlehemu huwa ni majira ya baridi kali sana. Hivyo, ili kuwalinda wanyama wao kutokana na baridi usiku, waliwapeleka kwenye mazizi yaliyoezekwa.

Sababu ya pili: Tukio pekee ambalo Yesu aliwaagiza kihususa wafuasi wake wakumbuke ni kifo chake, wala si kuzaliwa kwake, na huo ungefanywa kama mlo wa ushirika usio na mambo mengi. (Luka 22:19, 20) Pia, ona kwamba Injili za Marko na Yohana hazitaji kuhusu kuzaliwa kwa Yesu.

Tukio pekee ambalo Yesu aliwaagiza kihususa wafuasi wake wakumbuke ni kifo chake, wala si kuzaliwa kwake

Sababu ya tatu: Hakuna uthibitisho wa kihistoria unaoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walisherehekea kuzaliwa kwa Kristo. Hata hivyo, walikumbuka kifo chake. (1 Wakorintho 11:23-26) Lakini miaka 300 baada ya kuzaliwa kwa Yesu, dini zinazodai kuwa za Kikristo zilianza rasmi kuadhimisha Krismasi Desemba 25. Jambo la kuvutia ni kwamba katikati mwa karne ya 17, bunge la Uingereza lilipitisha sheria ya kupiga marufuku sherehe za Krismasi. Nchini Marekani, Mahakama Kuu ya Massachusetts ilichukua hatua kama hiyo. Kwa nini? Kitabu The Battle for Christmas, kinasema: “Hakuna sababu yoyote ya kibiblia au kihistoria inayothibitisha kwamba Yesu alizaliwa Desemba 25.” Kinaendelea kusema Wapuriti waliona “Krismasi kuwa sherehe ya kipagani ambayo watu fulani walijaribu kuifanya iwe ya Kikristo.”

Hilo linatusaidia kupata sababu ya nne: Chanzo kisichofaa cha sherehe hiyo. Krismasi ilitokana na ibada ya kipagani huko Roma ambayo ilikuwa na mchanganyiko wa sherehe za kuheshimu mungu wa kilimo Saratenina na mungu jua Sol Invictus, au Mithra. Wataalamu wa kuchunguza asili ya binadamu Christian Rätsch na Claudia Müller-Ebeling, ambao pia walishiriki katika kuandika kitabu Pagan Christmas, waliandika hivi: “Kama tu desturi na imani nyingi za kabla ya Ukristo, sherehe ya kale ya kukumbuka kurudi kwa jua ilibadilishwa na kuwa sherehe ya kukumbuka kuzaliwa kwa Kristo.”

Unapofikiria mambo yaliyotajwa katika makala hii, je, umeona ni kwa nini Wakristo wa kweli hawasherehekei Krismasi?