Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU: MATESO YATAKWISHA LINI?

Mwisho wa Mateso Umekaribia!

Mwisho wa Mateso Umekaribia!

Noelle alikuwa mtoto aliyependa kuchora. Siku moja wakati wa kiangazi alikuwa akitembea nyuma ya nyumba yao alipoanguka ndani ya kidimbwi cha kuogelea. Alikufa maji majuma mawili kabla hajafikisha umri wa miaka minne.

Charlotte, Daniel, Olivia, Josephine . . . Hayo ni majina ya baadhi ya wanafunzi 20 waliokuwa na umri kati ya miaka sita na saba miongoni mwa watu 26 waliouawa kwa kupigwa risasi shuleni huko Connecticut, Marekani, tarehe 14 Desemba, 2012. Wakati wa mazishi, Rais Obama alitaja majina ya watoto hao na kuwaambia waombolezaji hivi: “Lazima tukomeshe misiba hii.”

Bano, msichana mwenye umri wa miaka 18, alihamia Norway pamoja na familia yao kutoka Iraki mwaka 1996. Rafiki zake walimpa jina Miale ya Jua. Kwa kusikitisha, Julai 22, 2011, Bano alikuwa miongoni mwa watu 77 ambao waliuawa na mtu mwenye msimamo mkali aliyejivuna hivi: “Nasikitika kwamba. . . sikuua watu wengi zaidi.”

Matukio kama hayo hutukia ulimwenguni pote. Fikiria majonzi na huzuni ambayo imesababishwa na aksidenti, uhalifu, vita, ugaidi, misiba ya asili, na misiba mingine. Watu wengi wasio na hatia wamepoteza maisha yao, na mara nyingi bila sababu!

Baadhi ya watu humlaumu Mungu, wakisema Muumba wetu hatujali. Wengine husema kwamba Mungu huona mateso yanayotupata lakini anaamua kutoingilia kati. Hata hivyo, wengine husema misiba hiyo ilipangwa mapema. Watu wana maoni mbalimbali kuhusu jambo hilo. Tunaweza kupata wapi majibu yenye kutegemeka? Katika makala zifuatazo, tutachunguza Neno la Mungu, Biblia, ili tupate majibu ya chanzo cha kuteseka na mwisho wa kuteseka kwa wanadamu.