Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je,Wajua?

Je,Wajua?

Kwa nini wahalifu walivunjwa miguu kabla ya kuuawa?

Simulizi la Injili kuhusu kuuawa kwa Yesu pamoja na wahalifu wawili juu ya miti ya mateso linasema hivi: “Wayahudi wakamwomba Pilato aagize miguu yao ivunjwe na miili iondolewe.”Yohana 19:31.

Sheria ya Wayahudi ilisema kwamba maiti ya mhalifu aliyetundikwa mtini baada ya kuuawa “isibaki usiku kucha juu ya mti.” (Kumbukumbu la Torati 21:22, 23) Inaelekea Wayahudi walifuata sheria hiyo kuhusiana na mtu aliyetundikwa juu ya mti na Waroma. Katika kisa cha Yesu, kuvunja miguu ya wanaume hao kungeharakisha kifo chao ili wazikwe kabla ya Sabato kuanza baada ya jua kutua.

Kwa kawaida, mtu aliyeuawa kwa njia hiyo, alitundikwa mtini kwa kupigiliwa misumari mikononi na miguuni. Mti uliposimamishwa wima, angening’inia akiwa na maumivu makali, mwili wake wote ukiwa umeshikiliwa na misumari. Ili apumue, mtu huyo angelazimika kujiinua kwa kutumia misumari iliyopigiliwa kwenye miguu yake. Hivyo basi, mifupa ya miguu yake ilipovunjwa hangeweza kufanya hivyo. Angekufa kwa sababu ya kushindwa kupumua au kwa sababu ya mshtuko.

Makombeo yalitumiwaje vitani zamani?

Daudi alitumia kombeo kuua jitu lililoitwa Goliathi. Inaelekea Daudi alijifunza kutumia silaha hiyo alipokuwa mvulana mchungaji.1 Samweli 17:40-50.

Mchoro unaoonyesha wapiganaji Waashuru wakitumia makombeo kuvamia jiji la Wayahudi lenye ngome

Kombeo linapatikana kwenye michoro ya Wamisri na ya Waashuru wa nyakati za Biblia. Silaha hiyo ilitengenezwa kwa kuunganisha mfuko uliotengenezwa kwa ngozi au kitambaa na mikanda miwili. Mtu angeweka kwenye mfuko huo jiwe laini lenye kipenyo cha sentimeta 5 hadi 7.5 na uzito wa gramu 250 hivi. Halafu angezungusha kombeo juu ya kichwa chake na kuachilia mkanda mmoja kisha jiwe lingechomoka kwa kasi sana likiwa limelenga kabisa shabaha.

Makombeo mengi yaliyotumiwa vitani zamani yamepatikana huko Mashariki ya Kati. Inawezekana kwamba wapiganaji stadi walikuwa na uwezo wa kurusha mawe kwa kasi ya kilometa 160 hadi 240 kwa saa. Wasomi hawakubaliani ikiwa kombeo lingeweza kurusha mawe umbali ulio sawa na jinsi upinde unavyorusha mshale, lakini bado ni silaha hatari.—Waamuzi 20:16.