Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO | MARIA

Alikabiliana na Upanga wa Majonzi

Alikabiliana na Upanga wa Majonzi

MARIA alipiga magoti akiwa amelemewa na huzuni na uchungu mwingi. Bado alikuwa anakumbuka jinsi mwanawe alivyolia kwa sauti kabla hajafa baada ya kuteswa kwa saa nyingi. Kulikuwa na giza saa sita mchana. Dunia ilitetemeka kwa nguvu. (Mathayo 27:45, 51) Huenda Maria alidhani kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akionyesha ulimwengu jinsi alivyohuzunika sana kuona Yesu Kristo akifa.

Huku mwangaza wa mchana ukianza kuonekana tena huko Golgotha, yaani, Mahali pa Fuvu la Kichwa, Maria aliomboleza kifo cha mwanawe. (Yohana 19:17, 25) Huenda alianza kukumbuka mambo mengi. Labda alikumbuka jambo lililotukia miaka 33 mapema. Maria na Yosefu walipompeleka mtoto wao mpendwa hekaluni huko Yerusalemu, Simeoni, mwanamume aliyezeeka aliongozwa na roho takatifu kutoa unabii. Alitabiri mambo makuu kumhusu Yesu, lakini aliongezea kwamba siku moja, Maria angehisi kana kwamba amechomwa kwa upanga mrefu. (Luka 2:25-35) Katika kipindi hiki cha msiba, sasa Maria alijionea ukweli wa maneno hayo.

Maria alipatwa na maumivu makali ya majonzi

Inasemekana kuwa mtu anapofiwa na mtoto wake anahisi uchungu mwingi sana, na huo ndio msiba mbaya zaidi unaoweza kumpata mwanadamu. Kifo ni adui mkatili, na kinatuathiri sisi sote kwa njia fulani. (Waroma 5:12; 1 Wakorintho 15:26) Je, mtu anaweza kukabiliana na majonzi hayo? Tunapochunguza maisha ya Maria kuanzia mwanzo wa huduma ya Yesu mpaka alipokufa na baadaye, tutajifunza mengi kuhusu imani iliyomsaidia Maria akabiliane na upanga wa majonzi.

“LOLOTE ATAKALOWAAMBIA, FANYENI”

Acheni turudi nyuma miaka mitatu na nusu: Maria alijua kwamba kungekuwa na mabadiliko. Katika mji mdogo wa Nazareti, watu walikuwa wakizungumza kuhusu Yohana Mbatizaji na ujumbe wake wenye kuchochea kuhusu toba. Maria alijua kwamba mwanawe mkubwa aliona jambo hilo kuwa ishara; wakati wa kuanza huduma yake ulikuwa umefika. (Mathayo 3:1, 13) Maisha ya Maria na familia yake yangevurugika kwa kadiri fulani baada ya Yesu kuondoka nyumbani. Kwa nini?

Inaonekana kwamba huenda Yosefu, mume wa Maria tayari alikuwa amekufa. Ikiwa alikuwa amekufa, Maria alijua uchungu wa kufiwa. * Sasa Yesu hakuitwa tu “mwana wa yule seremala” bali pia “yule seremala.” Inaelekea Yesu alikuwa akiendesha biashara ya baba yake na ndiye aliyetafuta riziki ya familia yenye watoto sita hivi waliozaliwa baada yake. (Mathayo 13:55, 56; Marko 6:3) Hata kama Yesu alikuwa akimzoeza kazi Yakobo, ambaye huenda alimfuata kwa umri, haingekuwa rahisi kwa familia hiyo baada ya mwana wa kwanza kuondoka. Tayari Maria alikuwa na majukumu mengi; je, aliogopa mabadiliko hayo? Hatujui kwa hakika. Lakini hebu fikiria swali hili muhimu: Maria angehisije baada ya Yesu Mnazareti kuwa Yesu Kristo, yule Masihi aliyesubiriwa kwa muda mrefu? Simulizi  moja la Biblia linaelezea jambo fulani kuhusiana na hilo.—Yohana 2:1-12.

Yesu alienda kwa Yohana ili abatizwe, kisha akawa Mtiwa-Mafuta wa Mungu, au Masihi. (Luka 3:21, 22) Kisha akaanza kuchagua wanafunzi wake. Ingawa kazi yake ilipaswa kufanywa haraka, bado alipata wakati wa kufurahia pamoja na familia na rafiki zake. Akiwa pamoja na mama yake, wanafunzi wake, na ndugu zake, alienda kwenye karamu ya harusi huko Kana, mji ambao inaelekea ulikuwa kwenye kilima umbali wa kilomita 13 kutoka Nazareti. Sherehe ilipokuwa ikiendelea, Maria alitambua tatizo fulani. Labda aliona baadhi ya watu wa familia ya bwana na bibi arusi wakitazamana kwa wasiwasi huku wakinong’onezana. Walikuwa wameishiwa na divai! Kulingana na utamaduni wao, upungufu huo ungeaibisha familia hiyo, na kuharibu tukio hilo kabisa. Maria aliwahurumia, kisha akamgeukia Yesu.

Akamwambia Yesu hivi: “Hawana divai.” Alitazamia Yesu afanye nini? Tunaweza kuwazia alichotaka, lakini tunachojua ni kwamba alijua mwanawe ni mtu mkuu ambaye angefanya mambo makubwa. Labda alitazamia aanze sasa. Ni kana kwamba alikuwa akimwambia, “Mwanangu, tafadhali wasaidie!” Kwa kweli alishangazwa na jibu la Yesu. Alimwambia: “Nina nini nawe, mwanamke?” Maneno ya Yesu hayakuwa ya kukosa heshima, kama watu fulani wanavyofikiri. Hata hivyo, maneno yake yalikuwa na ushauri fulani. Yesu alikuwa akimkumbusha mama yake kwamba hakuwa na daraka la kuongoza huduma yake; lilikuwa daraka la Baba yake, Yehova.

Maria alikubali ushauri wa mwanawe, kwa sababu alikuwa mwanamke mnyenyekevu aliyeelewa mambo haraka. Akawageukia wale waliokuwa wakiwahudumia watu na kuwaambia: “Lolote atakalowaambia, fanyeni.” Maria alitambua kwamba hakupaswa kumwongoza mwanawe, badala yake, yeye pamoja na wengine walipaswa kufuata mwongozo wa Yesu. Naye Yesu alionyesha kwamba kama mama yake, aliwahurumia bwana na bibi-arusi. Alifanya muujiza wake wa kwanza kwa kugeuza maji yakawa divai bora. Matokeo yalikuwaje? “Wanafunzi wake wakamwamini.” Maria pia akamwamini Yesu. Hakumwona tu sasa kama mwanawe bali kama Bwana na Mwokozi wake.

Leo, wazazi wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa imani ya Maria. Ni kweli kwamba hakuna mtu ambaye amewahi kumlea mtoto aliye kama Yesu. Lakini mtoto anapokuwa mtu mzima huenda mabadiliko hayo yakatokeza hali ngumu. Huenda mzazi akawa na mwelekeo wa kumtendea mwana au binti yake kama mtoto mdogo, ingawa huenda hilo lisimpendeze mtoto wake. (1 Wakorintho 13:11) Mzazi anawezaje kuwasaidia watoto wake ambao ni watu wazima? Njia moja ni kuonyesha ana hakika kwamba mwana au binti yake ataendelea kufuata kanuni za Biblia na hivyo kupokea baraka za Yehova. Watoto ambao ni watu wazima wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa mzazi mwenye imani na usadikisho. Bila shaka, katika miaka iliyofuata Yesu alithamini kuungwa mkono na mama yake.

“NDUGU ZAKE WALIKUWA HAWAMWAMINI”

Vitabu vya Injili vinasema machache sana kumhusu Maria wakati wa miaka mitatu na nusu ya huduma ya Yesu. Hata hivyo, kumbuka kwamba inaelekea alikuwa mjane, mama asiye na mwenzi, labda bado alikuwa na watoto nyumbani. Tunaelewa kama hakuweza kumfuata Yesu alipokuwa akihubiri maeneo mbalimbali. (1 Timotheo 5:8)  Lakini aliendelea kutafakari mambo ya kiroho aliyokuwa amejifunza kuhusu Masihi na kuhudhuria mikutano katika sinagogi la kwao kama familia yao ilivyozoea kufanya.Luka 2:19, 51; 4:16.

Hivyo basi inaelekea kwamba Maria alikuwepo Yesu alipozungumza kwenye Sinagogi huko Nazareti. Alisisimka sana kumsikia mwanawe akitangaza kwamba sasa alikuwa ametimiza unabii kuhusu Masihi uliotabiriwa miaka mingi mapema! Hata hivyo, alivunjika moyo sana kuona kwamba wakazi wa Nazareti hawakumkubali mwanawe. Hata walijaribu kumuua Yesu!Luka 4:17-30.

Pia, Maria alivunjwa moyo na jinsi wanawe walivyomwona Yesu. Kwenye andiko la Yohana 7:5 tunaona kwamba ndugu wanne wa Yesu hawakuwa na imani kama ya mama yao. Tunasoma hivi: “Ndugu zake walikuwa hawamwamini.” Biblia haisemi mengi kuhusu dada za Yesu, ambao huenda walikuwa wawili. * Vyovyote vile, Maria alijua uchungu wa kuishi katika nyumba yenye watu walio na imani tofauti. Alihitaji kujitahidi kuwa mshikamanifu kwa Mungu na wakati uleule kushirikiana na watu wa familia yake na kuheshimu msimamo wao.

Pindi moja, kikundi cha watu wa ukoo, bila shaka kutia ndani ndugu za Yesu, waliamua kwenda “kumshika” Yesu. Walikuwa wakisema: “Amerukwa na akili.” (Marko 3:21, 31) Bila shaka, Maria hakufikiria hivyo, lakini aliwafuata wanawe, labda akitazamia kwamba wangejifunza jambo ambalo lingewasaidia kusitawisha imani. Je, walijifunza? Ingawa Yesu aliendelea kufanya miujiza na kufundisha kweli zenye kustaajabisha, ndugu zake hawakumwamini. Je, Maria alihangaika, hata karibu akate tamaa akijiuliza jinsi ambavyo angewashawishi?

Je, unaishi katika nyumba iliyo na watu wenye imani tofauti? Unaweza kujifunza mengi kutokana na imani ya Maria. Hakuacha kuwasaidia watu wake wa ukoo wasioamini. Badala yake, aliacha wajionee kwamba imani yake ilimletea shangwe na amani moyoni. Kwa upande mwingine, aliendelea kumuunga mkono mwanawe. Je, alimkosa Yesu? Je, nyakati nyingine alitamani kuwa na Yesu nyumbani pamoja na familia yake? Ikiwa ndivyo, alidhibiti hisia hizo. Aliliona kuwa pendeleo kumuunga mkono na kumtia moyo Yesu. Je, wewe pia unaweza kuwasaidia watoto wako ili watangulize kumtumikia Mungu maishani?

“UPANGA MREFU UTAICHOMA NAFSI YAKO”

Je, Maria alithawabishwa kwa kumwamini Yesu? Sikuzote Yehova huwathawabisha watu wenye imani, na bila shaka alimbariki Maria. (Waebrania 11:6) Hebu wazia alivyohisi aliposikia mwanawe akizungumza au kusikia habari kuhusu mahubiri yake kutoka kwa watu waliomsikia.

Mifano mingi ya Yesu inaonyesha jinsi alivyotumia mambo aliyojifunza kutoka kwa Yosefu na Maria

Katika mifano ambayo Yesu alitumia je, Maria alitambua mambo fulani ambayo Yesu alijionea utotoni huko Nazareti? Yesu alipozungumza kuhusu mwanamke anayefagia nyumba ili kutafuta sarafu iliyopotea, akisaga unga ili aoke mkate, au kuwasha taa na kuiweka juu ya kinara je, Maria alimfikiria yule mvulana mdogo aliyekuwa kando yake alipofanya mambo hayo? (Luka 11:33; 15:8, 9; 17:35) Yesu aliposema kwamba nira yake ni laini na mzigo wake ni mwepesi je, Maria alikumbuka siku moja alasiri miaka mingi iliyopita alipoona Yosefu akimfundisha Yesu jinsi ya kutengeneza nira kwa uangalifu ili isimwumize mnyama? (Mathayo 11:30) Bila shaka, Maria aliridhika sana alipotafakari pendeleo ambalo Yehova alikuwa  amempa maishani, pendeleo la kusaidia kulea na kumzoeza mwana ambaye angekuwa Masihi. Kwa kweli, alipata shangwe ya pekee alipomsikiliza Yesu, mwalimu mkuu zaidi ambaye alitumia vitu na matukio hayo ya kawaida kufundisha mambo muhimu!

Hata hivyo, Maria aliendelea kuwa mnyenyekevu. Mwanawe hakuwahimiza watu wamsifu-sifu, wala kumwabudu. Wakati wa huduma yake, mwanamke fulani alimwambia Yesu kwa sauti kwamba lazima mama yake alikuwa mwenye furaha kwa kumzaa. Yesu alimjibu hivi: “Hapana, badala yake, wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:27, 28) Na watu fulani katika umati walipomwambia Yesu kwamba mama na ndugu zake walikuwa karibu, alisema watu walioamini ndio waliokuwa mama na ndugu zake. Badala ya kukasirika, bila shaka Maria alimwelewa Yesu, mahusiano ya kiroho ni muhimu kuliko mahusiano ya kimwili.—Marko 3:32-35.

Hata hivyo, haiwezekani kuelezea hisia za Maria alipomwona mwanawe akiteseka na kufa juu ya mti wa mateso. Baadaye, mtume Yohana ambaye alijionea Yesu akifa aliandika jambo hili: Wakati wa tukio hilo, Maria alikuwa amesimama “kando ya mti wa mateso wa Yesu.” Hakuna kitu ambacho kingemzuia mama huyo mshikamanifu na mwenye upendo kusimama kando ya mwanawe mpaka mwisho. Yesu alimwona Maria, na ingawa kila mara alipopumua alihisi maumivu na haikuwa rahisi kuzungumza, alijikaza kusema. Alimpa mtume Yohana daraka la kumtunza mama yake. Kwa kuwa bado ndugu za Yesu hawakuwa waamini, Yesu alimpa mwamini mwenzake jukumu la kumtunza Maria. Hivyo, Yesu alionyesha jinsi ilivyo muhimu kwa mwanamume mwenye imani kutunza familia yake, hasa inapohusu mahitaji ya kiroho.—Yohana 19:25-27.

Hatimaye, Yesu alipokufa, Maria alihisi uchungu uliokuwa umetabiriwa, yaani, kuchomwa na upanga mrefu wa majonzi. Ikiwa tunashindwa kuwazia majonzi yake, basi ni vigumu kuelewa shangwe aliyohisi siku tatu baadaye! Maria alisikia kuhusu muujiza mkubwa zaidi, Yesu alikuwa amefufuliwa! Na shangwe yake ilizidi kwa sababu baadaye Yesu alimtokea Yakobo ndugu yake wa kambo, bila shaka akiwa peke yake. (1 Wakorintho 15:7) Jambo hilo liliwachochea Yakobo na ndugu wengine wa kambo wa Yesu. Baadaye tunasoma kwamba walikuja kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo. Baada ya muda walikuwa katika mikutano ya Kikristo pamoja na mama yao, “wakidumu katika sala.” (Matendo 1:14) Hatimaye wawili kati yao, Yakobo na Yuda, waliandika vitabu vya Biblia.

Maria alifurahi kuona wanawe wakigeuka na kuwa Wakristo washikamanifu

Maria anatajwa mara ya mwisho akiwa kwenye mkutano akisali pamoja na wanawe. Simulizi kuhusu Maria linaisha kwa njia nzuri, akituwekea mfano bora wa kuiga! Imani yake ilimsaidia kukabiliana na upanga wa majonzi na mwishowe akathawabishwa. Tukiiga imani yake, sisi pia tutakabiliana na maumivu ambayo ulimwengu huu mwovu unatuletea, na tutapata thawabu kubwa ajabu!

^ fu. 8 Baada ya kutajwa katika tukio lililotokea Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, Yosefu hatajwi tena kwenye masimulizi ya Injili. Baadaye, mama ya Yesu na vilevile ndugu na dada zake wanatajwa lakini Yosefu hatajwi. Pindi moja Yesu anaitwa “mwana wa Maria” bila Yosefu kutajwa.Marko 6:3.

^ fu. 16 Yosefu hakuwa baba mzazi wa Yesu, basi ndugu na dada za Yesu walikuwa ndugu na dada zake wa kambo.Mathayo 1:20.