Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE,MWISHO UMEKARIBIA?

“Mwisho”—Unamaanisha Nini?

“Mwisho”—Unamaanisha Nini?

Unaposikia maneno, “Mwisho umekaribia!” nini huja akilini mwako? Je, wewe huwazia mhubiri shupavu aliye jukwaani akihubiri kwa ishara nyingi na sauti kubwa huku akiwa na Biblia mkononi? Au je, unafikiria kuhusu mzee mwenye ndevu nyingi aliyesimama kando ya barabara, akiwa amevaa vazi refu na amejifunga kamba kiunoni, akiwa na bango lenye ujumbe kuhusu siku ya maangamizi? Kufikiria mambo hayo huwafanya watu fulani washikwe na hofu, watilie shaka au hata kuwachekesha.

Biblia inasema kwamba: ‘Mwisho utakuja.’ (Mathayo 24:14) Tukio hilo pia linaitwa “ile siku kuu ya Mungu” na “Har–Magedoni.” (Ufunuo 16:14, 16) Ni kweli kwamba watu wengi wamechanganywa na mafundisho ya kidini na uvumi mwingi na wenye kutisha kuhusu jambo hilo. Hata hivyo, Biblia inaeleza wazi ukweli kuhusu mwisho kwa kufafanua kikamili maana ya mwisho. Neno la Mungu linatusaidia pia kujua ikiwa mwisho umekaribia. Zaidi ya hayo, Biblia inatufundisha jinsi tunavyoweza kuokoka mwisho huo! Kwanza, acheni turekebishe baadhi ya maoni yasiyofaa kuhusu mwisho na kufafanua maana ya mwisho. Kulingana na Biblia, “mwisho” unamaanisha nini?

MWISHO HAUMAANISHI NINI?

  1. MWISHO HAUMAANISHI DUNIA KUCHOMWA MOTO.

    Biblia inasema hivi: “[Mungu] ameiwekea dunia msingi juu ya mahali pake palipofanywa imara; haitatikiswa mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Andiko hilo na mengine, yanatuhakikishia kwamba Mungu hataiharibu dunia wala hataruhusu kamwe iharibiwe!—Mhubiri 1:4; Isaya 45:18.

  2. MWISHO SI TUKIO LISILO NA RATIBA.

    Biblia inasema kwamba mwisho ni tukio lililopangwa, yaani Mungu ameweka wakati hususa wa kuleta mwisho. Tunasoma hivi: “Kuhusu siku ile au saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba. Endeleeni kutazama, endeleeni kukesha, kwa maana hamjui wakati uliowekwa ni gani.” (Marko 13:32, 33) Ni wazi kwamba, Mungu (“Baba”) ametenga “wakati uliowekwa” atakapoleta mwisho.

  3. MWISHO HAUTALETWA NA WANADAMU AU JIWE FULANI LA ANGANI LITAKALOGONGA DUNIA.

    Mwisho utaletwa na nani? Ufunuo 19:11 inasema hivi: “Nami nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli.” Mstari wa  19 unaendelea kusema hivi: “Nami nikamwona yule mnyama-mwitu na wafalme wa dunia na majeshi yao wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake.” (Ufunuo 19:11-21) Ingawa maneno hayo ni ya mfano, tunaweza kujua hili: Mungu atatuma jeshi la malaika ili kuwaangamiza adui zake.

Ujumbe wa Biblia kuhusu mwisho ni habari njema wala si habari mbaya

MWISHO UNAMAANISHA NINI?

  1. MWISHO WA SERIKALI ZA WANADAMU.

    Biblia inaeleza hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Kama ilivyotajwa katika fungu lililotangulia, “wafalme wa dunia na majeshi yao,” ambao watakuwa “wamekusanyika pamoja ili kupigana vita na yule anayeketi juu ya farasi na jeshi lake,” wataangamizwa.—Ufunuo 19:19.

  2. MWISHO WA VITA, JEURI, NA UKOSEFU WA HAKI.

    “[Mungu] anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:9) “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” (Methali 2:21, 22) “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”—Ufunuo 21:4, 5.

  3. MWISHO WA DINI AMBAZO HAZIKUMPENDEZA MUNGU WALA KUWASAIDIA WANADAMU.

    “Manabii wenyewe kwa kweli wanatoa unabii kwa uwongo; nao makuhani wanakandamiza kulingana na nguvu zao. . . . Nanyi mtafanya nini mwisho wake?” (Yeremia 5:31) “Wengi wataniambia siku hiyo, ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Na hata hivyo nitawaambia waziwazi: ‘Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.’”—Mathayo 7:21-23.

  4. MWISHO WA WATU WANAOENDELEZA NA KUUNGA MKONO MAMBO YA ULIMWENGU.

    Yesu Kristo alisema hivi: “Basi huu ndio msingi wa hukumu, kwamba nuru imekuja ulimwenguni lakini watu wamelipenda giza kuliko nuru, kwa maana matendo yao yalikuwa maovu.” (Yohana 3:19) Biblia inaeleza kuhusu uharibifu wa ulimwengu wa kale katika kipindi alichoishi mwanamume mwaminifu, Noa. “Ulimwengu wa wakati huo uliangamia kwa gharika ya maji. Lakini kwa neno hilohilo mbingu na dunia za sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zinahifadhiwa mpaka ile siku ya hukumu na ya kuangamizwa kwa watu wasiomwogopa Mungu.”—2 Petro 3:5-7.

Ona kwamba “siku ya hukumu na ya kuangamizwa” inayokuja inalinganishwa na “ulimwengu” wa siku za Noa. Ni ulimwengu gani ulioangamizwa? Dunia yetu haikuharibiwa; bali “watu wasiomwogopa Mungu” yaani, adui za Mungu ndio ‘walioangamia.’ Katika “siku ya hukumu” atakayoleta Mungu, adui za Mungu wataangamizwa. Lakini rafiki za Mungu wataokolewa kama ilivyokuwa kwa Noa na familia yake.—Mathayo 24:37-42.

Hebu wazia jinsi dunia itakavyopendeza baada ya Mungu kuondoa uovu wote! Ni wazi kwamba ujumbe wa Biblia kuhusu mwisho ni habari njema wala si habari mbaya. Hata hivyo, huenda bado ukawaza hivi: ‘Je, Biblia inasema mwisho utakuja lini? Je, uko karibu? Ninawezaje kuokoka mwisho huo?’