Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SWALI LA 2

Kwa Nini Ninahangaishwa Sana na Jinsi Ninavyoonekana?

Kwa Nini Ninahangaishwa Sana na Jinsi Ninavyoonekana?

KWA NINI NI MUHIMU

Kuna mambo mengine ya maana zaidi kuliko jinsi unavyoonekana kwa nje.

WEWE UNGEFANYA NINI?

Fikiria hali hii: Julia anapojitazama kwenye kioo, anaona kwamba yeye ni mnene sana. Anajiambia, “Ninahitaji kupunguza uzito.” Jambo la kushangaza ni kwamba wazazi wake na marafiki wake wanamwambia yeye ni mwembamba sana.

Hivi karibuni, Julia amekuwa akifikiria kuchukua hatua kali za kupunguza “kilo mbili tu.” Anachohitaji kufanya ni kujinyima chakula kwa siku kadhaa . . .

Ikiwa ungehisi kama Julia anavyohisi, ungefanya nini?

TUA NA UFIKIRI!

Huenda maoni yako kuhusu mwonekano wako yakawa kama mtu anayejitazama kwenye kioo kinachopotosha umbo

Si vibaya kuhangaikia jinsi unavyoonekana. Hata Biblia inasema kwamba wanawake na wanaume fulani walikuwa wenye kuvutia sana kama vile Sara, Raheli, Abigaili, Yosefu, na Daudi. Biblia inasema kwamba mwanamke fulani aliyeitwa Abishagi alikuwa “mrembo zaidi.”—1 Wafalme 1:4.

Hata hivyo, vijana wengi wanahangaikia mwonekano wao kupita kiasi. Kufanya hivyo kunaweza kutokeza matatizo mabaya sana. Fikiria:

  • Katika uchunguzi mmoja, asilimia 58 ya wasichana walidai kwamba wao ni wanene sana, ijapokuwa asilimia 17 tu kati yao ndio waliokuwa wanene sana.

  • Katika uchunguzi mwingine, asilimia 45 ya wanawake ambao ni wembamba sana walifikiri kwamba wao ni wanene sana!

  • Vijana fulani wametamani sana kupunguza uzito hivi kwamba wamepata ugonjwa wa kujinyima chakula ambao unahatarisha uhai, unaoitwa anoreksia.

Ikiwa una dalili za anoreksia au ugonjwa mwingine unaohusiana na kula, omba msaada. Anza kwa kuzungumza na mzazi wako au mtu mzima mwingine anayeaminika. Biblia inasema hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

Njia Bora Zaidi ya Kuboresha Mwonekano Wako!

Kwa kweli, jinsi mtu alivyo kwa ndani humfanya awe mwenye kupendeza au asiyependeza. Mfikirie Absalomu, mwana wa Mfalme Daudi. Biblia inasema hivi:

“Hakuna mwanamume aliyekuwa na sura nzuri sana . . . kuweza kusifiwa sana hivyo. Hakuwa na kasoro yoyote.”—2 Samweli 14:25.

Lakini kijana huyo alikuwa mwenye kiburi, alijitakia makuu, na alikuwa mwenye hila. Kwa hiyo, Biblia haimsifu Absalomu; inamtaja kuwa mtu asiye mshikamanifu hata kidogo na mwenye chuki ya uuaji.

Inafaa kwamba Biblia inatupa ushauri huu:

“Mjivike utu mpya.”—Wakolosai 3:10.

“Kujipamba kwenu kusiwe kule . . . kwa nje . . . , bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni.—1 Petro 3:3, 4.

Ingawa si vibaya kutamani kuwa na umbo lenye kupendeza, jambo la maana zaidi ni utu wako. Kwa kweli, kuwa na sifa za kiroho kutakusaidia uwe mwenye kupendeza machoni pa wengine kuliko kuwa na misuli yenye nguvu au umbo zuri! “Watu wanaweza kuvutiwa upesi na urembo wako,” anasema msichana anayeitwa Phylicia, “lakini watu watakukumbuka zaidi kwa sifa zako nzuri na jinsi ulivyo kwa ndani.”

CHUNGUZA JINSI UNAVYOONEKANA

Je, mara nyingi unajikuta huridhishwi na jinsi unavyoonekana?

Je, umewahi kufikiria kufanyiwa upasuaji au kufuata ratiba kali ya kula ili kurekebisha kasoro fulani mwilini?

Ikiwa ungeweza, ungebadili nini katika mwili wako? (Chagua kile ambacho ungependa kubadili.)

  • KIMO

  • UZITO

  • NYWELE

  • UMBO

  • USO

  • RANGI

Ikiwa umejibu ndiyo maswali ya kwanza mawili na kuchagua vitu vitatu au zaidi katika swali la tatu, fikiria jambo hili: Kuna uwezekano mkubwa kwamba wengine hawakuoni kwa njia isiyofaa kama unavyojiona. Ni rahisi kuhangaishwa kupita kiasi na jinsi unavyoonekana.—1 Samweli 16:7.