Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 2

Paradiso Yapotea

Paradiso Yapotea

Malaika mwasi amchochea mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, waukatae utawala wa Mungu. Dhambi na kifo zaingia ulimwenguni

MUDA mrefu kabla ya kuwaumba wanadamu, Mungu aliumba viumbe wengi wa kiroho wasioonekana—malaika. Katika bustani ya Edeni, malaika mwasi, ambaye baadaye alikuja kuitwa Shetani Ibilisi, alimshawishi kwa hila Hawa ale tunda la ule mti ambao Mungu alikuwa amewakataza.

Akimtumia nyoka kuzungumza, Shetani alidai kwamba Mungu alikuwa akimnyima mwanamke huyo na mume wake kitu fulani chenye kutamanika. Malaika huyo alimwambia Hawa kwamba yeye na mume wake wakila tunda hilo hawatakufa. Hivyo, Shetani alidai kwamba Mungu aliwadanganya watoto wake wa kibinadamu. Mdanganyi huyo alifanya ionekane kana kwamba kumwasi Mungu ni jambo lenye kupendeza ambalo lingewapa ujuzi na uhuru mwingi zaidi. Huo ulikuwa uwongo, uwongo wa kwanza duniani. Suala kuu lilikuwa enzi au utawala wa Mungu—iwapo Mungu ana haki ya kutawala na ikiwa anaitumia ifaavyo.

Hawa alimwamini Shetani. Akaanza kutamani tunda hilo, kisha akala sehemu yake. Baadaye akampa mume wake, naye pia akala. Hivyo wakawa watenda-dhambi. Tendo hilo lililoonekana kuwa dogo lilikuwa uasi. Kwa kukataa kimakusudi kutii amri ya Mungu, Adamu na Hawa waliukataa utawala wa Muumba aliyekuwa amewapa kila kitu, kutia ndani uhai mkamilifu.

“Atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.”—Mwanzo 3:15

Mungu aliwahukumu waasi hao. Alitabiri Uzao au Mkombozi aliyeahidiwa ambaye angemharibu Shetani, anayewakilishwa na nyoka. Kwa kutotekeleza hukumu ya kifo papo hapo, Mungu aliwaonyesha rehema wazao wa Adamu na Hawa ambao hawakuwa wamezaliwa. Watoto hao wangekuwa na tumaini kwa kuwa Yule ambaye Mungu angemtuma, angeondolea mbali madhara ya uasi huo katika Edeni. Hatua kwa hatua, kadiri Biblia ilivyoendelea kuandikwa, ilijulikana wazi Mwokozi huyo ni nani, na jinsi atakavyotimiza kusudi la Mungu.

Mungu alimfukuza Adamu na Hawa kutoka katika Paradiso. Walilazimika kutoa jasho na kuchoka ili kujiruzuku nje ya bustani ya Edeni. Kisha Hawa akawa mja-mzito na kumzaa Kaini, mtoto wa kwanza wa Adamu na Hawa. Wazazi hao wa kwanza walipata wana na mabinti wengine, kutia ndani Abeli na Sethi, babu ya Noa.

—Inatoka kwenye Mwanzo sura ya 3 mpaka 5; Ufunuo 12:9.