Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 22

Mitume Wahubiri kwa Ujasiri

Mitume Wahubiri kwa Ujasiri

Kutaniko la Kikristo laongezeka licha ya mateso

SIKU kumi baada ya Yesu kurudi mbinguni, wanafunzi wake 120 hivi walikusanyika katika nyumba fulani jijini Yerusalemu wakati wa Sikukuu ya Kiyahudi ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K. Ghafula, katika nyumba hiyo kukawa na kelele kama ile ya upepo wenye nguvu unaovuma. Wanafunzi wakaanza kuzungumza lugha ambazo hawakuwa wanazijua. Iliwezekanaje? Mungu alikuwa amewapa wanafunzi roho takatifu.

Nje, kulikuwa na umati kwa sababu watu walikuwa wametoka sehemu mbalimbali ili kusherehekea sikukuu hiyo. Walishangaa kuwasikia wanafunzi wa Yesu wakizungumza kwa ufasaha lugha zao wenyewe. Akieleza yaliyotokea, Petro alirejelea unabii wa Yoeli kwamba Mungu ‘angemimina’ roho yake, ambayo ingewawezesha wenye kuipokea kufanya miujiza. (Yoeli 2:28, 29) Uthibitisho huo wenye nguvu wa roho takatifu ulionyesha wazi kwamba badiliko kubwa limetokea: Mungu ameacha kushughulika na taifa la Israeli na kuanza kushughulika na kutaniko jipya la Kikristo lililokuwa limeanzishwa. Sasa, wote waliotaka kumtumikia Mungu walipaswa kuwa wafuasi wa Kristo.

Wakati huohuo upinzani uliongezeka, nao adui wakawatupa wanafunzi gerezani. Hata hivyo, wakati wa usiku, malaika wa Yehova alifungua milango ya gereza na kuwaambia wanafunzi waendelee kuhubiri. Ilipofika asubuhi wakaendelea kuhubiri. Wakaingia hekaluni na kuanza kufundisha habari njema kumhusu Yesu. Wapinzani wao wa kidini walikuwa na hasira nao wakawaagiza waache kuhubiri. Mitume wakajibu kwa ujasiri: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:28, 29.

Mateso yakaongezeka. Wayahudi fulani walimshtaki mwanafunzi Stefano wakidai kwamba amekufuru, nao wakamuua kwa kumpiga kwa mawe. Kijana, anayeitwa Sauli wa Tarso, alikuwa akitazama na kukubaliana na mauaji hayo. Kisha akaenda Damasko kumkamata mfuasi yeyote wa Kristo. Sauli akiwa njiani, nuru kutoka mbinguni ilimulika kumzunguka na akasikia sauti: “Sauli, Sauli, kwa nini unanitesa?” Akiwa amepofushwa na nuru hiyo, Sauli akauliza: “Wewe ni nani?” Sauti hiyo ikasema: “Mimi ni Yesu.”—Matendo 9:3-5.

Siku tatu baadaye, Yesu alimtuma mwanafunzi anayeitwa Anania ili kumponya Sauli. Sauli akabatizwa na kuanza kuhubiri kwa ujasiri kumhusu Yesu. Baadaye, Sauli akaitwa mtume Paulo naye akawa Mkristo mwenye bidii wa kutaniko la Kikristo.

Wanafunzi wa Yesu walikuwa wakiwatangazia habari njema za Ufalme wa Mungu Wayahudi na Wasamaria pekee. Sasa malaika amtokea Kornelio, ofisa-jeshi Mroma, anayemwogopa Mungu na kumwambia awatume watu wakamwite mtume Petro. Akiwa pamoja na wengine, Petro akamhubiria Kornelio na watu wa nyumbani mwake. Petro alipokuwa akizungumza, roho takatifu ikaja juu ya waamini hao kutoka kwa Mataifa, naye akaagiza wabatizwe katika jina la Yesu. Tangu wakati huo na kuendelea, watu wa mataifa yote wangeweza kupata uzima wa milele. Kutaniko lilikuwa tayari kuhubiri habari njema kwa mapana na marefu.

—Inatoka kwenye Matendo 1:1–11:21.