Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SEHEMU YA 8

Waisraeli Waingia Kanaani

Waisraeli Waingia Kanaani

Waisraeli waitwaa nchi ya Kanaani wakiongozwa na Yoshua. Yehova atumia waamuzi kuwakomboa watu wake kutoka mikononi mwa adui zao

KARNE nyingi kabla ya Waisraeli kuingia Kanaani, Yehova alikuwa ameahidi kwamba wazao wa Abrahamu wangeimiliki nchi hiyo. Wakiongozwa na Yoshua, sasa Waisraeli wako tayari kuimiliki Nchi ya Ahadi.

Mungu aliamua Wakanaani wanastahili kuangamizwa. Walikuwa wameijaza nchi mazoea machafu ya ngono na umwagaji wa damu kimakusudi. Hivyo, majiji ya Kanaani yaliyokuwa yametwaliwa na Waisraeli yalipaswa kuharibiwa kabisa.

Hata hivyo, kabla ya kuingia nchi hiyo, Yoshua aliwatuma wapelelezi wawili. Wapelelezi hao walikaa katika nyumba ya Rahabu jijini Yeriko. Rahabu aliwapokea na kuwalinda, ingawa alijua ni Waisraeli. Rahabu alimwamini Mungu wa Waisraeli kwa sababu alikuwa amesikia jinsi Yehova alivyokuwa ametenda ili kuwakomboa watu wake. Aliwaambia wapelelezi hao wamwapie kwamba yeye na watu wa nyumba yake hawataangamizwa.

Baadaye, Waisraeli walipoingia Kanaani na kulizunguka Yeriko, Yehova aliangusha kuta za Yeriko kimuujiza. Vikosi vya Yoshua vikaingia ndani na kuliharibu jiji hilo, hata hivyo, Rahabu na familia yake hawakuangamizwa. Kisha, kwa miaka sita tu, Yoshua akatwaa sehemu kubwa ya Nchi ya Ahadi. Baadaye, makabila ya Israeli yakagawiwa nchi hiyo.

Akikaribia mwisho wa utumishi wake wa muda mrefu kwa Mungu, Yoshua aliwakusanya watu pamoja. Akawaambia jinsi Yehova alivyoshughulika na babu zao, kisha akawatia moyo wamtumikie Yehova. Hata hivyo, baada ya Yoshua na wanaume wazee kufa, Waisraeli walimwacha Yehova, wakaanza kutumikia miungu ya uwongo. Kwa miaka 300 hivi, taifa hilo halikushikamana kabisa na sheria za Yehova. Wakati huo, Yehova aliruhusu Waisraeli wakandamizwe na adui zao, kama vile Wafilisti. Lakini Waisraeli walipomwomba Yehova msaada, aliweka rasmi jumla ya waamuzi 12 wawakomboe.

Kipindi cha Waamuzi wanaotajwa katika kitabu cha Waamuzi kilianza siku za Othnieli mpaka siku za Samsoni, mwanadamu mwenye nguvu zaidi aliyepata kuishi. Ukweli wa msingi unaothibitishwa tena na tena katika masimulizi yenye kusisimua ya kitabu cha Biblia cha Waamuzi ni: Kumtii Yehova huleta baraka, kutotii huleta msiba.

—Inatoka kwenye Yoshua; Waamuzi; Mambo ya Walawi 18:24, 25.