Hamia kwenye habari

Anaendelea Kuwa na Bidii Licha ya Ulemavu

Anaendelea Kuwa na Bidii Licha ya Ulemavu

 Virginia ni Shahidi wa Yehova ambaye ana ulemavu unaomzuia kufanya jambo lolote isipokuwa kusogeza macho yake (LIS). Mwili wake umepooza. Anaweza kuona na kusikia, kufumba na kufumbua macho, na kusogeza kichwa chake kidogo sana. Hawezi kuzungumza wala kula. Zamani alikuwa na afya nzuri na mwenye nguvu. Lakini asubuhi moja mnamo 1997, alihisi maumivu makali nyuma ya kichwa chake ambayo yaliendelea kwa muda mrefu. Mume wake alimpeleka hospitalini, kisha usiku huo Virginia akapoteza fahamu. Aliamka majuma mawili baadaye akiwa kwenye chumba cha wagonjwa mahututi akiwa amepooza na akiwa ameunganishwa kwenye mashini ya kumsaidia kupumua. Kwa siku kadhaa, hangeweza kukumbuka chochote, hata hangeweza kukumbuka yeye ni nani.

 Virginia anaeleza kilichotokea baada ya hapo. “Hatua kwa hatua kumbukumbu zangu zilianza kurudi. Nilisali kwa kuendelea. Sikutaka kufa nimwache mwana wangu akiwa bila mama. Ili kujipa ujasiri, nilijaribu kukumbuka mistari mingi ya Biblia kadiri nilivyoweza.

 “Hatimaye, madaktari walinihamisha kutoka kwenye chumba cha wagonjwa mahututi. Baada ya miezi sita katika hospitali na vituo mbalimbali vya afya, niliruhusiwa kwenda nyumbani. Bado nilikuwa nimepooza kabisa, na nilihitaji kupata msaada wa kufanya kila kitu. Nilivunjika moyo sana. Nilijihisi nikiwa bure mbele za Yehova na watu wengine. Nilikuwa na wasiwasi kwamba nisingeweza kumtunza mwanangu.

 “Nilianza kusoma kuhusu masimulizi ya Mashahidi wengine ambao walikuwa wamekabiliana na hali kama yangu na nikashangazwa na mambo waliyoweza kutimiza kwa ajili ya Yehova. Kwa sababu hiyo, nilijaribu kusitawisha mtazamo mzuri kwa kukazia mambo ambayo ningeweza kutimiza. Kabla ya kuwa mgonjwa, nilikuwa nikitumia muda mfupi tu kufanya mambo ya kiroho. Sasa nilikuwa na siku nzima kila siku. Kwa hiyo, badala ya kukata tamaa, nilikazia fikira sababu zilizonifanya nijitoe kwa Yehova.

 “Nilijifunza kutumia kompyuta. Ninachapa kwa kutumia programu inayotenda kupatana na jinsi kichwa changu kinavyosogea. Inachosha lakini teknolojia hiyo huniwezesha kujifunza Biblia na kuwaeleza wengine kuhusu tumaini langu kwa kuandika barua na barua-pepe. Ili kuwasiliana na watu wanaonizunguka, nina ubao ulioandikwa herufi zote. Mtu niliye naye huelekeza kidole kwenye herufi moja baada ya nyingine. Akichagua isiyofaa, ninafungua macho yangu; anapochagua herufi sahihi mimi hufumba macho. Tunafanya hivyo hadi maneno na sentensi zinakamilika. Baadhi ya akina dada ambao hutumia muda mwingi pamoja nami wamekuwa stadi wa kutambua ninachotaka kusema. Pindi fulani wanapokosea na kufikiri nilitaka kusema neno tofauti, tunacheka sana.

Kuwasiliana kwa kutumia ubao ulio na herufi za alfabeti

 “Ninafurahi sana kuhusishwa katika utendaji wa kutaniko. Sikuzote mimi huunganishwa kwa ajili ya mikutano, siku hizi ninafanya hivyo kupitia video iliyounganishwa kwenye mtandao. Ninaweza kuchapa maelezo yangu kisha mtu mwingine anayasoma kwenye sehemu ya maswali na majibu. Pia mimi hujiunga na kikundi kidogo cha Mashahidi ili kutazama programu ya kila mwezi ya JW Broadcasting. a

 “Nimekabiliana na ugonjwa huu wa kupooza kwa miaka 23 sasa. Nyakati nyingine mimi huhuzunika. Lakini ninafaulu kukabiliana na pindi hizo kwa kusali, kushirikiana na akina ndugu, na kwa kuendelea kuwa na bidii kiroho. Kwa kweli, kwa msaada wa kutaniko langu, nimefaulu kufanya upainia msaidizi kwa zaidi ya miaka sita. Nimejaribu kuwa mfano mzuri kwa mwanangu, Alessandro, ambaye sasa amefunga ndoa na anatumikia akiwa mzee. Akiwa pamoja na mke wake, wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida.

 “Mara nyingi mimi hutafakari mambo nitakayoweza kufanya katika paradiso wakati ujao. Jambo la kwanza ambalo ningependa kufanya ni kuzungumza kumhusu Yehova kwa kutumia sauti yangu mwenyewe. Ningependa kutembea kando ya kijito kilicho kijijini ili kufurahia mandhari maridadi. Na kwa kuwa nimekuwa nikilishwa vyakula vya majimaji kwa kutumia mrija kwa zaidi ya miaka 20, nina hamu kubwa ya kuchuma tofaa kutoka kwenye mti na kuuma tunda hilo. Na bila shaka, kwa kuwa mimi ni Mwitaliano, ninatazamia kwa hamu kutayarisha na kula vyakula vya Kiitaliano ninavyovipenda zaidi, kutia ndani piza!

 “‘Tumaini la wokovu’ limesaidia kulinda akili yangu. (1 Wathesalonike 5:8) Kujiona katika ulimwengu mpya kumenipa shangwe licha ya udhaifu wangu wa kimwili ambao nina uhakika utakwisha hivi karibuni. Naam, ninasubiri kwa hamu kufurahia ‘uzima ulio wa kweli’ ambao Yehova ameahidi kutupatia kupitia Ufalme wake.”—1 Timotheo 6:19; Mathayo 6:9, 10.

a Kiunganishi cha kuingia JW Broadcasting kinaweza kupatikana kwenye jw.org.