Hamia kwenye habari

Kasisi Apata Majibu

Kasisi Apata Majibu

Siku moja, Shahidi wa Yehova anayeitwa Eliso alikuwa akiongoza funzo la Biblia katika nyumba ya mwanamke anayependezwa wakati ambapo mwanamke huyo alipata wageni wasiotarajiwa. Kasisi mmoja alikuwa amekuja kumtembelea akiwa na mke wake. Eliso alikuwa amepata habari kwamba wenzi hao wa ndoa walikuwa wamempoteza mwana wao wa pekee katika kifo.

Eliso alipowapa pole kwa sababu ya kifo cha mwana wao, yule kasisi na mke wake walianza kulia kwa uchungu. Kisha kasisi huyo akasema hivi kwa hasira: “Siwezi kuelewa kwa nini Mungu aliruhusu jaribu kama hilo litupate! Angewezaje kumchukua mwana wangu na sina mtoto mwingine? Nimekuwa nikimtumikia Mungu kwa miaka 28, nikitenda mambo mengi mema, na sasa ananilipa kwa njia hii! Kwa nini Mungu alimuua mwanangu?”

Eliso aliwaeleza wenzi hao wa ndoa kwamba Mungu hakumchukua mwana wao. Pia alizungumzia habari kama vile fidia, ufufuo, na sababu inayomfanya Mungu aruhusu mambo mabaya yatukie. Kasisi huyo na mke wake walimwambia Eliso kwamba alikuwa amewapa majibu waliyokuwa wakisali wapate.

Juma lililofuata kasisi huyo na mke wake walirudi na kujiunga na mwanamke huyo alipokuwa akijifunza Biblia. Eliso alikuwa akizungumzia sura yenye kichwa “Tumaini Hakika kwa Wapendwa Wako Ambao Wamekufa,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Wenzi hao wa ndoa walishiriki mazungumzo hayo kwa hamu.

Baadaye wote wawili walihudhuria kusanyiko la pekee la Mashahidi wa Yehova lililofanywa Tbilisi, Georgia, na waliguswa moyo sana na upendo na umoja wa pekee ambao walijionea—sifa ambazo kwa muda mrefu walikuwa wamejaribu kuwasaidia washiriki wa kanisa lao wawe nazo, lakini hawakufanikiwa.