Hamia kwenye habari

Jumba la Ufalme Linanufaishaje Jamii Yako?

Jumba la Ufalme Linanufaishaje Jamii Yako?

Kwa zaidi ya karne moja, Mashahidi wa Yehova wamechora ramani na kujenga majengo yao ya ibada. Je, kuna jengo lolote la ibada linalojengwa katika eneo lenu linaloitwa Jumba la Ufalme? Jumba la Ufalme linaweza kuleta manufaa gani katika eneo lenu?

Flowery Branch, Georgia, Marekani.

“Zawadi Nzuri kwa Jamii”

Majumba ya Ufalme yamebuniwa kwa njia inayofanya eneo livutie. Jason, anayesaidia kuratibu ujenzi wa Majumba ya Ufalme nchini Marekani, alisema hivi: “Lengo letu ni kila Jumba la Ufalme liwe mojawapo ya majengo yenye kuvutia na yanayoheshimiwa katika eneo.” Shahidi ambaye ni mhandisi anayefanya kazi ya usanifu alisema hivi: “Tunataka jengo likikamilika liwe zawadi nzuri kwa jamii na liwe lenye kupendeza katika eneo.”

Wajenzi wa Majumba ya Ufalme ni Mashahidi wa Yehova, wanaopendezwa kikweli na ujenzi unaozingatia viwango bora. Mara nyingi kazi yao inatambuliwa na watu wengine. Kwa mfano, katika mradi wa karibuni jijini Richmond, Texas, Marekani, mkaguzi wa majengo wa eneo hilo alisema kwamba paa la Jumba la Ufalme ni zuri sana kuliko paa zote alizowahi kukagua. Katika kisiwa cha Jamaika, mkaguzi wa majengo alikipeleka kikundi kipya cha wakaguzi katika eneo la mradi wa ujenzi wa Jumba la Ufalme na kuwaambia hivi: “Hamhitaji kuwa na wasiwasi kuhusu watu hawa. Mashahidi wa Yehova hufuata kikamili ramani ya ujenzi, na hata majengo yao yanajengwa kwa viwango vya juu vya ujenzi kuliko viwango vilivyowekwa kwa ajili ya eneo hili.” Mkaguzi mmoja wa majengo katika jiji la Florida, Marekani, alisema hivi: “Nimekagua hospitali nyingi na miradi mikubwa ya serikali lakini hakuna mradi wowote wenye utaratibu mzuri kama huu. Ninyi mnafanya kazi nzuri sana.”

Concession, Zimbabwe

Matokeo Mazuri kwa Majirani

Mikutano inayofanywa katika Jumba la Ufalme inawasaidia watu wanaohudhuria kuwa na maisha yanayofaa. Wahudhuriaji wamekuwa wakisaidiwa kuwa baba, mama, na watoto bora. Rod, ambaye anafanya kazi na kikundi kinachoshughulikia uchoraji wa Majumba ya Ufalme alisema hivi: “Kila Jumba la Ufalme ni kituo cha elimu ambacho kinawachochea watu wawe na viwango vya juu vya maadili ambavyo vinanufaisha jamii zote.” Akaongezea hivi: “Eneo hili ni mahali ambapo unaweza kupata msaada unapokabiliana na changamoto za maisha. Watu katika Jumba la Ufalme ni wachangamfu na wana urafiki ambao unawavutia na kuwanufaisha wale wote wanaohitaji faraja na msaada wa kiroho.”

Wale wanaokutana katika Jumba la Ufalme wanawajali majirani wao, na wanawasaidia kwa haraka wanapopatwa na majanga. Kwa mfano, katika mwaka wa 2016 baada ya Kimbunga Matthew kupiga Bahamas, Mashahidi wa Yehova walirekebisha nyumba 254. Katika eneo fulani, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 80 anayeitwa Violet, ambaye nyumba yake ilikumbwa na mafuriko, alikwenda kwenye kikundi cha Mashahidi waliokuwa wakifanya kazi ya kutoa msaada. Aliahidi kuwapa kiasi chochote cha pesa ambacho wangehitaji ili kumsaidia. Lakini walikataa pesa zake na badala yake, kikundi hicho kilimsaidia kubadili vigae katika paa la nyumba yake lililokuwa likivuja. Wakarekebisha dari ya chumba chake. Baada ya kumaliza kazi, Violet alimkumbatia kila mtu katika kikundi hicho, akiwashukuru mara nyingi na kusema kwa msisimuko, “Kwa kweli nyinyi ni watu wa Mungu!”

Bad Oeynhausen, North Rhine-Westphalia, Ujerumani

‘Tunashukuru Kwamba Jumba la Ufalme Lipo Katika Eneo Letu’

Ili kufanya Jumba la Ufalme lidumu likiwa katika hali nzuri, Mashahidi wa Yehova huandaa programu za kuwazoeza washiriki wa kutaniko kudumisha majumba yao. Hilo limekuwa na matokeo mazuri. Kwa mfano, katika eneo la Arizona lenye watu wachache, mwanamke fulani alikubali mwaliko wa kuhudhuria mkutano katika Jumba la Ufalme. Alipendezwa na jinsi jumba lilivyodumishwa vizuri na alishangaa kusikia kuhusu programu ya udumishaji iliyohusisha kuchukua hatua kuboresha jengo likiwa katika hali nzuri. Mwanamke huyo alikuwa mwandishi wa jarida la habari la mji, na baadaye jarida hilo la habari lilitia ndani makala iliyokuwa na ripoti kuhusu Jumba la Ufalme linalodumishwa vizuri. Makala hiyo ilimalizia kwa kueleza hivi: “Tunashukuru kwamba . . . Jumba la Ufalme lipo katika eneo la jamii yetu.”

Unaweza kupata Majumba ya Ufalme katika maeneo ya watu wa jamii mbalimbali duniani pote. Unakaribishwa kwa moyo mkunjufu ututembelee. Uwe na uhakika utakaribishwa kwa uchangamfu.