Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sababu Gani Musikiaji wa Sala Anawaacha Watu Wateseke?

Sababu Gani Musikiaji wa Sala Anawaacha Watu Wateseke?

Sababu Gani Musikiaji wa Sala Anawaacha Watu Wateseke?

HATA ikiwa watu fulani wanasali, hawaamini kabisa kama Mungu iko. Sababu gani? Labda ni kwa sababu wanaona mateso mengi katika dunia. Je, umekwisha kujiuliza sababu gani Mungu anawaacha watu wateseke?

Je, kweli Mungu ndiye aliwafanya watu wawe namna walivyo leo—maana yake, wasio wakamilifu na wenye kuteseka? Ikiwa Mungu aliwaumba watu ili wateseke, basi hastahili heshima yetu, sivyo? Wazia mufano huu: Ikiwa unapendezwa na motokari fulani mupya lakini unaona kama inapondekana upande fulani, je, utasema kama mutengenezaji aliitengeneza ikiwa yenye kupondekana hivyo? Hapana! Bila kusita utasema kama mutengenezaji alipoitengeneza ilikuwa “muzuri” lakini iliharibiwa na mutu ao kitu fulani.

Vilevile, unapoona namna vitu vilivyo katika ulimwengu vilivyoumbwa kwa utaratibu na ukilinganisha mambo hayo na mivurugo ao mambo maovu yanayowatesa wanadamu leo, unaweza kusema nini? Biblia inafundisha kama Mungu aliwaumba mwanaume na mwanamuke wa kwanza wakamilifu, lakini baadaye wao wenyewe wakapoteza ukamilifu wao na kuharibisha mambo. (Kumbukumbu la Torati 32:4, 5) Habari njema ni hii: Mungu anaahidi kama atatengeneza mambo, ni kusema, atafanya wanadamu wawe wakamilifu tena. Basi, sababu gani anaacha mateso kwa muda murefu hivi?

Sababu Gani Mungu Anawaacha Watu Wateseke kwa Muda Murefu Hivi?

Ni kwa sababu ya ulizo lililotokezwa kuhusu ni nani anayepaswa kutawala wanadamu. Yehova hakuumba watu ili wajitawale wenyewe. Yeye ndiye alipaswa kuwa Mutawala wao. Biblia inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Jambo la kuhuzunisha ni kwamba mwanaume na mwanamuke wa kwanza walikataa utawala wa Mungu. Tendo lao la kuvunja sheria liliwafanya kuwa watenda zambi. (1 Yohana 3:4) Kwa kufanya hivyo, wakapoteza ukamilifu na wakaanza kuteseka wao na watoto wao.

Kwa muda wa miaka mingi, Yehova amewaacha watu wajitawale wenyewe, na historia imeonyesha kama watu hawana uwezo wa kufanya hivyo. Inaonyesha kama serikali ao guvernema zote za dunia zimewatesa watu. Hakuna hata serikali moja ambayo imeweza kuondoa vita, matendo ya kuvunja sheria, ukosefu wa haki, ao magonjwa.

Namna Gani Mungu Ataondoa Mateso?

Biblia inaahidi kama hivi karibuni Mungu ataleta dunia mupya ya haki. (2 Petro 3:13) Ni wale tu wanaotumia vizuri uhuru wao wa kuchagua kwa kumupenda Mungu na kupenda watu wengine ndio wataruhusiwa kuishi katika dunia hiyo.​—Kumbukumbu la Torati 30:15, 16, 19, 20.

Tena Biblia inasema kama katika “siku ya hukumu” inayokaribia sana, Mungu ataondoa mateso yote na wale wanaoyaleta. (2 Petro 3:7) Kisha hapo, Yesu Kristo, Mufalme aliyewekwa na Mungu atatawala watu watiifu. (Danieli 7:13, 14) Utawala wa Yesu utafanyia watu nini? Biblia inasema hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”​—Zaburi 37:11.

Yesu, Mufalme wa mbinguni, ataondoa mateso yote​—ni kusema, magonjwa, uzee, na kifo. Mateso hayo yalitokea kwa sababu wanadamu walikataa utawala wa Yehova, ‘chemuchemu ya uzima.’ (Zaburi 36:9) Yesu atawaponyesha wale wote wanaokubali utawala wake wenye upendo. Wakati atatawala dunia, ahadi hizi za Biblia zitatimia:

◼ ‘Hakuna mukaaji atakayesema: Mimi ni mugonjwa. Watu wanaokaa katika inchi hiyo watakuwa wamesamehewa kosa lao.’​—Isaya 33:24.

◼ “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”​—Ufunuo 21:4.

Inatia moyo sana kujua kama hivi karibuni Mungu atatimiza ahadi yake ya kuondoa mateso yote, sivyo? Kwa kungojea wakati huo, hatupaswe kukata tumaini na kusema kama Mungu hasikilize sala zetu kwa sababu tu anawaacha watu wateseke.

Mungu iko. Anaweza kusikia sala zako, hata unapomuelezea maumivu na huzuni yako. Na anapenda kabisa uishi wakati ambapo mashaka yako na maumivu yako yote vitakuwa vimekwisha.