Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Utu wa Mungu

Utu wa Mungu

Mungu ana mwili wa aina gani?

“Mungu ni Roho.” —Yohana 4:24.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inasema kwamba Mungu ni roho. (2 Wakorintho 3:17) Kwa sababu hiyo, yeye ni mkuu sana hivi kwamba hatuwezi kuwazia ukuu wake. Andiko la 1 Timotheo 1:17 linasema kwamba yeye ni “Mfalme wa umilele, asiyeweza kuharibika, asiyeonekana.” Biblia pia inasema: “Hakuna yeyote ambaye amemwona Mungu wakati wowote.”—1 Yohana 4:12.

Muumba wetu ni mkuu sana hivi kwamba hatuwezi hata kuanza kuwazia anavyoonekana. “Mnaweza kumfananisha Mungu na nani, nanyi mnaweza kuweka kando yake mfano gani?” inasema Isaya 40:18. Hata mbingu zenye kustaajabisha ni duni zikilinganishwa na Mweza-Yote.—Isaya 40:22, 26.

Hata hivyo kuna viumbe wenye akili ambao wanaweza kumwona Mungu na hata kuzungumza naye uso kwa uso. Hilo linawezekanaje? Linawezekana kwa sababu wao pia ni roho, na wanaishi mbinguni. (1 Wafalme 22:21; Waebrania 1:7) Yesu Kristo alisema hivi kuhusu viumbe hao wenye nguvu zinazopita za wanadamu, ambao pia wanaitwa malaika: “Sikuzote [wao] huuona uso wa Baba yangu aliye mbinguni.”—Mathayo 18:10.

 Je, Mungu yuko kila mahali?

“Basi, ninyi msali hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni.’” Mathayo 6:9.

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia haifundishi kwamba Mungu yuko kila mahali kama nguvu isiyo na utu. Badala yake, kama maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:9 na 18:10 yanavyoonyesha, Mungu ni mtu—ni “Baba”—na anaishi mbinguni, ‘makao yake yaliyofanywa imara.’—1 Wafalme 8:43.

Alipokuwa anakaribia kufa, Yesu alisema: “Ninauacha ulimwengu nami ninaenda kwa Baba.” (Yohana 16:28) Baada ya kufa akiwa mwanadamu na kufufuliwa akiwa roho, Kristo alipaa “mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele za uso wa Mungu.”Waebrania 9:24.

Mambo hayo ya hakika kumhusu Mungu ni muhimu. Kwa nini? Kwanza, kwa sababu Mungu ni mtu, tunaweza kujifunza kumhusu na kumkaribia. (Yakobo 4:8) Pia, ukweli kumhusu Mungu hutulinda dhidi ya ibada ya uwongo, kama vile kuabudu sanamu na vitu visivyo na uhai. “Watoto wadogo, jilindeni na sanamu,” linasema andiko la 1 Yohana 5:21.

Ni katika njia gani wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu?

“Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” —Mwanzo 1:27.

BIBLIA INASEMA NINI?

Sisi wanadamu tunaweza kuonyesha sifa za Mungu kama vile upendo, haki, na hekima. Kwa kweli, Biblia inasema hivi: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa, na endeleeni kutembea katika upendo.”—Waefeso 5:1, 2.

Mungu pia alituumba tukiwa na uhuru wa kuchagua, ambao unatuwezesha kuchagua yaliyo sawa badala ya yaliyo mabaya na kuwaonyesha wengine upendo katika njia mbalimbali. (1 Wakorintho 13:4-7) Pia tuna uwezo wa kuwa wabunifu, kufurahia umaridadi wa vitu, na kustaajabia ulimwengu unaotuzunguka. Zaidi ya yote, tumepewa uwezo wa kufahamu mambo ya kiroho, tamaa ya asili ya kujifunza kumhusu Muumba wetu na mapenzi yake kwetu.—Mathayo 5:3.

Jinsi kweli ya Biblia inavyoweza kukusaidia. Kadiri tunavyojifunza kumhusu Mungu na kumwiga, ndivyo tunavyoishi kwa njia aliyokusudia tuishi. Kwa kufanya hivyo, tunakuwa na shangwe zaidi maishani, na pia uradhi wa kweli na amani ya akili. (Isaya 48:17, 18) Mungu anajua kwamba sifa zake zenye kuvutia zinagusa mioyo ya watu, zinawavuta watu wenye mioyo minyofu kwake na kuwafanya wapate njia ya uzima wa milele.—Yohana 6:44; 17:3.